Na Mwandishi Wetu, Dar Es Salaam
Kuendelea kuthamini na kununua bidhaa zinazozalishwa hapa nchini kunatajwa ni chachu katika kukuza uchumi wetu kwa mtu mmoja mmoja hadi taifa kwa ujumla wake.
Mathalani bidhaa hizi zinazozalishwa hapa nchini licha ya kuwa zinaenda kutoa fursa za soko la ajira lakini pia huchangia pato kwa wanaouza malighafi hizo moja kwa moja
Kiwanda cha kuzalisha bidhaa za ngozi cha Woisso Original Products (WOP)kilichopo Salasala jijini hapa ni miongoni kwa viwanda vinavyozalisha bidhaa za ngozi hapa nchini na kuchangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa sekta hiyo ya ngozi.
Mkurugenzi wa kiwanda hicho Kenneth Woisso anasema kuwa bidhaa za ngozi zinazozalishwa hapa nchini kwa kiasi kikubwa zinachangia ukuaji wa pato la taifa uzalishaji wa ajira sanjari na kuzalisha wataalam wa utengenezaji wa bidhaa hizo
'Sekta hii ina faida na kama ilivyo hata vijana wanapata utaalamu hapa namna yakutengeneza bidhaa hizi hivyo kuwawezesha kujiajiri pia lakini katika masoko pia tunaendelea kujitangaza vyema'anasema
Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo ni kuwa ipo haja kwa sasa kwa watu kuwa na uelewa wakutosha kwa kupenda bidhaa zinazozalishwa hapa nchini kwani faida yake ni kubwa na huuzwa kwa bei inayoendana na hali halisi ya kipato cha mtanzania
Anasema wapo baadhi ya watu ambao hupenda kukimbilia bidhaa za ngozi kutoka nje ya nchi bila kujua athari zake kiuchumi na kuwa mataifa mengine hutumia mwanya huo kuzalisha bidhaa zenye mfanano wa ngozi hivyo kudidimiza soko la ndani.
Woisso anasema ikiwa jamii ya kitanzania itaendelea kuwa na mwamko wa kupenda bidhaa zinazozalishwa hapa nchini kama ilivyo kwa sasa ni kuwa kwa kipindi kifupi sekta hiyo itaenda kupiga hatua kubwa zaidi ya sasa
'Tunazalisha bidhaa mbali mbali zitokanazo na ngozi kama mikoba,mikanda,viti,viatu pochi na vingine vingi hii ni kuhakikisha katika uzalishaji wetu kila aina ya bidhaa unaoitaka ya ngozi utaipata hapa WOP'anasema
Michael Mshiu anasema sekta ya ngozi inaenda kufanya vizuri kama jitihada za maksudi zitafanywa ikiwa ni pamoja na kuthamini wazalishaji wa ndani badala ya kukimbilia zitokazo nje
'Hali hii ni lazima tuongeze jitihada za maksudi katika kuhakikisha sekta hii inaenda kukua ikiwa ni pamoja na kuendelea kuthamini bidhaa za wazalishaji wazawa'anasema






















































