SABAYA AUGUA KESI YASHINDWA KUENDELEA

 

Lengai Ole Sabaya akiongea na wakili wake Moses Mahuna alipoletwa mahakamani jana Novemba 2,2021

ALIYEKUWA Mkuu wa wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya ameugua gerezani hivyo kusababisha kesi yake ya uhujumu uchumi kukwama kuendelea.

Wakili wa Sabaya, Moses Mahuna leo (Novemba 3, 2021) ameieleza mahakama ya hakimu Mkazi Arusha mbele ya hakimu Mkazi, Patricia Kisinda anayesikiliza shauri hilo la uhujumu uchumi namba 27/2021.

Ameeleza mahakamani hapo kuwa taarifa za mteja wake kuugua amezipata asubuhi hivyo akaomba mahakama iahirishe shauri hilo mpaka kesho.

"Kama nilivyotangulia kusema mshitakiwa wa kwanza hayupo ni mgonjwa. Tumepata taarifa zake asubuhi hii hivyo tulikuwa tunaomba ahirisho mpaka kesho ili tupate taarifa zake kama amerecover ni hayo tu mheshimiwa," ameomba wakili Mwandamizi Mahuna.

Kwa upande wake wakili wa serikali mwandamizi, Ofmed Mtenga ameieleza mahakama hiyo kuwa hawana pingamizi na ombi hilo la hairisho ila akaomba kesho mshitakiwa aje na uthibitisho wa kuwa alikuwa mgonjwa.

"Hatuna pingamizi shauri liahirishwe mpaka kesho lakini "for the matter of record'(kwa ajili ya kuweka kumbukumbu). Kwa kuwa mpango wa upande wa mashitaka ni kuharakisha hii kesi wanaposema anaumwa," amesema Wakili, Mtenga na kuongeza.

....Maneno ya mdomo peke yake hayatosha tunaomba akija hiyo kesho aje na uthibitisho kweli kwamba anaumwa ili kuondoa doubts ambazo mtu yryote  anaweza kuwa nazo kuwa alichelewesha kesi makusudi,".


Hoja hiyo ilimuinua wakili wa utetezi, Mahuna ambaye aliamua kurejea majadiliano baina ya mawakili wa pande zote kabla ya mahakama kuanza na mara baada ya mahakama kuanza juu ya msimamo wa mteja wake, Sabaya ambaye aliomba kesi iendelee bila uwepo wake.


"Mheshimiwa tulijaribu kuwa kama maafisa wa mahakama kuisaidia mahakama lakini lengo la mshitakiwa ni kesi iendelee hata akiwa hayupo tukawasiliana na mawakili wa serikali wakasema kama ni siku moja tunaweza kuendelea na kesi," amesema Mahuna na kuongeza.

...Ila kama wako serious kuwa shauri lilipangwa kuendelea walete shahidi tumcross (wamuulize maswali ya dodoso) na  ushahidi wa ugonjwa nimepewa cheti chake na askari magereza hiki hapa (akinyanyua juu cheti cha matibabu na kumkabidhi karani) alitibiwa jana jioni na ameandikiwa ED (mapumziko) ya siku mbili...

....Kama upande wa jamhuri wako serious kesi iendelee tuko tayati kuendelea na kesi sasa hivi. Wamlete shahidi wao,".

Baada ya hoja hizo hakimu Mkazi, Kisinda alitoa uamuzi mdogo kuwa mahakama imekubaliana na ombi la mawakili wa utetezi la kuahirisha shauri hili mpaka kesho, Novemba 4, 2021 atamapokuwepo mshitakiwa.

Alieleza kuwa mahakama imeona haitakuwa busara shauri hilo kuendelea bila mshitakiwa kuwepo mahakamani.


Washitakiwa sita waliofika mahakamani walionekana kuchukua muda mrefu kujadiliana na mawakili wao ambapo baada ya hapo walirejeshwa kwenye mahabusu iliyopo mahakamani hapo kusubiri usafiri wa kuwarejesha mahabusu kwenye gereza la Kisongo.

Washitakiwa hao ni  pamoja na Enock Mnkeni, (41) maarufu  Dikdik, Watson Mwahomange, (27) maarufu Mamimungu, John Aweyo, maarufu  Mike One, Silvester  Nyengu, (26) maarufu Kicheche, Jackson Macha, (29) na Nathan Msuya, (31).

Katika mashitaka hayo Sabaya anakabiliwa na mashitaka yote matano ya kuongoza genge la uhalifu, matumizi mabaya ya madaraka, kushawishi na kujipatia fedha kwa njia ya rushwa na kutakatisha fedha.

 

Washitakiwa sita waliobaki wakikabiliwa na mashitaka mawili kila mmoja ya kuongoza genge la uhalifu na utakatishaji fedha kinyume cha sheria.


Hati hiyo ya mashitaka imesomwa Septemba 9, 2021 na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tarsila Gervas mbele ya hakimu mkazi, Dkt. Patricia Kisinda anayesikiliza shauri hilo la uhujumu uchumi namba 27/2021.

 

Akiwasomea mashitaka hayo, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tarsila aliieleza mahakama hiyo kuwa, shitaka la kwanza linawakabilia washitakiwa wote saba  ni la kuongoza genge la uhalifu kinyume cha sheria ya uhujumu uchumi.

 

Akisoma maelezo ya kosa, Wakili huyo ameeleza kuwa, mnamo Januari 22, mwaka huu,  Sabaya akiwa  katika maeneo tofauti ndani ya jiji la wilaya ya Arusha  akiwa mtumishi  wa umma kwa nafasi ya mkuu wa wilaya ya Hai iliyopo mkoani Kilimanjar na anadaiwa kukiuka masharti yake ya ajira.

 

Sabaya anadaiwa kushirikiana na washitakiwa wenzake sita ambao si maafisa wa serikali lakini kwa makusudi kabisa walifanya vitendo vya uhalifu kwa kutumia nafasi ya Lengai ole Sabaya ambaye ni mtumishi wa umma na kujipatia fedha za Kitanzania shilingi milioni 90 kwa manufaa yao.

 

Katika Shitaka la pili linalomkabili Sabaya peke yake ni la kujihusisha na vitendo vya rushwa kinyume na sheria ya kupambana na kuzia rushwa.

 

Imedaiwa mahakamani hapo kuwa  mnamo Januari 22, 2021, Sabaya akiwa kwenye maeneo ya Kwamrombo yaliyo katika kwenye jiji na wilaya ya Arusha alijihusisha na vitendo vya rushwa kwa kumtaka Frances Mroso ampatie shilingi milioni 90 za Kitanzania.

 

Sabaya anadaiwa kushirikiana na washitakiwa wenzake sita kama kushinikiza kupatiwa kiasi hicho cha fedha ili wasitoe taarifa za jinai dhidi ya Mrosso ambapo kwa wakati huo walikuwa wakimtuhumu kwamba alikuwa na makosa ya ukwepaji kodi.

 

Kosa la tatu ni kujihusisha na vitendo vya rushwa, shitaka linalomkabili Sabaya peke yake anayedaiwa kuwa mnamo Januari 22, 2021 alijihusisha na vitendo vya rushwa kwa  alijipatia shilingia milioni 90 kutoka Frances Mrosso akishirikiana na washitakiwa wenzake sita katika kumshinikiza ili wasitoe taarifa ya kosa la jinai ambalo walimtuhumu nalo Mrosso.

 

Kosa la nne ni matumizi mabaya ya madaraka kinyume cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa ambalo linamkabili Sabaya peke yake ambapo anadaiwa mnamo Januari 22, 2021 akiwa kwenye maeneo ya Kwamromboo jijini na wilayani Arusha alitumia vibaya mamlaka yake ya ukuu wa wilaya ya Hai iliyopo mkoani Kilimanjaro.

 

Sabaya anadaiwa kwa makusudi kabisa alimtisha Mrosso kumfungulia mashitaka ya kukwepa kodi kinyume cha sheria za tawala za mikoa kwa madhumuni ya kujipatia  shilingi milioni 90 kwa faida yake na washitakiwa wengine sita.

 

Kosa la tano ni utakatishaji fedha  kinyume na sheria ambalo linawakabili washitakiwa wote saba ambapo wanadaiwa kuwa mnamo Januari 22, 2021 maeneo ya Kwamrombo

, wote kwa pamoja walijipatia fedha kiasi cha shilingi milini 90 wakati wakijua walipokuwa wakipokea fedha hizo ni zao la vitendo vya rushwa.

 Washitakiwa wote walikana mashitaka hayo











 a.


0 Comments:

Post a Comment