SABAYA NA WENZAKE SITA WASOMEWA MASHITAKA UPYA

 

 

ALIYEKUWA Mkuu wa wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na washitakiwa wenzake sita leo wakiongozwa na askari magereza kuingia kwenye mahakama ya wazi 

 

ALIYEKUWA Mkuu wa wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya, (34), wenzake sita wanaokabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi wamesomewa upya hati ya mashitaka ambapo kwa sasa wanakabiliwa na mashitaka matano.

 

Katika mashitaka hayo Sabaya anakabiliwa na mashitaka yote matano ya kuongoza genge la uhalifu, matumizi mabaya ya madaraka, kushawishi na kujipatia fedha kwa njia ya rushwa na kutakatisha fedha.

 

Washitakiwa sita waliobaki wakikabiliwa na mashitaka mawili kila mmoja ya kuongoza genge la uhalifu na utakatishaji fedha kinyume cha sheria.

 

Mawakili wa serikali na wale wa utetezi kwenye kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Hai, Lengai ole Sabaya na wenzake, sita wakiteta kabla ya kesi kuanza kwenye mahakama ya wazi 

Hati hiyo ya mashitaka imesomwa leo (Septemba 9, 2021) na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tarsila Gervas mbele ya hakimu mkazi, Dkt. Patricia Kisinda anayesikiliza shauri hilo la uhujumu uchumi namba 27/2021.

 

Washitakiwa hao walisomea mashitaka hayo baada ya upande wa jamhuri kuwasilisha mahakamani hapo hati na kibali maalum kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashitaka  Nchini, (DPP) zilizoipa  mamlaka mahakama hiyo kusikiliza shauri hilo ambalo linapaswa kusikilizwa kwenye mahakama kuu.

 

“Mheshimiwa hakimu kama ilivyokuwa amri ya mahakama ilikuwa bado ni kutajwa. Upelelezi umekwisha kamilika ni shauri la uhujumu uchumi mahakama yenye mamlaka ya kusikiliza ni mahakama kuu lakini mwendesha mashitaka ameona kwa maslahi ya umma shauri hili lisikilizwe na mahakama ya hakimu mkazi,” wakili mwandamizi Tarsila alieleza mahakamani hapo.

 

Aliwasilisha mahakamani hapo kibali na hati hiyo huku akirejea vifungu vya sheria ya uhujumu uchumi alivyovitumia kuleta (hati na kibali hicho) kwa ajili ya mahakama kuipa mamlaka mahakama hiyo kuendelea kusikiliza shauri hilo.

 

“Mheshimiwa hakimu kwa kuwa mahakama hii imeshakuwa na mamlaka ya kusikiliza shauri hili tunaomba kuwasilisha hati ya mashitaka ili washitakiwa waweze kusomewa mashitaka yanayowakabili,”  Wakili wa Serikali Tarsila  ameieleza mahakama hiyo.

 

Washitakiwa wengine kwenye shauri hilo ni pamoja na Enock Mnkeni, (41) maarufu  Dikdik, Watson Mwahomange, (27) maarufu Mamimungu, John Aweyo, maarufu  Mike One, Silvester  Nyengu, (26) maarufu Kicheche, Jackson Macha, (29) na Nathan Msuya, (31).


 

WASOMEWA MASHITAKA

 

Akiwasomea mashitaka hayo, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tarsila aliieleza mahakama hiyo kuwa, shitaka la kwanza linawakabilia washitakiwa wote saba  ni la kuongoza genge la uhalifu kinyume cha sheria ya uhujumu uchumi.

 

Akisoma maelezo ya kosa, Wakili huyo ameeleza kuwa, mnamo Januari 22, mwaka huu,  Sabaya akiwa  katika maeneo tofauti ndani ya jiji la wilaya ya Arusha  akiwa mtumishi  wa umma kwa nafasi ya mkuu wa wilaya ya Hai iliyopo mkoani Kilimanjar na anadaiwa kukiuka masharti yake ya ajira.

 

Sabaya anadaiwa kushirikiana na washitakiwa wenzake sita ambao si maafisa wa serikali lakini kwa makusudi kabisa walifanya vitendo vya uhalifu kwa kutumia nafasi ya Lengai ole Sabaya ambaye ni mtumishi wa umma na kujipatia fedha za Kitanzania shilingi milioni 90 kwa manufaa yao.

 

Katika Shitaka la pili linalomkabili Sabaya peke yake ni la kujihusisha na vitendo vya rushwa kinyume na sheria ya kupambana na kuzia rushwa.

 

Imedaiwa mahakamani hapo kuwa  mnamo Januari 22, 2021, Sabaya akiwa kwenye maeneo ya Kwamrombo yaliyo katika kwenye jiji na wilaya ya Arusha alijihusisha na vitendo vya rushwa kwa kumtaka Frances Mroso ampatie shilingi milioni 90 za Kitanzania.

 

Sabaya anadaiwa kushirikiana na washitakiwa wenzake sita kama kushinikiza kupatiwa kiasi hicho cha fedha ili wasitoe taarifa za jinai dhidi ya Mrosso ambapo kwa wakati huo walikuwa wakimtuhumu kwamba alikuwa na makosa ya ukwepaji kodi.

 

Kosa la tatu ni kujihusisha na vitendo vya rushwa, shitaka linalomkabili Sabaya peke yake anayedaiwa kuwa mnamo Januari 22, 2021 alijihusisha na vitendo vya rushwa kwa  alijipatia shilingia milioni 90 kutoka Frances Mrosso akishirikiana na washitakiwa wenzake sita katika kumshinikiza ili wasitoe taarifa ya kosa la jinai ambalo walimtuhumu nalo Mrosso.

 

Kosa la nne ni matumizi mabaya ya madaraka kinyume cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa ambalo linamkabili Sabaya peke yake ambapo anadaiwa mnamo Januari 22, 2021 akiwa kwenye maeneo ya Kwamromboo jijini na wilayani Arusha alitumia vibaya mamlaka yake ya ukuu wa wilaya ya Hai iliyopo mkoani Kilimanjaro.

 

Sabaya anadaiwa kwa makusudi kabisa alimtisha Mrosso kumfungulia mashitaka ya kukwepa kodi kinyume cha sheria za tawala za mikoa kwa madhumuni ya kujipatia  shilingi milioni 90 kwa faida yake na washitakiwa wengine sita.

 

Kosa la tano ni utakatishaji fedha  kinyume na sheria ambalo linawakabili washitakiwa wote saba ambapo wanadaiwa kuwa mnamo Januari 22, 2021 maeneo ya Kwamrombo

, wote kwa pamoja walijipatia fedha kiasi cha shilingi milini 90 wakati wakijua walipokuwa wakipokea fedha hizo ni zao la vitendo vya rushwa.

 

Washitakiwa wote walikana mashitaka yao hivyo wakili wa serikali mwandamizi, Tarsila aliomba mahakama ipange tarehe kwa ajili ya kuwasomea washitakiwa hao hoja za awali kuhusiana  na makosa yao.


Mawakili wa utetezi Moses Mahuna na Charles Abraham hawakuwa na pingamizi na ombi hilo.

 

Hakimu Mkazi, Dkt Kisinda aliahirisha shauri hilo mpaka Septemba 16,mwaka huu ambapo washitakiwa wote walirudishwa mahabusu kwenye gereza la Kisongo kutokana na mashitaka yanayowakabili kutokuwa na dhamana.

 

MWISHO

0 Comments:

Post a Comment