BARAZA LA MADIWANI WA JIJI LA ARUSHA LEO


Mkurugenzi wa jiji la Arusha,Juma Iddi akitolea ufafanuzi hoja mbalimbali za madiwani wa jiji la Arusha.
Diwani wa kata ya Sombetini, Ally Bananga, (CHADEMA) akichangia hoja kwenye kikao cha baraza
waandishi wa habari wakiwa wamekaa mbele ya madiwani wakati wa kikao cha baraza la madiwani
MADIWANI wa Halmashauri ya Jiji la Arusha wameagiza kukamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria aliyekuwa Daktari wa Jiji hilo,Ibrahim  Isack  kwa tuhuma za kujimilikisha vifaa vya zahanati ya Levelosi.
Aidha wameagiza kukamilishwa mara moja kwa wataratibu za kumwezesha aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa jiji, Estomih Chang’a, ambaye sasa ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mpanda, ili afike kutoa maelezo ya juu ya upotevu vifaa hivyo.

Akiongea kwenye kikao cha Baraza la Madiwani jana, Diwani wa kata ya levelos, Ephata nanyaro, (CHADEMA), alisema kuwa hakubaliani na majibu ya Mkurugenzi wa Jiji, Juma Iddi kuwa suala hilo liendelee kushighulikiwa kwenye kamati ya fedha kwani suala hilo limekuwa likishughulikiwa kwa miaka mitatu sasa bila kupata ufumbuzi.

“Mimi nina ushahidi, kwanza nilimuona  Dkt Ibrahim akipakia vile vifaa kwenye lori, pili nilifuatilia KCMC wakanipa barua kuonyesha hawakuchukua vile vifaa hata wale Wamarekani waliofadhili mradi  huo, (Familly Health International) wamenitumia barua pepe hawakuchukua vile vitu.

“Sasa tutakuwa tunajadili nini wakati huu ni wizi, hii ni jinai wanatakiwa wakamatwe wafikishwe polisi,” alisema Nanyaro wakati akijadili taarifa za utekelezaji zilizokuwa zikiwasilishwa.

Akiongea na waandishi wa habari Nanyaro alisema kuwa vifaa hivyo vilikuwa vikitumiwa na KCMC kwa ajili ya kutafiti magonjwa ambukizi ikiwemo HIV ambapo mradi huo ulikuwa ukifadhiliwa na FHI, ambapo waliomba eneo kwa Halamshauri ya jiji kwa makubaliano kuwa mradi huo ukikamilika wataacha vifaa.

Nanyaro alisema kuwa halmashauri waliwapa eneo kwenye eneo la zahanati ya levelos  ambapo mradi huo ulianza 2008 na kukamilika julai, 2012 jambo alilodai kuwa baada ya hapo  Dkt Ibrahim aliamua kujitwalia vifaa hivyo kwa maelezo kuwa KCMC walivichukua wakati si kweli.

Alisema kuwa vitu hivyo ni vingi ingawa hakuwa anajua thamani yake ambapo alitaja baadhi kuwa ni pamoja na magari mawili, samani za ofisi, vifaa na samani za  maabara huku akidai Jenereta aliinusuru kwa yeye binafsi kuamua kuweka makufuli manne.

“Hapa wanadai kuwa Dkt Ibrahim hapatikani kupitia namba ya simu aliyowapa,  mimi ninaweza kuwaonyesha mahali alipo hata sasa kwani yuko hapahapa mjini, hata asubuhi nimemuona, wasipomkamata nitahamasisha wananchi wangu tumkamate tumepeleke polisi, Mkurugenzi akapeleke tuhuma zake,” alisisitiza Nanyaro.

Awali Mkurugenzi, Iddi alilieleza baraza hilo kuwa  wanasubiri majibu ya barua waliyomwandikia Katibu Mkuu wa TAMISEMI waliyomuomba amwagize mtumishi wake Chang’a kuja kujieleza mbele ya baraza la madiwani.
Alisema kuwa Dkt. Ibrahim alifika kwa ajili ya kujieleza kwenye baraza hilo Mei 15,mwaka huu lakini kikao hakikufanyika hivyo akaacha namba ya simu ambayo kwa siku nne mfululizo wamekuwa wakimpigia hawampati.

“Tatizo kwa sasa ni kuwa kule Ngorongoro, Dkt, Ibrahim kasimamishwa kazi kutokana na masuala mengine yanayofanana na haya mnayomtafutia, hivyo hata muajiri wake inamuia vigumu kumpata, inawezekana ameamua kuzima simu kabisa baada ya tume iliyokuwa ikimchunguza kuja kutuhoji na huku kuhusu masuala haya  ila tunaendelea kumtafuta,” alisema Iddi.

Alimtaka diwani, Nanyaro kuwakabidhi vielelezo alivyonavyo ili waone namna watakavyoweza kumchukulia hatua za kisheria Dkt Ibrahim baada ya mwanasheria wa jiji kuvifanyia kazi.


0 Comments:

Post a Comment