Watengeneza Maudhui 450 Arusha Wapigwa Msasa Kunufaika na Uchumi wa Ubunifu

 


ARUSHA: Serikali imewahimiza watengeneza maudhui nchini kuchangamkia fursa za uwezeshaji zinazotolewa ili kukuza taaluma zao na kujiimarisha kiuchumi kupitia sekta ya ubunifu inayokua kwa kasi.



Rai hiyo imetolewa jijini Arusha Aprili 8, 2026  na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo, Kelvin Kanje, wakati akifunga mafunzo maalum yaliyoshirikisha zaidi ya watengeneza maudhui 450. 



Mafunzo hayo yaliandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania.



Kanje Aliwapongeza watengeneza maudhui hao kwa kushiriki mafunzo kwa awamu ya kwanza, akiahidi kuwafikia watengeneza maudhui katika mikoa mingine.



Aidha, amewataka Watengeneza Maudhui walioshiriki mafunzo kwa awamu va kwanza kutumia mafunzo havo kuboresha kazi zao ili ziwaingizie kipato.



"Kwa wale mnaoanza mafunzo haya yatawasaidia kuinuka na wale ambao tayari mmeanza mfanye vizuri zaidi," amesema Kanje.



 Nidhamu ya Fedha na Mikopo

Akizungumza katika mafunzo hayo, Mkurugenzi Msaidizi wa Haki za Wasanii, Dk. Asha Mshana, alibainisha kuwa ongezeko la watengeneza maudhui ni fursa kubwa ya ajira, lakini mafanikio yake yanategemea nidhamu ya kifedha na uelewa wa kibiashara.

"Mfuko wa Utamaduni na Sanaa unatoa mikopo bila upendeleo kwa lengo la kuwawezesha wabunifu. Ni wajibu wa wanufaika kutumia fedha hizo kwa malengo yaliyokusudiwa na kurejesha kwa wakati ili kuendeleza mzunguko wa kuwainua wengine," alisisitiza Dk. Mshana.



Ubora wa Maudhui na Maadili

Mbali na usimamizi wa fedha, washiriki walihimizwa:


 Kuzingatia ubora wa kazi zao ili kushindana kimataifa.

 Kutumia lugha za kimataifa ili kupanua wigo wa soko lao.

 Kulinda maadili na usalama wa taarifa binafsi katika majukwaa ya kidijitali.



 Balozi wa Nishati Safi ya Kupikia

Katika hatua nyingine, Mhandisi Benezeth Kabunduguru kutoka Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia, aliwaomba wabunifu hao kutumia ushawishi wao kuelimisha jamii kuhusu matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira.

Alieleza kuwa kupitia video fupi na vichekesho, wasanii wana nafasi kubwa ya kuunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kufikia asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.



Akihitimisha mafunzo hayo, Kanje aliwapongeza washiriki kwa kujitokeza kwa wingi na kuwasisitiza kushirikiana na taasisi mbalimbali za serikali na binafsi ili kuboresha kazi zao na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

0 Comments:

Post a Comment