MIUNDOMBINU MLIMA KILIMANJARO INABORESHWA

 


 

HIFADHI ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro, (KINAPA)  imesema iko mbioni kuanza kutumia 'cable cars' kupandisha watalii kwenye mlima huo mrefu kuliko yote barani Afrika.

 

 

Kamishna Mwandamizi wa Uhifadhi TANAPA, Kanda ya Kaskazini, Herman Batiho ameyasema hayo Oktoba 10, mwaka huu wakati akiongea kwenye hafla ya kuwapokea wapanda mlima 150 waliopelekea bendera ya Taifa kwenye kilele cha mlima huo kwa ajili ya maadhimisho ya miaka 60 ya uhuru wa Tanzania Bara wakiongozwa na Kanali, Martin Msumari.

 

 

 Amesema KINAPA imeendelea kuboresha miundo mbinu yake ikiwemo njia za kupanda na kushuka, vifaa vya uokoaji badala ya kutumia baiskeli ya kitanda ya mguu mmoja kwa uokoaji sasa wanatumia helkopta kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

 

"KINAPA imeweza kuongeza mazao ya utalii kutoka yale ya kutembea kwa miguu kupanda mlima mpaka sasa wengine wanapanda mlima kwa baiskeli na tuko mbioni kuanza kutumia 'cable car' jambo ambalo litawezesha watalii hata wale ambao ni walemavu waweze kufika na kuona hifadhi yetu na mandhari mbalimbali zilizopo kule," anasema Batiho na kuongeza.

 

..Shughuli kama parachuti zinafanyika kwenye kile kilele cha mawenzi watalii wanapanda lakini  na kuna watalii wanafanya safari za siku moja kuona maporomoko ya maji ya Marangu na wengine wanaenda mpaka kituo cha Mandara...

 

...Kuna utalii wa kimichezo, tumeshuhudia kuna watalii nakuja kufanya michezo kwenye Uhuru  Crater, kuruka vikwazo pamoja na kukimbia hivi ni moja ya vitu vinavyovutia watalii wengi kuja na kuongeza mapato,".

 

Batiho amesema kuwa wamepanga mpaka kufikia mwaka 2026 watalii wawe wameongezeka kufikia watalii milioni 5 kwa mwaka kutoka watalii milioni 1.5 wanaotembelea hifadhi hiyo kwa mwaka ambapo itaongeza mapato kufikia dola za Marekani milioni 6.

 

Amesema kuwa wameweka mikakati ya kufikia malengo hayo ikiwemo hilo la kuanza kupandisha watalii mlimani kwa kutumia 'cable car', kuboresha miundo mbinu kwa kujenga mabanda katika njia ya Kidia na Marangu.

 

"Wapandaji nadhani mmeshuhudia pale Horombo kuna ujenzi wa mabanda unaendelea na bado kuna 'plan B' ya kuongeza mabanda zaidi ili kutosheleza mahitaji pale pamoja na kituo cha Kibo," amesema Batiho.

 

Hata hivyo amesema kuwa hayo yatawezekana endapo kwa pamoja wadau wote wakiwemo wananchi watashirikiana kulinda mazingira ya mlima huo kwani KINAPA haiwezi kuulinda mlima huo kwa mtutu wa bunduki pekee.

 

Pia Batiho amewaomba wale wanaoongoza na kuwahudumia watalii kufanya kazi hiyo vizuri na kwa uaminifu kwa kuacha kuwaibia wageni na kuwaomba fedha (Tip) kwani vitendo hivyo huwakera watalii.

 

 

"Sisi kama KINAPA tumejipanga kupanda miti kwa kushirikiana na wananchi wanaotuzunguka kwa sasa tumeanza na miche laki moja na zoezi hili limeashaanza na nia ni kupunguza hewa ya ukaa ambayo kwa kiwango kikubwa ndiyo inayochangia kuharibu ozoni,amesema -Batiho na kuongeza

 

....Nikuombe Mkuu wa mkoa muweze kuhamasisha wananchi ili hii miti tunayopanda wahakikishe inakua ili kukabiliana na hewa ya ukaa lakini wao wapate kuni na matunda,".

 

Kwa upande wake,  Mkurugenzi wa Kampuni ya uwakala wa utalii ya ZARA, Zainab Ansel alisema kuwa wametumia zaidi ya miezi sita kuandaa safari hiyo hivyo anamshukuru Mungu kwa safari hiyo kukamilika kwa mafanikio.

 

" Mwaka huu wamepanda watu 153 mwakani tutaomba tupewe muda wa kutosha kufanya matangazo ili watu wengi zaidi wajitokeze kupanda kusherekea miaka 61 ya uhuru,"alisema Zainab.

 

Hata hivyo aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea vivutio vingine vilivyopo nchini kwani Tanzania  imebarikiwa vivutio vingi sana vya utalii vulivyopo kwenye maeneo mbalimbalimbali ya nchi.

 

Akiwapokea wapanda mlima hao, mgeni rasmi ,  mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Steven Kagaiga amesema mlima  Kilimanjaro una umuhimu zaidi ya inavyofikiriwa na wengi kuwa ni kwa ajili ya utalii kwani ndiyo unaopeleka maji kwenye bwawa la nyumba ya Mungu linalotumika kwa shughuli za uvuvi na kuzalisha umeme hivyo kila mmoja ana wajibu wa kulinda na kutunza mazingira ya mlima huo.

 

 

Amesema kuwa maji yanayotoka kwenye mlima Kilimanjro ni muhimu kwa maisha ya wananchi kwani ndiyo ynayotumika kwa matumizi ya nyumbani, kilimo cha umwagiliaji na kwenye bonde la Pangani.

 

"Watu wengi wanafikiri mlima huu uko kwa ajili ya utalii tu ila huyu mama (Kamishina Msaidizi wa Uhifadhi KINAPA,Angela Nyaki) nikifika Kilimanjaro alikuja ofisini alinieleza kuwa kumbe maji ya kilimo yanatokana na mlima juu. Maji ya nyumba ya Mungu, bonde la  Pangani  yote yanatokana na mlima huu, hata  umeme wa Nyumba ya Mungu chanzo ni hapa," alisema Kigaogai na kuongeza.

 

....Kuanzia pale niliamua kuwa balozi wa huu mlima, na kuanzia pale nilikuwa mkali kuhakikisha mazingira yanahifadhiwa, huu mlima ni kitega uchumi na ni maisha ya wananchi wa Tanzania ...

 

Wananchi waunge mkono jitihada za kuuhifadhi mlima huu itakuwa vibaya tukiharibu mazingira kwa kukata misitu na kufanya shuguli za kilimo ndani ya hifadhi ya mlima huu ,".

 

Kigaigai amesema kuwa  takwimu zinaonyesha utalii wa ndani kwa ajili ya kupanda mlima Kilimanjaro unasuasua hivyo akatoa rai kwa wananchi wa Jumiya ya Afrika Mashariki, (EAC) wajenge utamaduni wa kutembelea vivutio vilivyo kwenye ukanda huo ili kukuza utalii wa ndani.

 

Kiongozi wa msafara huo kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania, (JWTZ), Kanali, Martin Msumari amesema kuwa wapanda mlima 79 wamefanikiwa kufika kwenye kilele cha uhuru.

 

 

"Desemba 9, tuliandika historia kwa kuwa uhuru 'peak' (kilele) palisongamana watu kutoka ndani na nje ya nchi, watu 75 kufika hapo si jambo dogo," alisema Kanali Msumari.

 

Aidha aliuomba uongozi wa TANAPA kumtumia Mtangazaji wa Shirika la habari la Uingereza, (BBC), Salim Kikeke kama balozi wa hiari wa kuutangaza mlima huo kwani ana watu wengi wanaomfuatilia ndani na nje ya nchi aweze kuwashawishi kuja kufanya utalii kwenye mlima huo.

 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa bodi ya TANAPA, Jenerali Mstaafu, George Waitara, alitoa zawadi ya shilingi milioni tano kwa waongoza utalii na wabeba mizigo wa kampuni ya uwakala wa utalii ya ZARA kazi nzuri waliyofanya kuhudumia msafara huo kwa siku siku suta walizokuwa mlimani.

 

"Namshukuru sana mama Zara(Zainab Ansel) kwa kuweza kufanikisha zoezi hili. Kabla ya kustaafu kama mkuu wa majeshi tuliweka utaratibu wa kupanda kila mwaka nikishirikisha watu mbalimbali.  Nashukuru Jeshi wameendeleza na nilipoteuliwa kuwa Mwenyekiti wa bodi ya TANAPA nikahakikidha wanaliweka kwenye kalenda zao,"alisema Waitara na kuongeza.

 

 

.....Nilienda mpaka kituo cha Mandara ili nione watu 150 wanapandaje mlima nikajiridhisha huduma ziko vizuri, sehemu za kulala ziko za kutosha chakula kiko vizuri...

 

...  'Guide' (muongoza utalii) Faustini Chombo ni mzuri na timu yake alinihakikishia wengi watafika na wamefika na wagumu (wabeba mizigo) mmefanya kazi kubwa kwa kuwatambua na kuwapa soda . Nawapa shilingi milioni tano.Mmefanya kazi nzuri sana mara zote niliwaona mnatabasamu mnajitolea kuumia ili mpanda mlima asiumie,".

 

Alisema kuwa suala la Mtangazaji, Kikeke kutangazwa kuwa balozi wa utalii wa mlima huo ataliwasilisha kwa Waziri wa Maliasili  na Utalii, Damas Ngombaro huku akidaI anaamini atalikubali kwani anaamini mtangazaji huyo atakuwa anakuja kila mwaka na marafiki zake kwa ajili ya kupanda mlima huo .

 

Hifadhi ya KINAPA ilianza mwaka 1973 na kwa msaada wa shirika la Misaada la Norway, (NORAD) waliweza kujenga mabanda kwenye kutuo cha Mandara na Horombo.

 

KINAPA kwa kushirikiana na wadau mbalimbali waliweza kufungua njia nyingi za kuweza kufika kileleni kwani walianza na njia moja ambapo kwa sasa zipo njia saba tano za kupanda mlimani na mbili za kushuka.

 

Hifadhi hiyo imekuwa na manufaa kwa wananchi wanaoishi kuzunguka hifadhi hiyo na Taifa kwa ujumla huku ikifanikiwa kupata tuzo mbalimbali ambapo mwaka 2013, ilipata tuzo tano kama sehemu nzuri zaidi ya kutembelewa na watalii.

 

 

 

0 Comments:

Post a Comment