TANAPA Watambua Mchango wa Samia Kwenye Ushindi wa Tuzo ya ESQR 2025

 


Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limetambua mchango mkubwa wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika mafanikio ya ushindi wa tuzo ya European Award for Quality Choice Achievement 2025 kutoka taasisi ya European Society for Quality Research (ESQR) nchini Sweden.



Akizungumza katika hafla ya mapokezi ya tuzo hiyo iliyofanyika Juni 2, 2025 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Kamishna wa Uhifadhi CPA (T) Musa Nassoro Kuji alisema:

"Shirika letu linaitoa tuzo hii kwa heshima ya mchango wa Rais Samia katika kuitangaza Tanzania kupitia filamu za 'The Royal Tour' na 'Amazing Tanzania'. Hili ni jambo kubwa ambalo limelifanya taifa letu litambuliwe kwa upekee kimataifa."



Tuzo ya ESQR 2025 ni ya sita mfululizo kushindwa na TANAPA tangu mwaka 2020, ikiwa ni ishara ya uendelevu wa utoaji huduma bora katika sekta ya utalii na uhifadhi nchini.

Kamishna Kuji aliongeza:
"Ushindi wa tuzo hii kwa mara ya sita mfululizo unatuongezea hamasa na ari ili tuendelee kutoa huduma bora kwa watalii na kuliheshimisha taifa kimataifa."
"Huduma bora ni utamaduni wetu TANAPA. Tunataka wageni waendelee kufurahia vivutio vyetu na kusaidia kukuza pato la taifa kupitia utalii."

Kauli mbiu ya "TANAPA Nyumbani kwa Tuzo" ilitawala hafla hiyo, ikiashiria fahari na mafanikio ya pamoja kwa shirika na taifa kwa ujumla.



Naibu Kamishna wa Uhifadhi, Steria Ndaga, alisema:
"Tuzo hii ni matokeo ya juhudi za pamoja kati ya Wizara ya Maliasili na Utalii, TANAPA na wananchi. Ni uthibitisho kuwa kazi yetu inatambuliwa kimataifa."

Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi Mwandamizi Godwell Meng’ataki aliyeshiriki hafla ya utoaji tuzo hiyo nchini Sweden alisema:
"Tuzo hii ni ushindi mkubwa kati ya nchi 42 na ni chachu ya kuendelea kuboresha zaidi huduma zetu."

Kupokelewa kwa tuzo hii kumeweka Tanzania katika ramani ya dunia kama nchi inayoongoza kwa huduma bora za utalii na uhifadhi, huku mchango wa uongozi wa juu wa taifa ukiendelea kuonekana kama sehemu muhimu ya mafanikio hayo.

0 Comments:

Post a Comment