SERIKALI; PSPTB DHIBITINI WANAOKIUKA MAADILI YA MANUNUZI NA UGAVI

 



SERIKALI imeahidi kuendelea kuunga mkono juhudi  za Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) , zinazolenga kuondoa uzembe na ukiukwaji wa maadili katika fani ya ununuzi na ugavi kwani pesa nyingi za serikali zinatumika kupitia taaluma hiyo.


Aidha imeitaka kumchukulia hatua madhubuti  mtaalamu yeyote atakayethibitika anakiuka kanuni za maadili au kutoa ushauri wa ununuzi kinyume na sheria ya ununuzi wa umma kwani ni  uzembe na ukosefu wa weledi  katika kusimamia mnyororo wa   ununuzi na ugavi unapelekea kukwamisha utekelezaji wa miradi na  miradi mingi   kufanyika chini ya kiwango.




Hayo yalisemwa leo Desemba mosi, 2021 jijini Arusha na Waziri wa Fedha na Mipango, Mwigulu Nchemba katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongela wakati akifungua kongamano la 12 la wataalamu hao.


Alisema kuwa bado kuna wataalamu wachache wanafanya  kazi chini ya kiwango cha taaluma yao hivyo akaiagiza  bodi ya PSPTB kuendelea  kusimamia taaluma hiyo kwa kuchukua hatua madhubuti kuinua weledi wa wataalamu hao pamoja na wengine wote wanaoshiriki katika mchakato wa ununuzi na ugavi kwa kuwajengea uwezo katika taratibu za manunuzi na usimamizi wa mikataba .



" Mada mliyoiweka katika  kongamano hili, inayosema ubunifu wenye suluhisho katika utekelezaji wa mnyororo  wa ununuzi na ugavi kwa kutambua  ushindani na mapinduzi ya viwanda kwa maendeleo ya jamii  itaipa changamoto  bodi ya   PSPTB na wataalam kuweza kutambua  umuhimu wao katika utekelezaji wa miradi mikubwa  ya kimkakati inayotekelezwa na serikali ili kuweza kuongeza tija na faida  katika sekta binafsi,"  alisema waziri Nchemba.



Alisema kuwa kuwepo kwa ukiukwaji mkubwa wa maadili kwenye kada hii iwe chachu   ya bodi kuongeza usimamizi wa maadili na kuchukuwa hatua stahiki kwa wahusika kwani taaluma hii ni muhimu sana ili kufikia adhima ya serikali  ya awamu  ya sita ya kuendelea kuwaletea watanzania maendeleo kwa kasi .



Waziri huyo wa Fedha na Mipango, alitoa wito kwa waajiri wote kutoa ushirikiano  kwa bodi hasa linapokuja swala la usimamizi wa taaluma ya ununuzi na ugavi pamoja kuzingatia matakwa yote na sheria za bodi ili kuleta tija ya miradi mbalimbali inayotekelezwa na serikali.


Alisema kuwa katika taasisi nunuzi 85 zilizofanyiwa ukaguzi kwenye viashiria vya rushwa  miradi mitatu yenye kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 616.5 ilibainika kuwa na viashiria vikubwa vya rushwa ukilinganisha na taarifa ya mwaka 2018/2019 ambayo iliobainika  kuwa ukaguzi wa miradi 131 ulionyesha kuwa na miradi 39 ilikuwa na viashiria vya rushwa .


Waziri Nchemba alisema kuwa kwa mujibu wa ukaguzi  uliofanywa na mamlaka ya uthibiti wa manunuzi ya umma  (PPRA) kwa mwaka wa fedha 2020/2021 umethibitisha kuwa ukaguzi wa mikataba 282 yenye dhamani ya zaidi ya  shilingi bilioni 5000.7 na mikataba 281 sawa na asilimia 99.6 imesimamiwa vizuri na kuleta dhamani ya fedha  huku mkataba mmoja ulionyesha kuwa na usimamizi wa  kiwango cha chini  sana.


Awali Mkurugenzi mtendaji  wa  PSPTB , Godfred Mbayi aliishukuru serikali kwa kumteua, Jacob Kibona kuwa mkurugenzi wa bodi ya wakurugenzi wa taasisi hiyo kwani kwa miaka mitatu nafasi hiyo ilikuwa wazi hali iliyokwamisha baadhi ya mambo katika utendaji wa taasisi hiyo.


 Alisema kuwa kwa mwaka 2021 wamesajili jumla ya wataalam 1,166 ambapo wamefanya mitihani  katika hatua tatu tofauti bila kutangaza kutokana na kutokuwa na bodi ya wakurugenzi  na idadi hiyo imefanya  idadi ya  wataalamu kuongezeka na kufikia  zaidi ya wataalam  elfu 12.


"Hata hivyo ndugu mgeni rasmi, tunazo 'session' tatu zilizofanya mitihani bila kutangazwa kutokana na kutokuwa na mkurugenzi wa bodi ya wakurugenzi ya wakurugenzi kitendo hicho kimewaathiri vijana wengi na maafisa walio kazini, hasa katika promosheni na ajira kwa vijana," alisema Mbayi


Akimkaribisha Waziri Nchemba kuzungumza na  wataalam hao, mwenyekiti wa bodi, Kibona alisema kuwa  atafanya kazi kwa weledi uliotukuka kwa kipindi chote  cha nafasi yake  na kumaliza matatizo yote ambapo bodi itahakikisha inachukuwa hatua kali za kinidhamu kwa wataalumu wote watakao sababisha watu kupoteza imani na taasisi hiyo ya ununuzi na ugavi



0 Comments:

Post a Comment