SAMIA AONYA WANAOKIMBILIA MARUPURUPU KWENYE MASHIRIKA YA UMMA


RAIS Samia Suluhu Hassan amesema kuwa anataka kuona mashirika ya umma yasiyotegemea kuchukua kodi za wananchi serikalini ili kujiendesha ambapo ameyataka  yajiendeshe kwa faida ili kuchangia bajeti ya nchi .

 

Aidha amesema kuwa lengo hilo litafikiwa baada ya kufanyika mabadiliko ya kiutendaji, kisera na kisheria ikiwemo kuondoa kuingiliwa kisiasa katika utendaji wa mashirika haya, sheria za manunuzi, na mikataba sahihi ya kiutendaji kati ya serikali na wale tunaowakabidhi kuendesha mashirika haya. 

 


Rais Samia ameeleza hayo leo tarehe 19 Agosti, 2023 wakati  akifungua kikao kazi cha Wenyeviti wa Bodi na Watendaji Wakuu wa Taasisi na Mashirika ya Umma jijini Arusha.

 

‘Mageuzi na maboresho haya kwa mashirika yetu ya umma ni ya lazima, na ninawapa baraka zangu zote na ushirikiano katika utekelezaji wake. Watendaji tuliowapa dhamana ya kuongoza mashirika haya waende na kasi hii ya mageuzi ili kufikia malengo ya Serikali katika kuwatumikia Watanzania. Wale wasioweza, mlango wangu uko wazi, waje waniambie, ‘Mama siwezi’,” amesema Rais Samia na kuongeza

 

…Mjizatiti kuzalisha na kufanya mashirika yasimame, kama ni shirika la huduma litoe huduma tunayoiona , kama ni shirika la biashara litoe biashara tunayoiona..Lakini mashirika yamekuwa ni sehemu ya kula raha, na ndio maana juzi tulikuwa tunazungumza Waziri wa Utumishi akasema jamani pale kwangu Utumishi nina vita, kila mtu anataka kuhama Serikalini kwenda  kwenye mashirika, kisa kuna marupurupu mazuri, mishahara minene lakini hakuna tija kwa Serikali, sasa hatuwezi kwenda hivyo,".

 

Rais Samia amesema kuwa ndoto ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu, Julius Nyerere katika kuanzishwa kwa mengi ya mashirika hayo ilikuwa kuona yanamilikiwa na umma wa Watanzania, yanaendeshwa kwa tija na yasiyo mzigo kwa wananchi.

 

“Hivi sasa tuna mashirika, taasisi na wakala za umma takribani 248, zenye mtaji wa shilingi Trilioni 73 lakini zinachangia chini ya asilimia 4 ya bajeti ya nchi yetu. Japo yapo baadhi ya mashirika yanayojitahidi kufanya vizuri, bado hatujafikia ndoto njema ya Baba wa Taifa kwa nchi yetu, na tunahitaji kufanya maboresho na mabadiliko makubwa ya uendeshaji wa mashirika haya ili kutoka hapa tulipo,” amesisitiza Rais Samia. 

 

 

 

 


0 Comments:

Post a Comment