Diddy Akutwa na Hati‍a ya Usafirishaji kwa Ajili ya Ukahaba, Asafishwa Kwenye Mashtaka ya Ulanguzi wa Ngono na Njama za Ulaghai

 


Baada ya majadiliano ya siku tatu yaliyochukua jumla ya saa 13, jopo la majaji limefikia uamuzi wa kesi dhidi ya msanii maarufu Sean "Diddy" Combs. 

Kesi hiyo, iliyofanyika jijini New York tangu mwezi Mei, ilihusu tuhuma tano nzito zikiwemo za ulanguzi wa ngono na njama za uhalifu.

Katika hukumu ya mwisho, Combs alipatikana na hatia ya makosa mawili kati ya matano aliyoshtakiwa nayo:

  • Njama za ulaghai: Hana hatia

  • Ulanguzi wa ngono wa Cassie Ventura: Hana hatia

  • Usafirishaji wa ukahaba wa Ventura na wengine: Ana hatia

  • Ulanguzi wa ngono wa mwanamke aitwaye “Jane”: Hana hatia

  • Usafirishaji kwa ajili ya ukahaba wa “Jane” na wengine: Ana hatia

Hukumu hii inamaanisha kwamba Combs atakabiliwa na kifungo kikubwa gerezani, huku tarehe ya kutoa adhabu rasmi ikitarajiwa mwezi Oktoba. 


Jaji Arun Subramanian amekataa maombi ya dhamana ya wakili wake, Marc Agnifilo, aliyependekeza kiasi cha dola milioni moja, sawa na takribani shilingi bilioni 2.6 za Kitanzania.

Jaji Subramanian alisema kuwa: “Haiwezekani kwa mshtakiwa kuthibitisha kuwa hatarishi kwa jamii. Ametenda vitendo vya ukatili wa nyumbani na ana mwelekeo wa kutumia nguvu.”



Wakili wa Cassie Ventura, Douglas Wigdor, alitoa tamko mara baada ya hukumu:
“Kwa kusimama kidete na kueleza aliyopitia, Cassie ameacha alama isiyofutika katika tasnia ya burudani na mapambano ya haki.”

Aliongeza kuwa: “Yuko katika hali nzuri. Anaendelea na maisha pamoja na familia yake na mumewe. Tunatumaini watu wataendelea kumtambua Cassie kwa ujasiri wake, kwa sababu amefanya jambo la tofauti.”

Wigdor aliendelea kuonyesha matumaini kwamba hukumu hii ni mwanzo wa kuwajibika kwa wale walio na mamlaka:
“Tunajua kiwango cha ‘beyond reasonable doubt’ ni kikubwa sana, lakini tunaridhika kuwa amepatikana na hatia ya makosa ya shirikisho. Hatimaye anakabiliwa na kifungo kikubwa, jambo ambalo hajawahi kukumbana nalo katika maisha yake.”

Wakili huyo pia aliandika barua kwa Jaji Subramanian akisisitiza kuwa Combs asiachiliwe kwa dhamana:
“Ventura anaamini kuwa Combs bado ni tishio kwa waathirika waliotoa ushahidi, ikiwemo yeye binafsi, pamoja na jamii kwa ujumla.”

Katika ushahidi wake mahakamani, Ventura alieleza jinsi Combs alivyomtawala binafsi na kitaaluma, pamoja na kumlazimisha kupanga sherehe za ngono zilizoambatana na matumizi ya dawa za kulevya – alizozitaja kama "freak offs". Alidai kuwa alikuwa akilazimika kushiriki na kuwahusisha wanaume wengine waliokuwa wakilipwa, kwa amri ya Combs.

Combs alikana mashtaka yote akisema: "Mahusiano yangu yalikuwa ya ridhaa, na japokuwa yalihusisha vipindi vya vurugu, sikuhusika katika ulanguzi."

Kesi hii imeibua mjadala mkubwa kuhusu matumizi mabaya ya mamlaka, unyanyasaji dhidi ya wanawake, na nafasi ya jamii katika kuwawajibisha watu wenye ushawishi mkubwa.

Mkutano wa maandalizi ya kutoa hukumu umepangwa kufanyika kwa njia ya mtandao mwezi Julai, huku macho yote yakielekezwa kwa adhabu ya mwisho ambayo Combs atakumbana nayo.

0 Comments:

Post a Comment