Na Queen Lema, Arusha

 

MKOA wa Arusha unatarajiwa kusimama miguu yote miwili kesho Agosti Mosi, wakati Princess Lounge, moja ya kumbi maarufu na zenye mvuto mkubwa wa kipekee barani Afrika Mashariki, itakapofanya maadhimisho makubwa ya kutimiza mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake.


 Akizungumza kuelekea tukio hilo la kihistoria, Mkurugenzi wa Princess Lounge, Catherine Urasa, amesema wameandaa sherehe kubwa na ya kukata na shoka itakayoweka historia mpya ya burudani mkoani Arusha.

Catherine amebainisha kuwa tangu kuanzishwa kwake, Princess imekuwa nguzo kuu na kichocheo kikubwa cha sekta ya burudani, huku ikisifika kwa kulisha vyema hisia za wapenda bata na starehe mkoani hapa.

Alieleza kuwa kwa kuzingatia Arusha ni kitovu cha utalii nchini, Princess Lounge imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kwenda sambamba na hadhi hiyo kwa kutoa burudani na huduma za kiwango cha kimataifa zinazovutia wageni wa ndani na nje ya nchi.


"Tunatimiza mwaka mmoja sasa wenye mafanikio makubwa sana. Tunafurahi kwa upendo na mapokezi tuliyopata, na tunapenda kuwaahidi wateja wetu kuwa tumejipanga vyema zaidi kuendeleza na kuiboresha sekta hii ya burudani kwa viwango vya juu zaidi," alisema kwa kujiamini Catherine.


Katika hatua nyingine, Mkurugenzi huyo amejivunia namna biashara hiyo ilivyoweza kuwa mkombozi kwa vijana kwa kutengeneza fursa za ajira kwa wale ambao hapo awali hawakuwa na kazi kabisa.


"Kama mnavyojionea wenyewe, hapa tuna mabinti warembo na wachapakazi ambao ni sehemu ya nembo yetu. Pia tuna vijana mahiri wa muziki (DJs) na wataalamu wa kuchoma nyama tamu na zenye ladha ya kipekee, ambao wote kwa pamoja ndio siri na nguzo ya mafanikio ya Princess," aliongeza.


Kufuatia hatua hiyo, Catherine ametoa wito na mwaliko rasmi kwa Watanzania wote na wakazi wa jiji la Arusha kujitokeza kwa wingi kesho kusherehekea kwa pamoja mafanikio hayo, ambapo kutakuwa na mfululizo wa burudani za kusisimua, vinywaji vya kila aina, na vyakula vya kutosha.



Maafisa na askari  wa jeshi la Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro waliopoteza maisha, kujeruhiwa na kufanya kazi kwa uhodari wametunukiwa vyeti na fedha kutokana na kujitoa kwao kwa hali na mali kulinda rasilimali za wanyamapori na misitu.



Tuzo hizo zimetolewa tarehe 31 Julai 2026 kwenye maadhimisho ya  siku ya  askari wanyamapori duniani ambayo huadhimishwa kwa lengo la kuutambua mchango wa  askari hao katika kulinda rasilimali za nchi na kuenzi mchango wa Askari 10 waliopoteza maisha yao na kujeruhiwa wakiwa kazini katika hifadhi ya Ngorongoro.



Naibu kamishna wa Uhifadhi huduma za shirika Aidan Makala  amewapongeza askari wote wa jeshi la uhifadhi kutokana na  kujitoa kwa hali na mali katika kazi hiyo huku akiwasisitiza kufanya kazi kwa kushirikiana na wananchi ili kulinda matakwa ya haki jinai.



Naibu Kamishna Makala ameleza kuwa,  askari  wa  uhifadhi ni nguzo ya ulinzi wa rasilimali za wanyamapori  na misitu ambapo  kazi hiyo haiishii kukabiliana na ujangili pekee  bali inakwenda sambamba na kudhibiti uharibifu wa mazingira hususan vyanzo vya maji, ulinzi wa maisha na mali za watu dhidi ya wanyamapori wakali na waharibifu na kuelimisha jamii kutunza rasilimali hizo.

 


Akielezea kuhusu maadhimisho ya siku ya  askari wanyamapori duniani, Afisa Uhifadhi mkuu anayesimamia idara ya huduma za Ulinzi Bw. Emmaanuel Kaaya amesema kuwa Siku hiyo ilianza kuadhimishwa mwaka 2007, kwa ushirikiano baina ya Shirikisho la Kimataifa la Askari wa Wanyamapori (International Rangers Federation - IRF) na mashirika mengine ya kimataifa. 


Lengo la kuanzishwa kwa maadhimisho haya ni kuutambua mchango wa Askari wa Wanyamapori na kuuenzi mchango wa Askari waliopoteza maisha wakiwa kazini. Ni siku ya kuwatambua na kuenzi mchango wa mashujaa wanaojitolea kila siku kuhakikisha hifadhi zetu zinaendelea kuwa salama kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vizazi vijavyo.


Kwa upande wake kamishna msaidizi mwandamizi wa Uhifadhi Gloria Bideberi amebainisha kuwa katika maadhimisho haya, Mamlaka imetoa vyeti na fedha taslimu  kwa zaidi ya watumishi 30 ikiwa ni sehemu ya kuutambua mchango wao katika kazi kwa kipindi cha mwaka 2025/26.


Maadhimisho hayo yalipambwa na michezo mbalimbali iliyojumuisha  mpira wa miguu, kukimbiza kuku, mazoezi ya viungo na maonesho ya kwata mbalimbali.

 



Mkuu wa Mkoa wa Arusha, CPA Amos Gabriel Makalla, ametoa agizo zito kwa wananchi wote waliolipwa fidia kupisha ujenzi wa miundombinu ya barabara za kujiandaa na Michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2027). 

Agizo hilo linalenga kumpa nafasi mkandarasi kuendelea na kazi hiyo bila vikwazo.


Makalla alitoa agizo hilo kufuatia ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya ujenzi na upanuzi wa miundombinu hiyo yenye urefu wa kilometa 9.1. Mradi huu mkubwa unatekelezwa kwa njia nne na Serikali kwa gharama ya shilingi Bilioni 87.9.

Maeneo Yanayohusika na Upanuzi wa Barabara
Mradi huo unajumuisha maeneo muhimu yafuatayo jijini Arusha:

  • Makutano ya Ngarenaro – Mzunguko wa Kisongo
  • Makutano ya Ngarenaro – Kona ya Nairobi

  • Makutano ya Ngarenaro – Soko la Kilombero
  • Kauli ya RC CPA Amos Makalla
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Makalla alimshukuru Rais kwa kutoa fedha hizo na kuwasihi wadau wote kushirikiana ili kukamilisha mradi huo kwa wakati.

"Nimshukuru  Rais kwa kuwezesha ujenzi wa barabara hizi, niwaombe watalamu wa sekta zote kutoa ushirikiano kuhakikisha hakuna kizuizi kwa Mkandarasi kufanya kazi. Serikali ishawalipa fidia wananchi wote kwa barabara zote za AFCON. Zaidi ninawashukuru ambao wameshaondoka, wameonesha uzalendo, na ambao hawajaondoka niwaombe waondoke ili kupisha ujenzi."

Manufaa Makubwa ya Mradi Huu Jijini Arusha
Kukamilika kwa miundombinu hii kutaleta mapinduzi makubwa kiuchumi na kijamii katika Jiji la Arusha:
Kuchochea Utalii na AFCON 2027: Barabara hizi zitakuwa kiungo muhimu wakati wa michuano na zitaboresha sekta ya utalii.
  1. Kupunguza Msongamano: Zitasaidia kwa kiasi kikubwa kutatua changamoto ya foleni za magari jijini Arusha.
  2. Kutokomeza Mafuriko: Meneja wa TANROADS Mkoa wa Arusha, Mhandisi Reginald Massawe, amebainisha kuwa mradi huu utajenga mitaro mikubwa ya kupeleka maji Mto TANAPA. Hii itaondoa kabisa kero ya mafuriko katika maeneo ya Majengo, Shamsi, na Ngarenaro.
Ujenzi huu ni hatua kubwa kuelekea maandalizi ya AFCON 2027 na maboresho ya kudumu ya Jiji la Arusha.


SHIRIKA la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limeingia kwenye hatua kubwa ya kuimarisha ulinzi na doria angani baada ya Kamishna wa Uhifadhi, Massana G. Mwishawa, kukagua ndege ndogo mbili (2) mpya aina ya Savannah zilizonunuliwa hivi karibuni.



Ndege hizo zimenunuliwa kupitia mradi unaofadhiliwa na BMZ, uliotekelezwa chini ya Wizara ya Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo ya Ujerumani. Lengo kuu la ununuzi huo ni kuongeza nguvu katika doria na uhifadhi wa wanyamapori kwenye Hifadhi za Taifa za Serengeti na Nyerere.


Ukaguzi huo umefanyika leo katika Karakana iliyopo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, Zanzibar, ambapo ndege hizo zinaendelea kuunganishwa tayari kwa kazi.


Akiwa uwanjani hapo, Kamishna Mwishawa amewapongeza mafundi wanaoendelea na kazi ya uunganishwaji wa ndege hizo kwa umakini mkubwa.


Pia, ametoa pongezi za kipekee kwa marubani wawili (2) ambao ni Askari Uhifadhi wa TANAPA. Marubani hao kwa sasa wapo kwenye hatua za mwisho za mafunzo yao maalum ya kurusha ndege hizo ili kuhakikisha usalama na ufanisi wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.


Ndege hizo za kisasa aina ya Savannah zinatarajiwa kuanza doria rasmi angani mwanzoni mwa mwezi Oktoba, 2026, hatua itakayosaidia kwa kiasi kikubwa kudhibiti ujangili na kulinda rasilimali za taifa.

 



Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro Abdul-Razaq Badru ameuambia mkutano wa 48 wa kamati ya Urithi wa Dunia kuwa Ngorongoro ni sehemu pekee ambayo binadamu duniani kote wanaweza kupata ushahidi sahihi wa chimbuko la asili ya binadamu.



Akizungumza mjini Busan,Jamhuri ya Korea wakati akiongoza Mkutano wa pembeni (Side event) ulioandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kupata uelewa wa pamoja kuhusu hali ya uhifadhi wa eneo la  Hifadhi ya Ngorongoro ambayo ni eneo la Urithi wa Dunia, Badru amesema Ngorongoro ina ushahidi uliohifadhiwa wa nyayo za binadamu na masalia ya kale katika eneo la Laetoli na Olduvai zinazothibitisha suala hilo.


“Ngorongoro si tu eneo la utalii bali pia ni mahali ambapo historia ya binadamu wote kisayansi ilianzia”, alisema kamishna Badru.


Katika kikao hicho ameeleza kuwa kila nyayo iliyohifadhiwa ndani ya hifadhi ya Ngorongoro inawakumbusha kurudi nyumbani kuona historia hiyo.


Badru amefafanua  kuwa Ngorongoro ni sehemu ambayo binadamu alianzia kutumia zana mbalimbali za mawe kama teknolojia ya awali ya shughuli za kibinadamu na ndipo alipoanza kufanya harakati za kimaisha.


Mkutano wa kamati ya Urithi wa Dunia una lengo la kufanya maamuzi kuhusu maeneo mapya yanayopendekezwa kuingizwa kwenye Orodha ya Urithi wa Dunia na kuimarisha juhudi za pamoja za kulinda, kuhifadhi, na kusimamia kwa uendelevu maeneo yenye thamani kubwa ya kiutamaduni na asili duniani.

 


WANANCHI wa Kijiji cha Manyire, Kata ya Mlangarini mkoani Arusha, wameanza rasmi ujenzi wa shule yao ya sekondari. Hatua hii inaleta ukombozi mkubwa wa kielimu na kumaliza changamoto ya muda mrefu ya wanafunzi kutembea umbali mrefu.


Utekelezaji wa mradi huo umeanza kushika kasi kufuatia Serikali kutoa fedha za awamu ya kwanza. Tayari mradi umekabidhiwa rasmi, ambapo wananchi kwa kushirikiana na mkandarasi wapo kazini kuchimba msingi wa majengo ya shule hiyo.

Diwani wa Kata ya Mlangarini, Emanuel Mrema, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka mradi huo unaogusa maisha ya wananchi.

"Ujenzi wa shule hii ni faraja kubwa kwa wananchi wa Manyire ambao kwa miaka mingi walikosa shule ya sekondari karibu. Watoto wetu walilazimika kutembea hadi kilomita 24 kila siku kufuata masomo, jambo lililoathiri mahudhurio na maendeleo yao kitaaluma," alisema Mrema.

Mrema alimpongeza Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, Dkt. Johannes Lukumayi, kwa juhudi zake za kupigania mradi huo bungeni. Pia aliishukuru Halmashauri ya Wilaya ya Arusha chini ya Mkurugenzi Mtendaji, Bw. Selemani Msumwi, kwa ushirikiano uliowezesha mradi kuanza.


Alibainisha kuwa vijana wa eneo hilo wamejitokeza kwa wingi kushiriki hatua za awali za ujenzi. Diwani huyo aliwasisitiza wananchi kuendelea kushirikiana na kulinda miradi ya maendeleo kwa faida ya vizazi vya sasa na vijavyo.

"Watoto wetu hawapaswi kurithi migogoro au visasi. Wanapaswa kurithi miradi ya maendeleo itakayoboresha maisha yao na kuwasaidia kufikia ndoto zao," alihitimisha Mrema.

 


Mwambata wa ubalozi wa Oman nchini Tanzania, Abdulrahman Salim Algaad akiwa na familia yake, ametembelea Hifadhi ya Ngorongoro na kushuhudia maajabu ya utalii yaliyopo katika kivutio namba moja cha utalii barani afrika

 


Akimpokea mwambata huyo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia Huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameeleza kuwa jitihada za mamlaka hiyo kuwafikia wadau mbalimbali zimeendelea kuzaa matunda ambapo watumishi kutoka balozi mbalimbali ndani na nje ya nchi wamendelea kutembelea hifadhi hiyo.

 


Akiwa ndani ya hifadhi hiyo, Abdulrahman Algaad na familia yake walipata fursa ya kushuhudia wanyamapori adimu wakiwa katika mazingira yao ya asili, wanyamapori wakubwa watano, misitu, maporomoko ya maji, urithi wa utamaduni na mambo kale, makumbusho ya urithi geopark na kueleza kuwa ndoto na hisia alizokuwa nazo zimekutana na uhalisia.

 

Mwambata huyo ameonyesha kuvutiwa na uzuri wa Hifadhi ya Ngorongoro na vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania na kupongeza hatua za uhifadhi zinazofanyika na kuifanya Ngorongoro kuendelea kuheshimika kimataifa na kuwa eneo la urithi wa dunia lenye hadhi tatu za kimataifa.

 


Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia huduma za utalii na masoko, Mariam Kobelo amebainisha kuwa ziara za viongozi na maafisa wa kidiplomasia wanaotembelea Ngorongoro zinachangia kuitangaza Tanzania kimataifa, kuimarisha ushirikiano katika sekta ya utalii, kuongeza ushirikiano kupitia diplomasia ya uchumi.

 

Happy Lazaro, Arusha.

Serikali imeweka bayana kuwa mafanikio ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yatategemea kwa kiwango kikubwa mchango wa Mawakili wa Serikali, hususan katika kusimamia masuala ya kisheria yanayohusu miradi mikubwa ya maendeleo na uwekezaji.



Akifunga mafunzo maalumu ya siku tatu kwa Mawakili wa Serikali yaliyofanyika jijini Arusha, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Zainab Katimba, amesema wakati umefika kwa mawakili hao kuwa zaidi ya washauri wa sheria na kuwa wadau muhimu wa maendeleo ya Taifa kupitia utaalamu wao.



Ameeleza kuwa mafunzo hayo yamekusudiwa kuwajengea uwezo wa kukabiliana na changamoto mpya zinazojitokeza katika mazingira ya utawala na uchumi, huku akiwataka kutumia maarifa waliyoyapata kuboresha usimamizi wa mikataba, utoaji wa ushauri wa kisheria na utatuzi wa migogoro kwa kuzingatia maslahi mapana ya nchi.



Kwa mujibu wa Katimba, Serikali inahitaji wataalamu wa sheria wanaoweza kufanya uchambuzi wa kina, kufikiri kimkakati na kuhakikisha kila mkataba au uamuzi wa kisheria unalinda rasilimali za Taifa na kuchangia ukuaji wa uchumi.



Amesema anaamini washiriki wa mafunzo hayo watakuwa chachu ya mabadiliko katika taasisi wanazotoka na wataongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao, hatua itakayosaidia kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.



Naye Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Samwel M. Maneno, amesema programu hiyo imeandaliwa kwa kuzingatia mahitaji ya sasa ya taaluma ya sheria, ikijumuisha mada kuhusu mikataba ya kimkakati, ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP), usimamizi wa vihatarishi vya kisheria, usuluhishi wa migogoro pamoja na matumizi ya Akili Unde (AI) katika utoaji wa huduma za kisheria.



Aidha, amewataka  Mawakili wa Serikali kuendelea kuyafanyia kazi maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhusu kuongeza ubora wa utendaji wa taaluma ya sheria, ikiwa ni pamoja na kusoma na kuyatumia mafunzo yaliyomo katika kitabu Mama Samia Doctrine of Law ili kuimarisha uchambuzi wa masuala ya kisheria na usimamizi wa mikataba ya Serikali.



Mafunzo hayo ya Bespoke 2026, yaliyobeba kaulimbiu "Repositioning State Attorneys for Strategic Legal Leadership in Realizing Tanzania Development Vision 2050," yaliwakutanisha Mawakili wa Serikali kutoka wizara, taasisi, wakala na mamlaka za serikali za mitaa kwa lengo la kuongeza ufanisi wa uongozi wa kisheria katika kusukuma mbele ajenda ya maendeleo ya Taifa.



 


Bodi ya Wakurugenzi Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro ikiongozwa na makamu Mwenyekiti Dkt. Harriet Mtae jana tarehe 11 julai, 2026 imekagua uboreshaji wa miundombinu ya utalii eneo la Nyayo za Laetoli lililopo hifadhi ya Ngorongoro 



Wakiwa Laetoli Wakurugenzi hao wamekagua uhifadhi wa Nyayo zilizogundulika katika eneo hilo miaka zaidi ya milioni 3.6 iliyopita na kuangalia hatua za utekelezaji wa mradi wa Geopark unaohusisha ujenzi wa jengo la kupokelea wageni, jengo la kupumzika wageni, jengo lililojengwa kwa ajili ya kuhifadhi Nyayo sambamba na miundombinu mingine.


Naibu Kamishna wa Uhifadhi Joas Makwati anayesimamia uhifadhi, utalii na maendeleo ya jamii ameeleza kuwa ziara hiyo imelenga kutathmini utekelezaji wa miradi inayofanywa na mamlaka kwa lengo la kuimarisha shughuli za uhifadhi, kuboresha huduma za utalii na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Hifadhi ya Ngorongoro.



Pamoja na kukagua miundombinu ya utalii wakurugenzi hao wamepokea taarifa ya hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi hiyo pamoja na mipango ya kuendelea kuboresha mazingira ya utalii na shughuli za uhifadhi.


Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya NCAA, Dkt. Harieth Mtae, alisema miradi hiyo inaakisi dhamira ya mamlaka ya kuendelea kuwekeza katika uboreshaji wa vivutio vya utalii na kuongeza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wageni.





Ameongeza kuwa maboresho hayo yanatarajiwa kuongeza thamani ya vivutio vya utalii, kuvutia watalii zaidi na kuendelea kuitangaza Hifadhi ya Ngorongoro kama moja ya vivutio vinavyoongoza duniani.



 



Waziri wa maliasili na utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) leo tarehe 10 julai, 2026 amekutana na bodi ya wakurugenzi mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro katika ofisi za mamlaka hiyo zilizopo Karatu mkoani Arusha na kusisitiza umuhimu wa bodi hiyo kufuatilia kwa karibu shughuli zote za utendaji ili kuanza mwaka mpya wa fedha 2026/2027 kwa kasi na ufanisi.


Mhe. Kijaji amesema  kuwa bajeti ya mwaka mpya wa fedha inaanza na utekelezaji wa dira ya taifa ya maendeleo ya mwaka 2050 hivyo vikao vyake na bodi za taasisi zilizopo chini ya wizara vina lengo la kuanza utekelezaji wa dira, bajeti na ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa pamoja.


Ameitaka bodi hiyo kuongeza nguvu katika kuimarisha uhifadhi, kutangaza utalii  na kusimamia maendeleo ya jamii na kusisitiza kuwa jitihada hizo ziendane na kasi ya kukamilisha miundombinu wezeshi ikiwemo barabara kuu ya Loduare hadi Golini, kuimarisha mawasiliano ndani ya eneo lote la hifadhi, kukamilisha mradi wa fensi ya umeme ili kupunguza migongano kati ya wanyamapori na wananchi, kudhibiti ujangili na kuendelea kuimarisha mahusiano ya hifadhi na wananchi wanaoizunguka.


“Tulinde uhifadhi wa Ikolojia ya Ngorongoro kwa wivu mkubwa, tuendelee kubuni mazao mapya ya utalii na kuyatangaza, tujipange kikamilifu kuhakikisha Ngorongoro kama premium destination inawafikia na kuwashawishi wageni watakaohudhuria matukio ya AFCON, mkutano wa umoja wa Mabunge duniani, tuzo za  dunia za utalii na shindano la Miss world ambapo matukio yote yatafanyika Tanzania kati ya mwezi oktoba 2026 na Julai mwaka 2027”  amesisitiza Dkt. Kijaji.



Katibu wa Bodi, ambae ni kamishna wa Uhifadhi Ngorongoro Abdul-Razaq Badru amemueleza Mhe. waziri kuwa, Ngorongoro imepiga hatua ya kimageuzi kwenye mifumo ya kidijitali (ICT Transformation), uhifadhi endelevu kwa kuimarisha doria za kisasa, kuboresha miundombinu hasa barabara ya tabaka gumu kutoka geti la loduare hadi Seneto (km 29.5) kwa gharama ya TZS 80.3 bilioni  


Badru ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2025/26 eneo la Ngorongoro idadi ya watalii ilifikia 1,061,620 na fedha shilingi 269.5 Bilioni zilikusanywa. Ngorongoro imeendelea na jitihada za kulinda hadhi tatu za kimataifa kutoka UNESCO ambazo ni Urithi wa Dunia (World Heritage Site), Hifadhi ya Biosphere (Man and Biosphere Reserve), na Geopark ya Dunia (Ngorongoro-Lengai Global Geopark) ili ziendelee kuinufaisha nchi yetu.


Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi Ngorongoro Dkt. Harriet Mtae amemueleza Mhe waziri kuwa, katika kipindi cha miezi sita (06) iliyopita bodi ya Ngorongoro imetekeleza majukumu  kwa kuzingatia sheria, kanuni pamoja na maelekezo ya Serikali ili kuhakikisha Mamlaka inatekeleza kikamilifu dhamana yake ya kuhifadhi maliasili za Wanyamapori, malikale na urithi wa dunia, kuendeleza utalii endelevu na kuboresha shughuli za maendeleo ya jamii.

 


Tukio la Ngorongoro kuonesha vivutio vya utalii mubashara kupitia runings kubwa iliyofungwa katika banda la Wizara ya Maliasili na Utalii

limevutia wananchi wengi wanaotembelea  maonesho ya 50 ya biashara ya kimataifa jijini  Dar es Salaam kwa kuoneshwa maajabu yaliyopo Ngorongoro hususan Kreta ya Ngorongoro, makundi ya wanyama mbalimbali ikijumuisha pundamilia, nyumbu, swala, nyati na wanyama adimu kama  faru, simba, tembo na  na  chui na kujihisi kama wapo nyumbani Ngorongoro.



Afisa Uhusiano Mkuu wa Ngorongoro  Walter Mairo ameeleza kuwa  kupitia runinga iliyofungwa viwanja vya maonesho wageni wanaotembelea wanaona wanyama aina mbalimbali ndani ya Kreta, tambarare za Ndutu ambapo maisha ya Nyumbu kuzaliwa, kukua, kusafiri na kurejea na kuanza kizazi kipya kila mwaka


Mairo ameongeza kuwa, matukio mubashara yanaonesha wananchi jinsi teknolojia ya kidigitali na utalii wa asili vinavyoweza kushirikiana kuelimisha, kuburudisha na kuonyesha ushahidi kuwa Ngorongoro si tu hifadhi, bali ni jukwaa la kidunia linalounganisha urithi, biashara na teknolojia sehemu moja.


Karibu Sabasaba timu yetu yenye wabobezi na watopezi imejipanga kukupa  hadhithi za Ngorongoro zitakazokuduwaza kuwa Ngorongoro sio mahali pa kuangalia tu, bali mahali pa kuelewa, kujifunza na kuishi uzoefu usiosahaulika.

 



Na Mwandishi wa OTR


Kibaha, Pwani. Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) imejiwekea lengo la kukusanya Sh2 trilioni kama mapato yasiyo ya kodi katika mwaka huu wa fedha 2026/27, ikiwa ni zaidi ya lengo la Sh1.79 trilioni ambalo Serikali imeipa taasisi hiyo.



Akifungua Mkutano wa Pili wa Baraza la Wafanyakazi wa OTR uliofanyika Alhamisi, Julai 9, 2026, wilayani Kibaha, mkoani Pwani, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alisema kufikiwa kwa lengo hilo kutategemea kuongeza kasi ya utendaji, ubunifu, ushirikiano na uwajibikaji ndani ya OTR na katika taasisi na kampuni 308 zinazosimamiwa na ofisi hiyo.



"Ili tuweze kufikia lengo letu la kukusanya Sh2 trilioni katika mwaka wa fedha 2026/27, itatubidi tutanue mbavu na kutoa jasho zaidi," alisema Bw. Mchechu.


Alisisitiza kuwa mafanikio hayo yatawezekana ikiwa OTR itaendelea kujenga mazingira bora ya kazi, kuimarisha utamaduni wa taasisi unaovutia na kuhifadhi watumishi wenye uwezo, sambamba na kuhakikisha uwekezaji wa Serikali wenye thamani ya Sh92.3 trilioni unazalisha matokeo yanayoonekana kwa wananchi.



Katika mwaka wa fedha 2025/26, OTR ilikusanya Sh1.327 trilioni kama mapato yasiyo ya kodi, ikiwa ni ongezeko la asilimia 30 kutoka Sh1.028 trilioni zilizokusanywa mwaka 2024/25.



Kati ya kiasi hicho, gawio lilichangia Sh800.5 bilioni, sawa na asilimia 60 ya makusanyo yote; michango ya asilimia 15 ya mapato ghafi kutoka taasisi za umma zisizo za kibiashara ilifikia Sh406 bilioni, sawa na asilimia 30 ya makusanyo; huku mapato mengineyo, yakiwemo faida za uwekezaji na michango mingine inayotokana na umiliki wa Serikali, yakifikia Sh121.5 bilioni, sawa na asilimia 10 ya makusanyo yote.


"Wajibu wetu sasa ni kulinda mafanikio haya na kutoridhika na tulipofika. Tunapaswa kuhakikisha OTR inakuwa taasisi yenye uwezo na utayari wa kutekeleza wajibu wake mkubwa zaidi katika kusimamia uwekezaji wa umma na kuchangia utekelezaji wa Dira 2050," alisema.


Alisema tangu kuanza kwa mwaka mpya wa fedha Julai 1, 2026, matarajio ya Serikali, wananchi na wadau kuhusu mchango wa OTR katika uchumi yameongezeka.


"Ofisi ya Msajili wa Hazina ina ahadi na wajibu mkubwa kwa Serikali wa kuvuka viwango vya sasa vya gawio na michango, kuendelea kuongeza thamani ya uwekezaji wa Serikali na kuhakikisha mapato yasiyo ya kodi yanaendelea kukua," alisema.


Bw. Mchechu alisema azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuongeza mchango wa mapato yasiyo ya kodi hadi kufikia asilimia 10 ya mapato yote ya Serikali ifikapo mwaka 2030, kutoka wastani wa sasa wa takribani asilimia tatu.


Alisema kufikia lengo hilo kutahitaji taasisi zinazosimamiwa na OTR kuongeza tija, ufanisi na mapato, kuimarisha nidhamu ya kifedha, kupunguza utegemezi usio wa lazima kwa Serikali, pamoja na OTR yenyewe kuongeza ubora, kasi na ufanisi wa usimamizi wake.


"Hii ni ahadi kubwa, na utekelezaji wake unategemea mchango wa kila mmoja wetu," alisisitiza.

Aliwataka watumishi kuongeza ubunifu katika utekelezaji wa majukumu yao, kufanya kazi kwa kasi, ubora na ufanisi, kutumia teknolojia na takwimu kufanya maamuzi bora, kuimarisha utamaduni wa uwajibikaji na ushirikiano, kuendelea kujifunza na kujenga uwezo, pamoja na kusimamia kwa uadilifu matumizi ya rasilimali za umma.


"Kila mtumishi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina anapaswa kuona uhusiano wa moja kwa moja kati ya kazi anayofanya na matokeo yanayotarajiwa na Taifa," alisema.


Akizungumza Juni 30, 2026, wakati wa kupokea gawio na michango ya Sh1.327 trilioni kutoka OTR, Rais Dkt. Samia aliitaka taasisi hiyo kuhakikisha mashirika na taasisi za umma zinaongeza tija, ufanisi na ushindani, huku zikipunguza utegemezi wa ruzuku za Serikali na kuimarisha uwezo wa kujitegemea kifedha.


"Mafanikio haya yasitufanye turidhike. Uwekezaji wa umma ni mkubwa na matarajio ya wananchi ni makubwa zaidi," alisema Rais Samia.


Alionya kuwa taasisi zinazofanya vizuri zisifiche udhaifu wa zile zinazosuasua.


"Kila taasisi iliyokabidhiwa mali za umma inapaswa kujieleza kwa lugha ya matokeo: imezalisha nini, imeongeza thamani kiasi gani, imechangia mapato kiasi gani, na imepunguza kwa kiwango gani utegemezi wake kwa Serikali," alisema.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mipango, Utafiti na Maendeleo wa OTR, Bw. Emanuel Luvanda, alisema utekelezaji wa Mpango Mkakati wa OTR wa mwaka 2026/27–2030/31 utaweka mkazo katika kuimarisha utawala bora, uongozi na usimamizi wa rasilimali watu, usimamizi wa utendaji, uhamasishaji wa rasilimali, kuboresha uwekezaji, ushirikishwaji wa wadau na kuijengea taasisi uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Aliyasema hayo wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2025/26 pamoja na vipaumbele vya Mpango Mkakati wa OTR mbele ya Baraza la Wafanyakazi.


Naye Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Bw. Chacha Marigiri, alisema OTR itaendelea kuwawezesha watumishi kuongeza elimu na ujuzi kupitia mafunzo na kujiendeleza kimasomo ili kuboresha utendaji na kuongeza tija.


"Tutaendelea kutengeneza mazingira rafiki kwa watumishi wetu," alisema, huku akisisitiza kuwa hakutakuwa na nafasi kwa watumishi wavivu na wazembe.