ARUSHA, TANZANIA – Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, amesema kuwa uhuru wa vyombo vya habari nchini hauwezi kudumu wala kuwa wa kweli ikiwa wanahabari wenyewe hawana uhakika wa kipato na ustawi wa kiuchumi.
Akizungumza katika Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani jijini Arusha, Makonda ameeleza kuwa hali duni ya kiuchumi inawaweka wanahabari katika mazingira magumu yanayowafanya washawishiwe kwa urahisi na maslahi ya wanasiasa au wafanyabiashara.
Amesema hali hiyo ni hatari kwa uadilifu wa taaluma kwani inafungua milango kwa watu wenye maslahi binafsi kufadhili wanahabari ili kulinda taswira zao badala ya kuripoti ukweli.
Makonda amesisitiza kuwa mwelekeo wa sasa wa vyombo vya habari lazima ubadilike. Amewataka wanahabari kuacha kujikita zaidi kwenye siasa na "kubrand" watu, na badala yake waelekeze nguvu zao katika kuibua na kutangaza fursa za kiuchumi zilizopo nchini, hususan katika sekta za utalii, kilimo na biashara.
"Tanzania ina utajiri mkubwa wa vivutio vya utalii na bidhaa zenye ushindani kama kakao, parachichi na tangawizi. Ikiwa vyombo vya habari vitatoa kipaumbele kwa sekta hizi, vitasaidia kuvutia uwekezaji, kutafuta masoko ya kimataifa, na hatimaye kujijengea msingi imara wa mapato," alisema Makonda.
Aidha, amebainisha kuwa vyombo vya habari ni nguzo muhimu katika kuifikisha Tanzania kwenye uchumi wa viwanda. Amesema kuna umuhimu wa wanahabari kubobea katika uchambuzi wa sekta za uzalishaji ili kusaidia Taifa kunufaika na rasilimali zake kwa kuongeza thamani ya bidhaa (value addition), badala ya kuishia kuuza malighafi nje ya nchi.
Makonda amehitimisha kwa kukemea tabia ya baadhi ya wanahabari kutumika kama vyombo vya kulinda maslahi ya watu fulani, akisisitiza kuwa mwelekeo huo unadhoofisha uaminifu wa umma kwa tasnia ya habari na kurudisha nyuma maendeleo ya Taifa.


















































