Shinikizo la damu na magonjwa ya moyo yameendelea kuwa tishio kubwa kwa afya ya wananchi, baada ya kubainika kuwa kati ya wananchi takribani 3,000 waliojitokeza katika kambi ya uchunguzi wa afya ya moyo na magonjwa yasiyoambukiza kwa mikoa ya Kanda ya Kaskazini, asilimia 25 waligundulika kuwa na shinikizo la damu huku asilimia 9 wakibainika kuwa na matatizo ya moyo.



Taarifa hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge, leo Jumanne Januari 06, 2025, wakati wa ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Amos  Makalla, aliyefika kukagua zoezi hilo la uchunguzi na matibabu bure katika Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (Seliani).


Dkt. Kisenge amesema changamoto ya shinikizo la damu imeonekana kuwaathiri zaidi wananchi wenye umri wa kuanzia miaka 45 hadi 80, hali inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na mtindo mbaya wa maisha ikiwemo kutofanya mazoezi ya mwili, unene uliokithiri, ulaji usiozingatia lishe bora, unywaji wa pombe kupita kiasi na uvutaji wa sigara.


Ameeleza kuwa ulaji mkubwa wa vyakula vya wanga hususan nyakati za jioni bila kufanya mazoezi husababisha nishati hiyo kubadilika kuwa mafuta mwilini na kuongeza hatari ya kupata magonjwa yasiyoambukiza, ikiwemo shinikizo la damu na magonjwa ya moyo.


Akizungumzia mustakabali wa huduma za moyo mkoani Arusha, Dkt. Kisenge amesema ujenzi wa Kituo cha JKCI katika Hospitali ya Seliani utaimarisha upatikanaji wa huduma za kibingwa kwa wananchi wa Arusha na mikoa ya jirani, pamoja na kuwahudumia watalii na washiriki wa Michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON) itakayofanyika mkoani Arusha mwaka 2027.


“Nichukue fursa hii kuwahimiza wananchi kupima afya zao mara kwa mara, hasa afya ya moyo. Ndiyo maana JKCI imeamua kutembea mikoa mbalimbali nchini kutoa huduma za uchunguzi wa moyo bure,” amesema Dkt. Kisenge.



Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Arusha,  AmosMakalla, ameishukuru JKCI kwa kufungua kituo cha huduma za moyo mkoani Arusha, akisema hatua hiyo itapunguza rufaa kwenda Dar es Salaam na kuwasaidia wananchi kupata matibabu kwa wakati.


Makalla amesema wananchi wasiokuwa na uwezo na watakaopata rufaa ya matibabu zaidi watawezeshwa na Serikali ili kupata huduma za kibingwa katika Taasisi ya Moyo JKCI Dar es Salaam, huku akihamasisha wananchi kujiunga na mifumo ya bima ya afya kwa wote.



Wananchi wa Mkoa wa Arusha na mikoa ya jirani wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha programu ya vipimo na matibabu bure ya magonjwa ya moyo, wakisema imekuwa msaada mkubwa kwa wananchi wenye kipato cha chini na wale waliokuwa hawajawahi kupima afya ya moyo hapo awali.


 


Mwandishi wetu Endulen Ngorongoro.

Tarehe  20 Desemba, 2025


Uhusiano kati ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na jamii inayoishi ndani ya eneo la hifadhi umeendelea kuimarika kufuatia ziara za Kamishna wa Uhifadhi wa NCAA, Bw. Abdul-Razaq Badru katika vijiji mbalimbali vilivyoko tarafa ya Ngorongoro ambapo leo tarehe 20 Desemba,2025  ametembelea Kata ya Enduleni, wilayani Ngorongoro.



Akiwa ameambatana na baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya Ngorongoro na Diwani wa Kata ya Endulen Mhe. Elias Sakara Nagol, Kamishna Badru ameeleza kuwa, lengo la ziara hiyo ni kuendelea kuimarisha uhusiano kati ya Uongozi wa hifadhi ya Ngorongoro na jamii, pamoja na kukagua maboresho ya miundombinu ya maji inayotumika kwa  matumizi ya wananchi, mifugo na wanyamapori.



Katika ziara hiyo Kamishna Badru amewaeleza wananchi wa vijiji vya Kata ya Enduleni kuwa Mamlaka inatekeleza Miradi ya Maji katika kata za Endulen, Kakesio, Olbalbal na maeneo mengine na  aliwahimiza wananchi kushiriki kikamilifu katika usimamizi na utunzaji wa miradi hiyo ambayo inagharimu fedha za Serikali.



Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Enduleni, Dkt. Elias Sakara Nagol, amempongeza Kamishna Badru na wasaidizi wake kwa kuendeleza uhusiano  ya karibu na jamii inayoishi ndani  kwa kuwatembelea mara kwa mara, kusikiliza kero zao na kushirikiana nao katika masuala mbalimbali ya kijamii na kuahidi kuwa wananchi wataendelea kuwa mabalozi wazuri wa kutunza na kulinda hifadhi kupitia programu ya uhifadhi shirikishi.



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe, ameonesha kuridhishwa na kasi, ubora na usimamizi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa ndani ya Jiji la Arusha, akisisitiza kuwa miradi hiyo inapaswa kukamilika kwa wakati bila kuongezewa muda.



Akizungumza jijini Arusha leo Alhamisi, Desemba 18, 2025, wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku mbili mkoani Arusha, Waziri Shemdoe amesema ziara hiyo imelenga kukagua na kutathmini utekelezaji wa miradi ya kimkakati inayotekelezwa kupitia Mradi wa Uendelezaji Miji Tanzania (TACTIC) pamoja na miradi mingine ya maendeleo ya Jiji la Arusha.

Katika ziara hiyo, Waziri alitembelea na kukagua ujenzi wa Soko la Kilombero, uwanja wa mpira, Soko la Morombo, jengo la Utawala la Jiji la Arusha pamoja na Kituo Kikuu cha Mabasi kinachojengwa Bondeni City. Miradi hiyo inalenga kuboresha huduma za kijamii, kuimarisha mazingira ya biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa jiji.

Waziri Shemdoe amesema miradi hiyo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 30 inaonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuleta maendeleo kwa wananchi wa Arusha.

Amesema kasi ya utekelezaji wa miradi hiyo inaonesha usimamizi mzuri na uwajibikaji wa viongozi na watendaji wa Jiji la Arusha, hali inayochangia matumizi bora ya fedha za umma na kukamilika kwa miradi kwa viwango vinavyokubalika.

Aidha, Waziri Shemdoe ameuagiza uongozi wa Jiji la Arusha kuhakikisha wafanyabiashara waliokuwepo awali katika Soko la Kilombero wanapewa kipaumbele mara baada ya soko hilo kukamilika, huku akisisitiza uwazi na haki katika zoezi la ugawaji wa vizimba.



Ameonya dhidi ya vitendo vya baadhi ya watendaji au viongozi kuchukua vizimba na kuvikodisha kwa wananchi kwa maslahi binafsi, akisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa yeyote atakayekiuka maelekezo hayo.



Kwa upande wake, Meya wa Jiji la Arusha, Maximilian Matle Iranghe, amesema jiji litaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati, kwa ubora unaotakiwa na kwa kuzingatia malengo ya Serikali na matarajio ya wananchi.

Meya Iranghe ameishukuru Serikali Kuu na Wizara ya TAMISEMI kwa ufuatiliaji na ushirikiano unaoendelea, akisisitiza kuwa miradi hiyo itachangia kuongeza ajira, mapato ya jiji na kuboresha maisha ya wakazi wa Jiji la Arusha.



MAMLAKA ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) imetoa mafunzo kwa Mawakala wa Forodha waliopo Mpaka wa Namanga, wilayani Longido mkoani Arusha, kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa maombi ya vibali vya kuingiza na kutoa mazao nchini kupitia Dirisha Moja la Mfumo wa Tanzania Customs Integrated System (TANCIS), uliounganishwa kutoka mfumo wa awali wa e-Kilimo.



Akizungumza wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika Disemba 18, 2025 Namanga wilayani Longido, Afisa Kilimo wa COPRA Kanda ya Kaskazini, 

 Peter Kabelelo, alisema kuwa katika kuboresha utoaji wa huduma za vibali, Wizara ya Kilimo imeunganisha Mfumo wa e-Kilimo na Mfumo wa Tanzania Customs Integrated System (TANCIS) ili mifumo hiyo iweze kusomana.


Alisema lengo la hatua hiyo ni kurahisisha na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za vibali ambazo hapo awali zilikuwa zikiombwa kupitia mfumo wa e-Kilimo. Alifafanua kuwa hapo awali mteja alihitajika kutumia mifumo mbalimbali kutoka taasisi tofauti ili kupata huduma moja, kama vile COPRA, TPHPA na TANCIS.


“Maboresho yaliyofanyika yamewezesha kuunganishwa kwa mifumo hiyo ili mteja atumie mfumo mmoja tu wa TANCIS kupata huduma kutoka taasisi mbalimbali kama COPRA, hivyo kurahisisha zaidi utoaji wa huduma,” alisema Kabelelo.

Aliongeza kuwa faida nyingine ya matumizi ya mfumo huo ni kupatikana kwa takwimu sahihi za mazao yote yanayosafirishwa nje au kuingia nchini, pamoja na kujua thamani ya mazao hayo kwa usahihi.


Kwa upande wake, Afisa Biashara wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido, Bw. Rajabu Mmunda, alisema kuwa lengo la mafunzo hayo ni pamoja na kusikiliza maoni na changamoto za Mawakala wa Forodha kuhusu matumizi ya mfumo wa TANCIS.


Aliwashukuru mawakala hao kwa kushiriki mafunzo hayo na kueleza kuwa changamoto walizozitaja zitafanyiwa kazi ili kuhakikisha mfumo huo unawarahisishia utendaji wa kazi kama ilivyokusudiwa na Serikali.


Naye Wakala wa Forodha wa Kampuni ya A & ED Co. Ltd, Bw. Robynson Masai, aliishukuru COPRA kwa kuwapatia elimu hiyo, akisema kuwa mafunzo hayo yamewawezesha kuufahamu vizuri mfumo wa TANCIS na namna unavyofanya kazi.


Hata hivyo, aliomba COPRA kuendelea kuwa karibu na mawakala hao ili kusaidia kutatua changamoto za kimfumo pindi zinapojitokeza na wanapohitaji msaada wa haraka.


Aidha, Wakala wa Forodha wa Kampuni ya Njechele Co. Ltd, Petro Mveyange, aliomba COPRA kufungua ofisi katika Mpaka wa Namanga ili kurahisisha utatuzi wa changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa maombi ya vibali.

 


11 Desemba, 2025, Dodoma

Ofisi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetangaza kwa masikitiko kifo cha Mbunge wa Peramiho, Jenista Joakim Mhagama, kilichotokea leo tarehe 11 Desemba, 2025, Jijini Dodoma.

Katika taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Bunge, Msemaji wa Bunge, Mheshimiwa Mussc Azzan Zungu, ametoa pole kwa familia ya Marehemu, Waheshimiwa Wabunge, pamoja na wananchi wa Jimbo la Peramiho. "Kwa masikitiko makubwa, naomba kutangaza kifo cha Mbunge wa Peramiho, Jenista Joakim Mhagama. Natoa pole kwa Waheshimiwa Wabunge wote, familia ya Marehemu, ndugu, jamaa, na wananchi wa Jimbo la Peramiho. Mwenyezi Mungu awape moyo wa uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu," alisema Mheshimiwa Zungu.

Ofisi ya Bunge, kwa kushirikiana na familia ya Marehemu, inaendelea kuratibu mipango ya mazishi, na taarifa zaidi zitapatikana kadri zitakavyopatikana.

Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu mahali pema peponi. Amina.




Na Mwandishi wetu, Ngorongoro.


Jamii ya kabila la Wahadzabe inayopatikana pembezoni mwa Ziwa Eyasi Wilaya ya Karatu Mkoani Arusha ni miongozi mwa makabila yaliyopo katika mzunguko wa Jiopaki ya Ngorongoro Lengai. Jamii hii ni wanufaika wa mradi wa makumbusho mpya ya kijiolojia (Urithi Geopark) iliyopo katika mji wa Karatu.



Nchi ya Tanzania na barani Afrika kwa ujumla zipo kanuni na taratibu mbalimbali ambazo jamii au makabila hujiwekea kama njia ya kuenzi na kutunza mila na desturi zao.


Katika kabila la Wahadzabe (Watindiga) kwa wanandoa (mke na mume) kufanya tendo la ndoa na mtu mwingine nje ya ndoa (Kuchepuka) inatafsiriwa kuwa ni laana kubwa kwa kabila hilo ambapo mtu anayefanya kosa hilo na ikathibitika adhabu yake ni kuuwawa na mtu aliyewafumania (aliyewashuhudia) kisha akishatekeleza mauji anapiga ukunga au yowe ili jamii ikusanyike na wazee wa kimila kutoa taarifa rasmi kwa jamii kuhusu kitendo hicho ambacho kinatafsiriwa kuwa ni kuleta laana na nuksi kwenye familia. 



Njia inayotumika kuwaua waliochepuka ni kuchomwa na mishale yenye sumu mwilini Mithili ya mnyama anayewindwa, Mishale inayotumika ina sumu kali ambayo huenea haraka kwenye mwili wa mwanadamu na kupoteza maisha ndani ya muda mfupi.


Katika maisha ya mapenzi na ndoa kwa jamii ya wahadzabe zipo kanuni mbalimbali ambazo wamejiwekea ikiwemo kila mwanaume anayeoa na mwanamke anayeolewa kuheshimu ndoa yake na kuepuka kwa vyovyote vile kushiriki tendo la ndoa na mwanamke au mwanaume mwingine.



Baada ya kuoana bibi na bwana harusi hutakiwa kuishi kwa upendo na jamii hufuatilia ndoa hiyo ili kuhakikisha kuwa hakuna mtu miongoni mwao anayefanya tendo la ndoa nje ya mwenza wake, jamii hiyo ipo makini katika kufuatilia mienendo ya wanandoa ili kuhakikisha kuwa usalama wa familia unakuwepo katika kipindi chote cha ndoa hiyo.


Mchakato wa kuwaua wanandoa waliochepuka haufanyiki kwa kukurupuka bali uchunguzi na ufuatiliaji wa kina hufanyika mpaka pale watu wanaoaminika watakapowashuhudia watuhumiwa wakiwa katika kilele cha ndoa hiyo.


Kwa mujibu wa Kiongozi wa Mila za Wahadzabe Mzee Shagembe Gambai Jamii hiyo imeweka utaratibu huo wa kuwaua watu wanaochepuka ili kuimarisha nidhamu za familia, ukoo na jamii kwa ujumla ndio maana hadi sasa utaratibu huo umezoeleka na kuheshimiwa hivyo ni nadra sana kusikia mhadzabe akichepuka.


Katika kuhakikisha kuwa kila mmoja anajifunza ubaya wa kuchepuka zoezi la kuwaua waliofumaniwa hufanyika hadharani likishuhudiwa na jamii yote ya eneo hilo wakiamini kuwa kitendo hicho kinatoa darasa kwa wanandoa wengine kuacha tabia hiyo.


Mzee Shagembe anasimulia kuwa Ndoa kwa jamii ya wahadzabe si suala la kufa na kuzikana laah hashaa, jamii hiyo huruhusu kuachana na ikitokea hivyo unaruhusiwa kuoa au kuolewa na mtu mwingine hata kama huyo unayeanza naye uhusiano upya ni mtu wako wa karibu au rafiki wa aliyekuwa mwenza wako.


Jamii ya Wahadzabe hawaamini katika ndoa za mke zaidi ya mmoja, Kwao ndoa ya mke na mume mmoja tu na hairuhusiwi mwanaume kuoa mke zaidi ya mmoja sababu kubwa ikiwa ni kuimarisha upendo kwa wale walioamua kuishi kama mke na mume.

 



Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimefungua kesi namba 56 ya mwaka 2025 katika Mahakama ya Haki ya Afrika Mashariki, likilalamikia hatua ya Serikali ya Tanzania kuzima mtandao wa intaneti kuanzia tarehe 29 Oktoba hadi tarehe 4 Novemba 2025. LHRC inadai kuwa kuzimwa kwa mtandao kulileta madhara makubwa kwa wananchi na kilikiuka haki za kikatiba na za kimataifa.

Katika ombi lao, LHRC inaiomba Mahakama iiamuru Serikali ya Tanzania isizime mtandao tena bila kufuata taratibu za kisheria, ikiwa ni pamoja na kuwa na kifungu cha sheria maalum au amri ya mahakama. Kituo hicho pia kinataka Mahakama itoe tamko kwamba kuzimwa kwa mtandao kilikiuka vifungu vya Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, hususan vifungu 6(d), 7(2), na 8(1)(c), na kwamba hatua hii ilikosa uhalali wa kisheria.

Kuzimwa kwa mtandao, kulikodumu kwa siku saba, kulisababisha usumbufu mkubwa kwa Watanzania, wakiwemo kupoteza fursa za kupata huduma za kibenki mtandaoni, huduma za afya mtandaoni, na taarifa muhimu kuhusu usalama, hasa wakati wa uchaguzi mkuu. LHRC inasisitiza kuwa kuzimwa kwa mtandao hakukulenga kupunguza vurugu kama ilivyodaiwa na serikali, bali kilikuwa ni kitendo cha kupindukia na kinyume na miongozo ya kidemokrasia.

Aidha, LHRC inaiomba Mahakama itoe amri ya kudumu ya kuzuia Serikali kuzima mtandao tena bila kuwa na kifungu cha sheria cha kuiwezesha kufanya hivyo, na pia itoe amri ya radhi kwa umma wa Watanzania kwa madhara yaliyojitokeza kutokana na kuzimwa kwa mtandao.

Inatarajiwa kuwa Mahakama ya Haki ya Afrika Mashariki itapokea majibu kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Tanzania ndani ya siku 45 baada ya kupokea ilani ya kufunguliwa kwa kesi hii.

  

Happy Lazaro,Arusha 

Shirika linajishughulisha na uhifadhi wa Tembo la WILD SURVIVORS  waja na teknolojia ya kisasa ya utatuzi wa migogoro kati ya Tembo na jamii zinazopakana na hifadhi.


Hayo yamesemwa jijini Arusha leo na Afisa miradi ya jamii wa shirika hilo,Masalu John Masaka wakati akizungumza na waandishi wa habari katika kongamano la 15 la kisayansi la TAWIRI  linalofanyika jijini Arusha .




Amesema kuwa lengo  la kushiriki kongamano hili  ni kuwaambia watu kazi wanazofanya ili kufanikisha hizi kazi za utatuzi wa migogoro kati ya tembo na jamii zinazopakana na hifadhi 

Amefafanua kuwa, lengo la kuanzishwa kwa shirika hilo ni kuhakikisha kwamba jamii zinazopakana na hifadhi zinaishi kwa amani na Tembo kwa kutumia njia rafiki kama mizinga ya nyuki .



Aidha ametoa wito kwa jamii  pamoja na wahifadhi kufanya kazi pamoja kwa kukutumia njia rafiki ili tuweze kuishi pamoja na tembo kwani idadi ya watu inapoongezeka na idadi wanyama inapoongezeka ardhi haiongeki ,hivyo tunahitajika kufanya kazi kwa pamoja  wakiwemo jamii iliyoathiriwa wahifadhi pamoja na wanyamapori.




" Tunafanya kazi zaidi za kuhifadhi Tembo kwa namna ambayo tunatatua migogoro kati ya Tembo na wakulima wanaopakana na hifadhi ."amesema Masaka .


"Tumekuja hapa kwenye mkutano huu kwa ajili ya kuwaeleza watu shughuli ambazo tunazifanya kwa mfano tunatumia mizinga ya nyuki ambayo inatoa mazao kama asali ambayo inakuwa faida kwa vikundi  vya akinamama katika vijiji ambavyo tunafanya kazi."amesama Masaka .



"Tumekuja pia kwenye huu mkutano kwa lengo la kueleza watu namna ambavyo tunakusanya data  na tunatumia vifaa gani tunatumia kamera  pamoja na teknolojia ya simu ambayo tunakuwa na application inayoitwa survey one two three tunatumia kukusanya data ."amesema .



Amefafanua kuwa tangu shirika lianzishwe wamepiga hatua kwani wameshaweka uzio wa mizinga  ya nyuki zaidi  ya kilometa 20 katika maeneo mbalimbali kwani wana uzio wa nyuki kilometa saba upande wa Ngorongoro vijiji vya wilaya ya Karatu na kilometa sita kwa upande wa serengeti na kilometa sita katika vijiji vya Rukwa katavi vijiji ambavyo vinapatikana na hifadhi ya Taifa Katavi .


"Tumeona mabadiliko yapo matukio ya Tembo kuingia mashambani  na kula mazao ya wakulima yamepungua na tumeona katika vijiji ambavyo tumefanya navyo kazi mwanzoni  ikiwemo Ngorongoro wakina mama wameanza kupata kipato kutokana na mazao ya nyuki ."amesema .



"Tunawafundisha na tunawapa mafunzo  ya namna ya kuweka uzio wa mizinga ya nyuki namna ya kuvuna mazao ya nyuki na na namna ya kuchakata na kuwaunganisha  na soko ."amefafanua  Masaka .



"Kwa uchunguzi ambao tumefanya ni kuwa tembo anawaogopa nyuki hivyo anavyokaribia karibu na mzinga wa nyuki na anapousukuma ule waya ambayo umeunganisha mzinga mmoja hadi mwingine  na nyuki anapotikiswa wakiwa na asali wale nyuki walinzi wanatoka nje kuangalia kitu ambacho kinataka kuchukua mazao yake ba wale nyuki wanapotoka nje wanatoa ile sauti na tembo akisikia anaamua kuondoka."ameongeza Masaka .



 


Wananchi wa Kitongoji ya Ormekeke Kijiji cha Nasipaoriong tarafa ya Ngorongoro wameanza kunufaika na mradi wa maji baada ya Serikali kupitia Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kuchimba kisima chenye uwezo wa kuzalisha lita 13,00 kwa saa na kujenga tanki  lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita 135,000 kwa ajili ya matumizi ya binadamu na mifugo.



Akiwa katika ziara ya kukagua utekelezaji wa mradi huo Kamishna wa Uhifadhi Ngorongoro Abdul-Razaq Badru ameeleza kuwa kukamilika kwa mradi huo kรผmeleta  manufaa makubwa  kwa wananchi wa maeneo ya Ormekeke, Nasipaoriong na Olduvai yaliyopo hifadhi ya Ngorongoro ambao kipindi cha kiangazi walilazimika kuhamishia mifugo maeneo ya mengine kufuata maji


“Mradi huu tuliuanza kwa  kuwashirikisha wananchi ikiwa ni utekelezaji wa kuboresha mahusiano ya NCAA na jamii kwa kutatua changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo ambalo moja wapo ni maji, umeshakamilisha na kitongoji cha Ormekeke wameanza kutumia maji, rai yangu kwa wananchi ni kulinda na kusimamia miundombinu ya mradi huu kupitia kamati za maji na mazingira ambazo wameshaziunda” alisema  Kamishna Badru.



Mwenyekiti wa Kitongoji cha Ormekeke Bw.  Oreteti Olenjorio ameeleza kuwa eneo la kitongoji hicho ni kame na halina chanzo chochote cha maji hivyo uamuzi wa Serikali kupitia mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro kuchimba maji ni msaada mkubwa kwa matumizi ya wananchi na mifugo na kuahidi kulinda miundombinu ya mradi huo  kupitia jumuiya za maji na kuzingatia sheria za hifadhi.



Kwa mujibu wa Msimamizi wa Mradi huo Mhandisi Godlove Sengele pamoja na mradi huo kunufaisha wananchi na mifugo yao pia utahudumia Makumbusho ya Olduvai, Leakey Camp, Mtui Camp, Nyumba za Maaskari pamoja na jamii ambayo imejengewa vituo vinne vya kuchotea maji na vituo vitatu vya kunyweshea mifugo.




Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Profesa Palamagamba Kabudi, asema tawasifu ya Balozi Daniel Ole Njoolay ni hazina ya kipekee itakayodumu kwa vizazi vijavyo—hasa ikizingatiwa kwamba safari yake ya elimu, utumishi na uongozi imejaa miujiza, majaribu makubwa na ushindi uliopatikana kwa juhudi na uhodari.





Ameyasema hayo katika hafla ya uzinduzi wa kitabu cha Balozi Njoolay kilichofanyika Novemba 29, 2025 katika ukumbi wa Corridor Spring Hotel jijini Arusha kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, akiwemo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushurukiano wa Afrika Mashariki, James Millya, mabalozi na viongozi wastaafu.



  Prof. Kabudi alisema maisha ya Balozi Njoolay—hasa safari yake ya elimu na uongozi—yamejaa miujiza, vikwazo, ujasiri na maamuzi magumu yaliyojenga msingi wa mafanikio yake.


Katika hotuba hiyo yenye msisitizo mkubwa wa thamani ya kumbukumbu na usomaji wa vitabu, Prof. Kabudi alimshukuru Mungu kwa kuwezesha tukio hilo muhimu, huku akipongeza uthubutu wa Balozi Njoolay kuandika kitabu kinachoeleza simulizi ya maisha yake kuanzia utotoni hadi safari yake katika utumishi wa umma na diplomasia.



Alisema kitabu hicho ni zawadi muhimu kwa taifa, akibainisha kuwa ni wachache mno wenye moyo wa kuandika na kurithisha maarifa yao. Alikumbusha pia mazingira magumu aliyoyapitia Balozi Njoolay wakati jamii ya Maasai ilipokuwa ikiona elimu si jambo la lazima, hadi pale serikali ilipolazimisha watoto kwenda shule.



Prof. Kabudi aliwataka vijana na Watanzania kwa ujumla kusoma kitabu hicho ili kuishi na kujifunza kupitia uzoefu huo wa kipekee. Alihusisha umuhimu huo na desturi yake binafsi ya kusoma hotuba za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, akisema kuwa tawasifu na hotuba hizo bado zinatoa mwanga mkubwa katika zama za leo.


Akinukuu hotuba ya Nyerere ya mwaka 1965 iliyowasisitiza vijana kujenga na kulinda taifa, Prof. Kabudi alieleza kuwa taifa linaweza kudidimia kama vijana hawajengi misingi thabiti ya uzalendo, maadili na dhamira ya kulihudumia.


Katika kuhimiza usomaji wa vitabu, Prof. Kabudi aliainisha manufaa kadhaa ikiwemo kupanua maarifa, kuchochea ubunifu, kuimarisha maadili na kuongeza uwezo wa kujenga hoja na kufanya maamuzi sahihi. Aliitaka jamii, hasa familia, kuwahamasisha watoto na vijana kusoma vitabu kama sehemu ya malezi na ujenzi wa fikra.


Kwa waandishi wa vitabu, aliwasihi kuendelea kuandika bila kukata tamaa licha ya changamoto ya wananchi wengi kutopenda kusoma. Aliwatia moyo kwamba kila kitabu ni chombo cha maarifa kitakachowanufaisha wengi katika siku za usoni.


Prof. Kabudi alimpongeza Balozi Njoolay kwa uzalendo na utumishi wake uliotukuka, akisema amekuwa mfano bora wa kuigwa na viongozi pamoja na vijana nchini. Pia alishauri kitabu hicho kisambazwe kwa njia za kidijitali ili kuwafikia wasomaji wengi zaidi ndani na nje ya Tanzania.


Baada ya hotuba hiyo, Waziri Kabudi alizindua rasmi kitabu cha Balozi Daniel Ole Njoolay, akiitimisha shughuli hiyo kwa wito wa kuenzi na kuishi hekima iliyomo katika kurasa zake.


 



Katika hafla ya uzinduzi wa kitabu chake Tawasifu ya Balozi Daniel Ole Njoolay, iliyohudhuria na viongozi mbalimbali wakiwemo Mgeni Rasmi, Prof. Palamagamba Kabudi, Waziri wa Habari; pamoja na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, James Millya, Balozi Daniel Ole Njoolay alitoa risala yenye kugusa hisia kuhusu maisha yake, safari ya elimu na utumishi wake kwa umma.



Balozi Ole Njoolay alieleza kuwa chanzo cha kitabu hicho:
“Uamuzi wa kuandika kitabu hiki nilichukua miaka mitatu iliyopita, baada ya msukumo wa marafiki wengi ambao kwa muda mrefu walinishauri kufanya hivyo. Baadhi yao wapo hapa leo. Kitabu hiki kinaeleza maisha yangu na utumishi wangu kwa umma, safari ambayo kwa sehemu kubwa imejaa miujiza.”

Safari ya Elimu Katika Mazingira Magumu



Balozi Njoolay alisimulia changamoto za kupata elimu katika jamii ya Kimasai kipindi hicho, ambako wazazi walikataa watoto kwenda shule wakiamini ni sawa na ‘kuwapoteza’.

“Wazee walipokubaliana angalau kila boma litoe mtoto mmoja, mzazi alichagua mtoto ambaye si ‘rasilimali kubwa sana’. Mimi nilichaguliwa kwa sababu nilikuwa sichungi mbuzi vizuri,” alisema kwa utani uliochekesha ukumbi.


Alieleza kuwa alipoanza shule, mzazi alilazimika kulipa ada mwaka mmoja baada ya kuanza masomo. Baada ya baba yake kufariki dunia, watu walimwambia mama yake aache kumsomesha kwa kuwa alikuwa mjane.
“Hata hivyo, mama yangu hakukata tamaa. Nilipofaulu kwenda sekondari, aliniuliza kama nataka kuendelea. Nilimwambia ndiyo, akaniambia basi tuuze ng’ombe iliyobaki. Huo ndio ulikuwa msingi wa safari yangu.”

Uongozi Bila “Godfather”



Akimweleza hadhira jinsi alivyoingia kwenye uongozi, Balozi Njoolay alisema matukio mengi katika maisha yake yalikuwa ya kipekee.
“Nilishinda ujumbe wa NEC (Vijana) nikiwa na miaka 29. Nilikuwa mgeni kabisa ndani ya chama, lakini nikaomba kura kwa mara ya kwanza na nikachaguliwa,” alisema.

Aliendelea kueleza kuwa uteuzi wake kuwa Mkuu wa Mkoa kwa miaka 16 ulikuwa “maajabu mengine”, na zaidi ni uteuzi wake kuwa Balozi licha ya kutokuwa mwanadiplomasia kwa taaluma.
“Walioniteua waliridhika na utendaji wangu, na wananchi waliridhika na utendaji wangu. Huo ndio ulikuwa msingi wa safari yangu ya uongozi.”

Shukrani kwa Mwandishi

Katika risala hiyo, Balozi Njoolay alimpongeza na kumshukuru mwandishi mkongwe wa habari, Bw. Hassan Hassan.
“Amebeba jukumu kubwa katika uandishi wa kitabu hiki. Amefanya kazi kwa uadilifu na umakini mkubwa,” alisema.

Wito kwa Vijana na Wasomaji

Balozi Njoolay alisema lengo lake kuu ni kuwainua na kuwapa dira vijana wa sasa, hasa wale wanaotamani kutumikia taifa.
“Baadhi ya watu walinisukuma kuyaandika haya ili viongozi vijana wapate kujifunza. Ni imani yangu kwamba mtafurahia kukisoma na huenda mkafaidika nacho. Mungu awabariki sana,” alihitimisha.

Uzinduzi huo uliendelea kwa furaha na tafakuri, huku hadhira ikionyesha kuthamini mchango wa Balozi Ole Njoolay—kiongozi ambaye safari yake ni somo la ujasiri, kujituma na uaminifu katika utumishi wa umma.


 


Arusha, Tanzania — Uzinduzi wa kitabu Tawasifu ya Balozi Daniel Ole Njoolay umefanyika jijini Arusha na kuhudhuriwa na viongozi wa Serikali, wabunge, wanadiplomasia, wasomi, viongozi wa dini, pamoja na wananchi kutoka maeneo mbalimbali.



Katika hafla hiyo, Salim Salim, kwa niaba ya kamati ya maandalizi, aliwasilisha muhtasari wa yaliyomo ndani ya kitabu hicho na kusisitiza kuwa ni miongoni mwa kazi bora zaidi za kihistoria na kiwasifu kuwahi kuandikwa na mtumishi wa umma nchini Tanzania.



Akiwasilisha muhtasari huo, Salim alisema kwamba mara tu alipokianza kitabu hicho, hakutaka kukiweka chini kwa sababu simulizi za Balozi Njoolay zinamvuta msomaji kutoka ukurasa mmoja hadi mwingine.

“Balozi anafanana na wazee wetu wa zamani ambao walikuwa mabingwa wa kutoa hadithi. Daniel is a master storyteller,” alisema.

Sifa za viongozi wakuu wa Taifa



Katika muhta
sari wake, Salim alinukuu maneno ya viongozi wakuu wa nchi yaliyomo kwenye kitabu hicho, ikiwemo Dibaji iliyoandikwa na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Joseph Sinde Warioba, ambaye alimwelezea Balozi Njoolay kama kiongozi wa mfano wa kuigwa.

Katika maneno yake yaliyohifadhiwa mwishoni mwa kitabu, Mhe. Warioba anasema:

“Sifa zake ni mfano wa kuigwa. Amefanya kazi ndani ya umma kwa bidii, ubunifu, uadilifu na uaminifu… nimekisoma kitabu hiki kwa msisimko. Kina mengi ya kujifunza, hasa kwa vijana wanaoanza maisha ya utumishi na uongozi.”

Salim pia alinukuu maneno ya Rais Mstaafu Benjamin William Mkapa (apumzike pema peponi), aliyewahi kumwambia Balozi:

“Mkuu, ninachokupendea huwa unasema ukweli hata kama ule ukweli unaniumiza.”

Zaidi ya tawasifu ya kawaida



Salim alifafanua kuwa kitabu hicho hakisimulii tu historia ya maisha ya Balozi Njoolay, bali kinafundisha maadili, unyenyekevu, uongozi na misingi ya utu wa mtu. Alisema maneno tawasifu au wasifu hayatoshi kueleza uzito wa yaliyomo ndani ya kitabu hicho.

“Kitabu hiki ni ushuhuda hai (a living testimony) wa jinsi Daniel alivyojibu kwa ukarimu wito wa kutumikia na kushirikiana na Muumba. Kina kusukuma kufikiri, kujiangalia, na kutathmini ubora na udhaifu wa maisha yako,” alisisitiza.

Alikilinganisha kitabu hicho na kazi kubwa za viongozi maarufu duniani kama Nelson Mandela (Long Walk to Freedom), Barack Obama (Dreams from My Father), na Mahatma Gandhi (All Men Are Brothers), akisisitiza kuwa kitabu cha Ole Njoolay nacho kina nafasi ya kutafsiriwa kwa Kiingereza siku zijazo.

Hazina kwa Taifa

Mwisho wa hotuba yake, Salim Salim alisema wazi kuwa Balozi Daniel Ole Njoolay ni hazina muhimu kwa Taifa la Tanzania, na kwamba bado kuna haja kubwa ya kuendelea kumtumia katika majukumu ya kitaifa.

Akihitimisha, alinukuu maneno ya Mchungaji Martin Luther King Jr.:

“Swali kuu la kujiuliza maishani ni hili: Unawafanyia nini watu wengine?”

“Mhe. Daniel anaelewa uzito wa swali hili, na amelifanyia kazi kwa kiwango cha juu sana. Lakini haya yote hayatoshi kusimuliwa—ni lazima usome kitabu mwenyewe,” aliongeza.

Uzinduzi huo mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Habari Prof. Palamagamba Kabudi ambapo viongozi mbalimbali walihudhuria akiwemo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, James Millya, Mbunge wa Arumeru Magharibi, Dr Lukunay,  viongozi wa Chama Cha Mapinduzi, ( CCM) , viongozi wa umma wastaafu  na watu mashuhuri. 



Waziri wa Maliasili na utalii Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) ameelekeza taasisi za uhifadhi kuimarisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika uhifadhi na ulinzi wa rasilimali za wanyamapori ili kupunguza migogoro kati ya binadamu na wanyamapori.



Dkt. Kijaji ametoa maelekezo hayo leo tarehe 28 Novemba, 2025 wakati akizungumza na Menejimenti ya Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro wakati wa ziara ya kujitambulisha kwenye taasisi na kukagua utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Mamlaka hiyo.



Katika kikao hicho . Waziri Kijaji ameelekeza kuwa kila taasisi ni lazima iwekeze kwenye teknolojia za kฤฑsasa ili kuimarisha ulinzi wa rasilimali za nchi ambazo ni kichocheo cha wageni mbalimbali kutembelea nchi yetu.



Kwa upande wake naibu waziri wa wizara hiyo Hamad Hassan Chande amewataka watumishi katika sekta ya uhifadhi na utalii kufanya kazi kwa kuzingatia weledi na ubunifu katika kuwahudumia wageni.



Akiwatambulisha viongozi hao kwa menejimenti ya Ngorongoro Katibu Mkuu wa wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi amewataka watumishi wa mamlaka hiyo kutoa ushirikiano wa kutosha ili kuharakisha mipango ya serikali inatekelezwa.



Mapema viongozi hao wa wizara walipata fursa ya kukagua ujenzi wa Makao makuu ya mamlaka hiyo, kukagua shughuli za utalii katika lango La Loduare na Makumbusho ya kihistoria ya Urithi ya Jiopaki ya Ngorongoro (Urithi Geo Museum)

 


Arusha — Donkeys in Tanzania are facing a serious threat of extinction due to illegal cross-border trade that involves secretly transporting the animals out of the country, the Animal Welfare Association of Tanzania (ASPA) has warned.



Diana Msemo, Animal Welfare Education Officer at ASPA, issued the alert during a media training held over the weekend in Arusha. She explained that the growing demand for donkey skins has fueled a dangerous black market, causing a sharp decline in donkey populations.

Msemo noted that donkeys are the second most important livestock species in Tanzania—after cattle—due to their significant contribution to the national economy and the daily lives of pastoralist communities.

“There is a high demand for donkeys, especially in neighboring countries like Kenya, where they are secretly slaughtered. Donkeys are smuggled out of Tanzania through unofficial routes and end up in the skin trade,” she said.

Donkeys, commonly used for farming, transportation, and domestic chores, play a crucial role in supporting pastoralist families. Msemo emphasized that donkeys are not only work animals but also essential to children in pastoralist households, enabling them to fulfill daily duties and attend school.



ASPA’s Community Development Officer, Albert Mbwambo, stressed the need for communities to recognize the importance of donkeys and protect them. “Despite the rapid loss of donkeys, we must continue educating the public on the dangers of this illegal trade and ensure these animals are preserved and valued,” Mbwambo said.

ASPA is working with partners such as BROOKE East Africa to advocate for animal welfare and raise public awareness of the consequences of the illegal donkey trade.