Wosia wa Papa Francis: “Nataka Kupumzika Karibu na Mama Yetu Bikira Maria”

 



Katika hali ya unyenyekevu na imani thabiti, Papa Francis aliacha wosia wake tarehe 29 Juni 2022 – maandiko yenye uzito mkubwa kiroho, yaliyotolewa hadharani baada ya kifo chake, yakifichua wito wake wa mwisho kuhusu mahali pa kupumzika milele.


Imani Thabiti kwa Bikira Maria

Katika utangulizi wa wosia wake, Papa Francis alianza kwa kumtaja Mungu Mtakatifu kwa maneno:

"Kwa jina la Utatu Mtakatifu. Amina."

Akiwa na utulivu wa kiroho na matumaini ya maisha ya milele, aliandika kwa dhati:

“Ninapotambua kufika kwa machweo ya maisha yangu ya duniani, na kwa tumaini thabiti katika maisha ya milele, nataka kuweka wazi matakwa yangu ya mwisho kuhusu mahali pa mazishi yangu.”

Akiwa na upendo wa kipekee kwa Bikira Maria, Mama wa Yesu, ambaye alimwamini maisha yake yote na huduma yake kama kasisi na askofu, Papa aliomba apumzike karibu naye:

“Katika maisha yangu yote, na wakati wa huduma yangu ya kipadre na uaskofu, nimejitoa kila mara kwa Mama wa Bwana wetu, Bikira Maria. Kwa sababu hii, naomba kwamba mabaki ya mwili wangu yapumzike – yakisubiri siku ya Ufufuo – katika Kanisa Kuu la Kipapa la Maria Mkuu (Basilika ya Santa Maria Maggiore).”

Safari ya Mwisho Kuelekea Mahali pa Sala

Katika wosia huo, Papa Francis alieleza kwa undani hisia zake kuhusu mahali hapo takatifu, akisema:

“Ninapenda safari yangu ya mwisho ya duniani iishie mahali hapa pa kale pa Bikira Maria, ambapo kila mara nilisimama kusali mwanzoni na mwisho wa kila safari yangu ya Kitume.”

Aliendelea kueleza kuwa hapo ndipo alipokuwa akiweka mbele ya Mama Bikira Maria sala na nia zake zote kabla ya safari, na kumshukuru kwa upendo wake wa kimama kila aliporudi.

Kaburi Rahisi Lenye Maana Kubwa

Akitilia mkazo unyenyekevu ambao ulikuwa alama ya maisha yake yote, Papa Francis alitoa maagizo maalum kuhusu kaburi lake:

“Naomba kaburi langu liwe kwenye eneo la mazishi lililo upande wa ukuta, kati ya Kanisa la Pauline (Kapela ya Salus Populi Romani) na Kapela ya Sforza, kama inavyoonyeshwa kwenye ramani niliyoiambatisha.”

Alihitaji kaburi lake liwe rahisi:

“Kaburi hilo liwe ardhini; rahisi, lisilokuwa na mapambo maalum, likiwa na maandishi haya pekee: Franciscus.

Aidha, alieleza kuwa gharama za maandalizi ya mazishi hayo zitalipwa kupitia mchango wa mfadhili aliyeshajitolea, na kwamba:

“Nimewaelekeza wahusika kuhakikisha fedha hizo zinapelekwa kwa Basilika ya Santa Maria Maggiore.”

Alimtaja Kardinali Rolandas Makrickas, Kamishna Maalum wa Basilika hiyo, kama mtu aliyekabidhiwa maagizo haya.


Sadaka ya Maumivu kwa Amani Duniani

Katika maneno yake ya mwisho ya kiroho, Papa Francis alihitimisha wosia wake kwa kugusa nyoyo:

“Bwana awape thawabu mwafaka wote waliyonipenda na wanaoendelea kuniombea.”

Akigusa mateso aliyoyapitia katika miaka ya mwisho ya maisha yake, aliyaweka mikononi mwa Mungu kama sadaka:

“Mateso yaliyoashiria sehemu ya mwisho ya maisha yangu, nayatoa kwa Bwana, kwa ajili ya amani duniani na udugu kati ya watu.”

Urithi wa Imani, Unyenyekevu na Huruma

Wosia huu wa Papa Francis si tu hati ya kisheria ya Kikristo, bali ni kielelezo cha maisha aliyoyaishi kwa ajili ya wengine. Aliishi kwa unyenyekevu, akahudumu kwa huruma, na sasa amepumzika kwa amani katika mahali alipopapenda zaidi – karibu na Mama Bikira Maria, mlezi wake wa milele.

Katika jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu – Amina.


0 Comments:

Post a Comment