Happy Lazaro,Arusha .
KAMPUNI ya EFTA Tanzania imewazawadia wakulima waliokopa zana za kilimo na kurejesha mikopo yao kwa uaminifu, kwa kuwarejeshea nusu ya riba waliyoilipa wakati wa marejesho ya mikopo hiyo.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa EFTA Tanzania, Nicomed Bohay wakati akizungumza katika hafla ya kukabithi hundi za rejesho la asilimia 50 ya riba kwa wateja waliorejesha mikopo yao kwa nidhamu hafla iliyofanyika katika maonesho ya nanenane Njiro.
Bohay amesema Taasisi hiyo imeamua kurejesha takribani shilingi milioni 100 kwa wateja wake nchini kama motisha ya ulipaji mzuri wa mikopo.
"jumla ya wateja 37 nchini tayari wamenufaika na mpango huo mwaka huu, huku kila mmoja akipokea kiasi tofauti cha fedha kulingana na kiwango cha riba alicholipa."amesema Bohay .
Amesema kuwa, mpango huo unawahusu wakulima waliokopa matrekta, matrela na zana nyingine za kilimo na kutekeleza masharti ya mikopo bila kuchelewa.
Bohay amesema EFTA, ambayo hutoa mikopo ya zana mbalimbali bila kuhitaji dhamana na inaofisi nane nchini, inashiriki Maonesho ya Nanenane katika kanda tano za Arusha, Dodoma, Morogoro, Mbeya na Mwanza.
Amesema kuwa,mwaka huu taasisi hiyo imeamua kutumia maonesho hayo kuwatambua wateja wake bora na kuonyesha kuwa uaminifu katika ulipaji wa mikopo una manufaa ya moja kwa moja.
Amefafanua kuwa mafanikio ya wateja katika ulipaji yameifanya EFTA kupunguza kwa kiwango kikubwa mikopo chechefu (NPL), ambayo kwa sasa ipo asilimia moja pekee.
Bohay ameongeza kuwa,kiwango hicho ni cha kuvutia katika sekta ya fedha na kimeiwezesha taasisi hiyo kuelekeza sehemu ya fedha ambazo zingetengwa kwa ajili ya mikopo chechefu kurudi kwa wateja wake kama zawadi.
Aidha, amewahimiza wakopaji wote nchini kujenga utamaduni wa kulipa mikopo kwa wakati, akisema rekodi nzuri ya mkopaji huwekwa kupitia mfumo wa Credit Reference Bureau wa Benki Kuu ya Tanzania na humrahisishia kupata mikopo kutoka taasisi mbalimbali za fedha siku zijazo.
Amesema hatua hiyo inalenga kujenga uhusiano wa kudumu kati ya taasisi za fedha na wakulima, pamoja na kuhamasisha matumizi ya mikopo yenye nidhamu kwa maendeleo ya sekta ya kilimo.
Wakizungumza mara baada ya kukabithiwa mfano wa hundi hizo wakulima hao walishukuru kwa namna taasisi hiyo inavyowajali na kuwapa motisha wa kuendelea kukopa zaidi.
"Kitendo kilichofanywa na Taasisi hii ni mfano wa kuigwa na taasisi zingine kwani kinatupa moyo wa kuendelea kukopa zaidi zana za kilimo ambapo taasisi hii imekuwa mkombozi mkubwa sana kwa wakulima."amesema .
Kwa upande wao wateja walionufaika na mkopo huo , Sebastian Gwalku kutoka Mkoa wa Manyara amesema kuwa ,amekuwa mteja wa EFTA kwa kupata mkopo uliomwezesha kukuza shughuli za biashara ambapo kupitia mkopo huo ameweza kuendeleza biashara na kuongeza kipato.
"Leo ninafurahi sana kuwa miongoni mwa wanufaika wanaokabidhiwa hundi kama ishara ya kutambua uaminifu wetu katika kurejesha mikopo kwa wakati na nawashukuru sana EFTA kwa fursa hii na kwa kuendelea kuwawezesha wafanyabiashara na wajasiriamali kufikia malengo yao."amesema .
"Ninawahamasisha wafanyabiashara wengine kutumia fursa zinazotolewa na EFTA na kuhakikisha wanarejesha mikopo yao kwa wakati ili nao waweze kunufaika na fursa kama hii."amesema .

















































