BODI ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, (CPB) inasambaza tani 225 za mbegu bora za ngano kwa wakulima wilaya tano kwenye mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara.
Aidha bodi hiyo kwa kushirikiana na kampuni ya kuzalisha na kusambaza mbegu ya Seed Co Tanzania limited, wameahidi kutoa elimu na usaidizi wa kitaalam kwa wakulima kwenye maeneo hayo ili kuwawezesha kupata mavuno mengi na bora.
Meneja wa CPB kanda ya Kaskazini, Hiza Kiluwasha Machi 13, mwaka huu alikabidhi tani 17 za mbegu hizo kwa uongozi wa chama cha ushirika cha wakulima wa ngano Monduli juu, (AMCOS).
Mbegu hizo zilipokelewa na viongozi wa ushirika huo akiwemo, Mwenyekiti, Moloimeti Sane na Katibu, Sifael Lormunyoi ambapo zilihifadhiwa kwenye ghala la kijiji cha Emairete kata ya Monduli juu tayari kusambazwa kwa wakulima.
Mbegu hizo za ngano ya chakula zinaelezwa kuwa na ubora wa hali ya juu kutokana na kuwa na protini ya kutosha hivyo ngano itakayovunwa inafaa zaidi kwa matumizi ya nyumbani na viwandani ambapo hutumika kutengenezea mikate, keki, chapati na vyakula vingine.
"Tuna faraja kubwa sana kuletewa Mbegu ya ngano . Mbegu hii hatujawahi kuiotesha hivyo tutajitahidi kuwa makini sana wakati wote wa kilimo cha ngano hii ya chakula kuanzia ikiwa shamba mpaka kuvuna ili tuweze kujua ubora wake. Tunataka tufanye vizuri ili tuondokane na adha ya kilimo cha shayiri ambacho tumedumu nacho kwa muda merefu lakini kwa sasa soko linayumba," alisema mwenyekiti Sane na kuongeza.
...Tunaishukuru serikali kwa kweli kutusaidia kwenye zao la ngano ya chakula ambalo lina bei hakika kuliko mazao mengine tunayolima . Tunalima yanabaki stoo yanaoza. Kwa hii ya kutupatia soko la uhakika tunaishukuru serikali kwa kutujali wakuima wa ngano,".
Kwa upande wake katibu wa AMCOS, Lormunyoi alisema kuwa wa kitendo cha CPB kuingia nao mkataba wa kununua ngano yote watakayoivuna kimewapa faraja sana kwani wanalima wakiwa na uhakika wa kuuza mazao yao tena kwa bei nzuri.
WAKULIMA KUANZA KUPANDA NGANO HIYO LEO
Meneja wa CPB kanda ya kaskazini, Kiluwasha alisema kuwa ngano hiyo imesambazwa kwenye maeneo ambayo wameishaingia mikataba na wakulima kwa ajili ya kununua ngano yao pindi wakivuna.
Alisema kuwa programu hiyo inatekelezwa kanda ya kaskazini ambapo tayari wameshakabidhi mbegu hizo za ngano kwa wakulima wa Nangwa wilayani Babati mkoani Manyara , Karatu na Monduli Juu mkoani Arusha pamoja na West Kilimanjaro wilayani Siha mkoani Kilimanjaro.
"Tutahakikisha wakulima tulioingia nao mkataba wote wanapata mbengu na jumatatu wote watakuwa wanapanda mbegu hizo shamba," alisema Kiluwasha na kuongeza.
"Hii ngano ni ile ina ubora imekidhi viwango, itaanza kupandwa jumatatu. Tunatekeleza maagizo ya Rais (John Magufuli) kuhakikisha zao la ngano linafufuliwa na tunahamasisha wakulima wengi kulima,".
Alisema kuwa CPB imeingia makubaliano ya kimkataba na wakulima wa Monduli juu kuhakikisha wanapolima wanawapatia mbegu na wanapovuna wananunua ngano yao yote.
"Kwa hiyo ile ngano ina soko tayari, na soko lao ni sisi bodi ya Nafaka na Mazao mchanganyiko ambapo tutainunua yote kwa bei nzuri hivyo tuna uhakika taratibu zote zikifuatwa na wataalam wetu watakuwa shambani kuanzia mwanzo wakati wa kuandaa mashamba, upandaji na utunzaji mpaka mwisho wanapovuna, alisema Kiluwasha na kuongeza ..
...Tunatarajia kwamba zao mbegu hizi zitafanya vizuri na wakulima watafaidika kwa kupata mavuno mengi yenye ubora unaokubalika,".
MBEGU ZIMEAGIZWA ZAMBIA
Kiluwasha alisema kuwa wameshirikiana na kampuni ya mbegu ya Seed Co Tanzania limited kuagiza mbegu hizo zinazozalishwa na kampuni hiyo nchini Zambia ambazo wanawauzia wakulima shilingi 2,900 kwa kilo moja.
Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Seed.Co, ukanda wa Afrika Mashariki, Clive Mugadza alisema kuwa kampuni yake italeta wataalam wake wawili watakaopita kwenye maeneo ya mashamba ya wakulima waliuziwa mbegu hizo kwa ajili ya kuwapatia elimu na ujuzi zaidi juu ya namna bora ya kulima ngano hiyo ili iwe na matokeo mazuri.
Aliwashukuru CPB na serikali kwa ujumla kwa kuiamini kampuni yao na kufanya kazi pamoja huku akisifu namna taasisi nyingine za serikali zinazohusika na kuangalia ubora ikiwemo shirika la viwango nchini, TBS walivyofanya shughuli hiyo vizuri na kuwezesha mbegu hizo kuwafikia wakulima kwa wakati.
Mugadza alisema kuwa kampuni hiyo imejipanga kuanza kuzalisha mbegu hizo hapa nchini ambapo itashirikiana na wakulima wadogo ambao watawapa elimu namna bora ya kuzilima na kuvuna kisha wao watazinunua na kumalizia kuziandaa kwenye kiwanda chao cha mbegu kilichopo Kisongo, Arusha.
Hata hiyo imeelezwa itakuwa na manufaa kwa wakulima kwani bei ya mbegu itapungua huku wakulima watakaokuwa kwenye programu ya kulima ngano kwa ajili ya mbegu hizo wakinufaika kwa kupata soko la uhakika la mazao yao.

0 Comments:
Post a Comment