Showing posts with label Barabara. Show all posts
Showing posts with label Barabara. Show all posts

 


Mawasiliano ya barabara kati ya Jiji la Mwanza na Mkoa wa Shinyanga yamekatika usiku wa kuamkia leo baada ya daraja la Mkuyuni kusombwa na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa iliyonyesha katika maeneo hayo. 

Hali hii imezua usumbufu mkubwa kwa wakazi na wasafiri kutoka mikoa mbalimbali, ambao walikumbana na msongamano wa magari na kushindwa kufika katika maeneo yao kwa wakati.

Changamoto ya Daraja la Mkuyuni

Daraja la Mkuyuni limekuwa likikumbwa na changamoto za muda mrefu, ambapo lilikuwa likifanyiwa ujenzi wa upanuzi na serikali kupitia mkandarasi. Hata hivyo, ujenzi huo umecheleweshwa kwa muda mrefu, hali ambayo imeongeza usumbufu kwa wananchi na wasafiri. 


Leokadia James, Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Amani, alieleza masikitiko yake kuhusu kucheleweshwa kwa mradi huo akisema:

“Haiwezekani kwa zaidi ya miezi minne sasa mkandarasi bado anachezea hapa. Usumbufu umekuwa mkubwa, serikali iwajibike au imlipe mkandarasi kama wanadai hawajamlipa,” alisema James.

Serikali Yatoa Ahadi ya Kukamilisha Ujenzi

Kwa mujibu wa Mhandisi Pascal Ambrose, Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mwanza, serikali imetenga Shilingi bilioni 5.5 kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo, ambapo ujenzi ulianza mwezi Januari 2025 na unatarajiwa kukamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu. 


Mhandisi Ambrose alisisitiza kuwa, licha ya changamoto zilizojitokeza, serikali inaendelea kuhakikisha kuwa mradi huu unakamilika kwa wakati.

“Serikali imejizatiti kuhakikisha kuwa kazi inaendelea, na tutafanya kila liwezekanalo ili daraja hili likamilike kwa haraka,” aliongeza.

Mvua Zasababisha Athari Nyingine Kusini

Katika maeneo mengine, mvua kubwa ya masika pia ilisababisha athari kwa miundombinu ya barabara, ambapo mwishoni mwa wiki, daraja la Cheketu Somanga lilisombwa na maji, na kusababisha mawasiliano kati ya Lindi na Dar es Salaam kukatika. 


Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, alithibitisha kutokea kwa hali hiyo na kutoa taarifa kuwa barabara hiyo imefunguliwa baada ya matengenezo ya dharura.

“Kuanzia sasa barabara ya kutoka Dar es Salaam kwenda mikoa ya kusini imefunguka rasmi lakini magari yanayopita ni madogo na yale ya abiria,” alisema Waziri Ulega.

Upanuzi wa Daraja la Mkuyuni Uendelee

Mradi wa ujenzi wa daraja la Mkuyuni umeendelea kukumbwa na changamoto, lakini Mwakilishi wa Kampuni ya Jasco, Nestory James, alisema kuwa walilazimika kubadili mchoro wa awali wa daraja ili kuzingatia ukubwa wa mafuriko yaliyokuwa yakitokea. 


Alieleza kuwa ujenzi utaendelea sasa baada ya mabadiliko hayo, na mradi utakapokamilika, utaondoa kabisa changamoto ya mafuriko katika eneo hilo.

“Awali, usanifu ulionekana kuwa lijengwe daraja la kawaida, lakini kutokana na changamoto ya maji kuwa kubwa, tumelazimika kuchora mchoro mwingine na tayari umekamilika. Ujenzi utaendelea na mradi utakapokamilika, utawezesha kingo za mto na daraja hili kuinuliwa, jambo litakaloondoa kabisa changamoto ya mafuriko,” alisema James.


Ingawa kumekuwapo na changamoto kubwa katika utekelezaji wa miradi hii ya barabara na madaraja, hatua za kiserekali zimeanza kutekelezwa ili kuhakikisha mawasiliano yanarejea kuwa ya kawaida. 


Wakazi na wasafiri wanatarajia kuwa miradi hii itakapokamilika, itakuwa suluhisho la kudumu kwa matatizo ya mafuriko na usumbufu wa usafiri katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Kusini.




Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Camillus Wambura amesema Jeshi la Polisi limeweka mikakati madhubuti ya kudhibiti ajali za barabarani ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyokuwa akiyatoa mara kwa mara ya kuhakikisha ajali za barabarani zinadhibitiwa ipasavyo.



IGP Wambura ameyasema hayo wakati akipokea vifaa 3050 kati ya 10000 vya kupima ulevi kwa madereva kutoka Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) vilivyokabidhiwa na Mkurugenzi wa LATRA, CPA Habibu Saluo, Makao Makuu ya Polisi Jijini Dodoma Januari 6, 2025.


IGP Wambura alisema kupitia Kikosi cha Usalama barabarani watakuwa wakali kwa madereva wazembe ambao wamekuwa wakisababisha ajali za barabarani ambapo pia wataendelea kutoa elimu ili kuhakikisha kuwa watanzania wanakuwa salama.


"Tumeweza kuzuia uhalifu wa aina mbalimbali na sasa nguvu pia tunazielekeza kwenye usalama barabarani kwa kuwa takwimu za ajali bado zipo juu hivyo ni lazima tuwe wakali sana ili kuona sheria za usalama barabarani zinafuatwa ili kuokoa maisha ya watanzania," alisema IGP Wambura.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) CPA Habibu Suluo amesema, utendaji kazi wao unahitaji sana ushirikiano kutoka Jeshi la Polisi ambalo ndilo lenye dhamana ya kusimamia Sheria za Usalama Barabarani na hivyo vipima ulevi hivyo vitasaidia Kikosi cha Usalama Barabarani katika kudhibiti ajali za barabarani zinazosababishwa na madereva walevi na wazembe pindi wanapokuwa barabarani na kuendesha pasipo kuzingatia sheria.


CPA Suluo alisema uwepo wa vifaa hivyo utasaidia kupima madereva mara kwa mara wawapo barabarani jambo ambalo litasaidia kufanya barabara zetu kuwa salama.


Aidha alisema wataendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo matumizi ya mifumo katika kufanya ukaguzi wa magari ambapo kwa sasa wanaendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika maeneo mbalimbali.


Hafla ya makabidhiano ya vifaa hivyo ilihudhuriwa na Makamishna wa Polisi, Manaibu Kamishna wa Polisi, baadhi ya Makamishna Wasaidizi Waandamizi wa Polisi na Maofisa kutoka LATRA.


Mhandisi Seff aelezea uwezo wa daraja hilo


Berega, Kilosa



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kiasi cha Shilingi bilioni 1.2 zilizobaki wakati wa ujenzi wa Daraja la Berega zitumike kuboresha barabara ya Berega - Kinyolisi - Makuyu kwa kujenga daraja moja la mawe lenye urefu wa Mita 45 (stone arch-bridge), Ma-boksi Kalavati. 


Fedha hizo pia zitajenga Madrifti 6, na kuweka changarawe katika maeneo korofi ili barabara hiyo iweze kupitika katika majira yote ya mwaka ambapo kazi hiyo ya maboresho ya barabara imeanza.


Dkt. Samia aliyasema hayo jana wakati akiongea na wananchi wa Berega ikiwa ni muendelezo wa ziara yake Mkoani Morogoro.


Alisema barabara hiyo ya kiwango cha changarawe itaanzia ng’ambo ya daraja hilo mpaka Kijiji cha Makuyu Km. 18.7 inapounganika na barabara ya Gairo -Kilindi inayohudumiwa na TANROADS.


“Injinia amesema hapa wamefanya matumizi mazuri sana ya fedha kwenye ujenzi wa daraja hili na zimebaki Shilingi bilioni 1.2 ambazo zinakwenda kutumika kuboresha barabara ya kiwango cha changarawe, kujenga madaraja sita na makaravati 15, hivyo kuifanya iweze kupitika wakati wote.


Aidha, alisema anaamini barabara hiyo itaweza kupitika misimu yote na kurahisisha usafiri wa binadamu na bidhaa zao.


Naye, Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff alisema kwamba daraja hilo limesanifiwa kuwa na uwezo wa kubeba tani 120 kwa wakati mmoja na kudumu kwa miaka isiyopungua 100.


Aliongeza kusema kuwa daraja hilo limejengwa kwa zege na nondo na linabebwa na nguzo mbili za pembeni (aburtments) na nguzo sita za katikati (Piers),”nguzo zote zimejengwa juu ya msingi wa nguzo ndefu 67 (piles) zenye kina cha wastani wa mita 15 kutoka usawa wa kitanda cha mto”.


Hata hivyo alisema ujenzi wa daraja hilo umehusisha pia kazi za kuzuia mmomonyoko wa udongo pembezoni mwa mto. 


Daraja la Berega lina urefu wa mita 140 na upana wa mita 10.5, mita 7.5 kati ya hizo ni kwa ajili yakupitisha magari na mita 3.0 yaani mita 1.5 kila upande ni mabega ya daraja kwa ajili ya usalama wa watembea kwa miguu na waendesha baiskeli.