MAKAMU WA RAIS ARIDHISHWA UJENZI MAKAO MAKUU YA NCAA


 

MAKAMU wa Rais, Dkt Philip Mpango ameipongeza  Mamlaka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro,(NCAA) kwa kuamua kujenga makao makuu yake nje ya hifadhi hivyo kuonyesha kwa vitendo umuhimu wa  kupunguza shughuli za kibinadamu ndani ya hifadhi kwa uhifadhi endelevu.

Ameyasema hayo leo, Mei 16,2023 wakati akiweka jiwe la msingi kwenye jengo la makao makuu ya NCAA,  linalojengwa kwenye mji wa Karatu.





“Niseme kwa kifupi nimeridhishwa na kazi inayoendelea kampuni ya ukandarasi inayojenga jengo hili, (kampuni ya China Jiangxi International Economic and Technical Cooperation Limited) wasimamizi,  Wizara ya Maliasili na Utalii na uongozi mzima wa NCAA,” amesema Profesa, Mpango na kuongeza

 

…Nimeangalia nimeona ujenzi ni bora kabisa na imejengwa mpaka kufika hapa... Kazi nzuri ingawa najua kazi bado ni kubwa, kukamilisha jengo la utawala, nyumba za kamishina wa uhifadhi na za wafanyakazi wengine,”.

“ Simamieni kazi hizo zikamilike kwa wakati na ubora unaotakiwa tunataka kupata thamani ya fedha katika ujenzi huu.Tunataka kama inawezekana zitumike mali ghafi kutoka hapahapa nchini mpaka ‘furniture’ (samani)  itapendeza sana tukitumia ‘furniture’  zetu za hapahapa nchini,”.



AWAPA NENO WATUMISHI

Dkt Mpango aliwaeleza watumishi wa NCCA kuwa jengo hilo la makao makuu likapokamilika na kuanza kulitumia  wahakikishe wanalitunza kwa weledi wa hali ya juu  kwa faida ya kizazi cha sasa cha Tanzania, Ulimwengu na vizazi vijavyo.

 

“Mtakapopata jengo la utawala la kisasa na makazi bora natumani itakuwa ni hamasa kwenu watumishi kufanya kazi kwa ari na ufanisi zaidi hivyo mna dhamana kubwa sana kwa Taifa rasilimali hizi ambazo Mungu alitupa ni muhimu sana kwa Taifa,” amesisitiza Dkt Mpango na kuongeza.

….Nachotaka mimi ni mapinduzi ya kiutendaji,  muongeze ufanisi zaidi na muweze kujiendesha kibiashara nimesikia suala la mapato lakini jitahidini muweze kufanya zaidi mzidi malengo mliyojiwekea,”.

 

‘Tunachangamoto ya jirani zetu wengine ni majangili wengine wanaleta ng’ombe tena wanaleta kutoka nje ya mipaka yetu ninachowaomba watumishi wa mamlaka lakini pia wananchi msishirikiane na majangili na niwambe sana muwe macho na jitihada zozote za kuharibu uhifadhi.”.

 

MAHUSIANO NA JAMII



Makamu wa Rais, ameikumbusha NCAA kuisaidia jamii inayowazunguka kwenye eneo hilo jipya la makao yao makuu kwa kuwakwekea miundo mbinu itakayowasaidia kuendesha shughuli zao za ufugaji kwa ufanisi zaidi.

 

“Waliotuzunguka hapa kwa kiasi kikubwa ni wafugaji bila shaka pia wako na wakulima. Serikali inafanya juhudi kubwa kuboresha miundombinu ya shule zetu, afya na maji,” amesema Dkt Mpango na kuongeza .

 

….Lakini ningependa nitume ombi mahsusi kwa mamlaka ya Ngorongoro kama sehemu ya kuboresha mahusiano na jamii muongeze nguvu katika ujenzi wa malambo ya maji kwa ajili ya mifugo,”.


 

MCHENGERWA  AELEZEA MATARAJIO





Kwa upande wake Waziri wa Maliasili na Utalii, Mohamed Mchengerwa amesema kuwa kukamilika na kuanza kutumika kwa majengo hayo inategemewa kupunguza gharama za uendeshaji wa NCAA, kuongeza ufanisi na utoaji wa huduma kwa wateja wao na kupunguza shughuli za kibinadamu ndani ya hifadhi.

Amesema kuwa  zoezi hilo lilienda sambamba na kuhamisha kwa hiari wananchi waliokuwa ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kwenda Msomera mkoani Tanga.

“Hii ni awamu ya kwanza ya Mradi huu, tunawapongeza sana wajenzi wa mradi huu kampuni ya China Jiangxi International Economic and Technical Cooperation Limited kwa kwenda kwa spidi nzuri lakini unaokidhi viwango ambavyo wizara tunautegemea,” amesema Waziri Mchengerwa na kuongeza.

 

…Kwa sasa hivi ujenzi uko zaidi ya asilimia 35, (wajenzi) wameahidi ifikapo mwezi Oktoba utakuwa umekamilika na ofisi zitakuwa zimefunguliwa. Tunategemea mkandarasi atakamilisha ujenzi wake kama ambavyo ametuahidi,”.

 

UJENZI KUGHARIMU ZAIDI YA BILIONI 10.4 



Kwa upande wake, Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, NCAA,  Elibariki Bajuta amesema kuwa ujenzi huo  unatekelezwa na kampuni ya China Jiangxi International Economic and Technical Cooperation Limited kwa gharama ya shilingi bilioni 10.4.

 

Amesema kuwa mkataba wa ujenzi huo ulisainiwa mwezi Agosti mwaka jana na ujenzi kuanza rasmi oktoba mwaka huohuo ambapo unatarajiwa kukamilika Oktoba mwaka huu ukijumuisha jengo la utawala na nyumba tatu za makazi ya Kamishina wa uhifadhi na wasaidizi wake wawili.

 

Bajuta amesema kuwa kutakuwa na awamu ya pili ya mradi huo utakaogharimu kiasi cha shilingi bilioni 2.5 ambao utajumuisha ujenzi wa zahanati, karakana mbalimbali za ujenzi, ufundi seremala na umeme na cafeteria kuwawezesha wafanyakazi kupata huduma ya chakula.

 

Pia Ujenzi wa viwanja vya michezo na sehemu ya ukaguzi na magwaride na shughuli za ukakamavu na sehemu itakayotumika kwa ajili ya malazi na mapumziko kwa viongozi.

 

 “Chimbuko la ujenzi huu umetokana na tishio la kutoweka kwa bayoanuwai urithi wa utamaduni na rasilimali za miamba kunakochangiwa na kuongezeka kwa shughuli za kibinadamu ongezeko la watu na mifugo pamoja na mimea vamizi ndani ya hifadhi,” amesema Bajuta na kuongeza.

…Sisi (NCAA)  tuliona ni vema kuondoka ndani ya hifadhi tuje huku na tuliona ni njia moja ya kupunguza gharama kwa sababu tulikuwa tunaishi Karatu halafu tunaingia ndani ya hifadhi na kurudi,”.

 

“Tuliona hiyo itasaidia shughuli za kibinadamu zifanyike nje ya hifadhi na shughuli za uhifadhi na utalii zifanyike ndani ya hifadhi,”.

Akizungumzia utendaji wa NCAA, Bajuta amesema kuwa taasisi hiyo imefanikiwa kukusanya kiasi kikubwa cha fedha kuliko wakati wowote tokea kuanzishwa kwake.

 

“Katika kipindi cha kuanzia Julai,2022 mpaka Aprili, 2023 tumeshapokea jumla ya wageni 612, 252 ambapo wageni 231,181 ni watalii wa ndani na watalii wa nje ni 381,071. Idadi hii ya watalii imeongezeka kwa asilimia 89 ukilinganisha na mwaka uliopita,” amesema Bajuta na kuongeza.

 

…Ongezeko hilo limechangia kuongezeka kwa mapato ambapo mpaka Mei 9, 2023 tumeshakusanya shilingi bilioni 163.74 hii ni kiwango kikubwa sana cha fedha ambacho hakijawahi kukusanywa tangu NCAA  kuanzishwa,”.

 

 



Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Mawakala wa Utalii nchini,(TATO), Wilbard Chambulo, amesema kuwa hatua ya NCAA kujenga makao makuu yake nje ya hifadhi ni uamuzi sahihi kwani inapunguza msongamano wa magari yaliyokuwa yakiingia hifadhini kwa shughuli zisizo za utalii.

“ (NCAA) Wanapotoka kule ndani wameacha nafasi ya uasili (nature) iendelee na pia itasaidia kukuza uchumi kwa wananchi wa Karatu kwani watapata huduma mbalimbali kutoka kwenye eneo hili na hata thamani ya vitu vitaongezeka,” amesisitiza Chamburo na kuongeza

 

…Ofisi hizi kuwa nje ya hifadhi imetusaidia hata  sisi (Makampuni ya Uwakala wa Utalii) kwa sababu haitulazimishi kulipia au kupata kibali kama ilivyokuwa ili uweze kuingia ndani ya hifadhi kwa jili ya kupata huduma za kiofisi. Hii itapunguza ule msongamano wa magari ya wafanyakazi na sisi ambao hatukuwa tukienda kwa ajili ya kuingiza watalii bali kufuata ofisi hizi ndani ya hifadhi,”

 

…Tuwaache magari ya watalii ndiyo yapite ndani ya hifadhi kwa ajili ya kutalii,”.

 

 

 


0 Comments:

Post a Comment