MKURUGENZI Mtendaji wa benki ya CRDB, Dk Charles Kimei amemwaga
machozi wakati akiwashukuru watendaji wa benki hiyo kwa ushirikiano
wanaompa unaomfanya apate sifa za kuiendesha benki hiyo kwa mafanikio.
Aidha wanahisa wa benki hiyo wameitaka bodi ya wakurugenzi ya benki hiyo kumuongezea
mkataba wa kazi Dk Kimei ili kutoa muda zaidi wa kumpata mtu sahihi wa
kushika nafasi hiyo huku wakiwaambia kama wataamua kujiuzulu kupinga
uamuzi huo wanahisa wako tayari kuchagua bodi mpya.
Hayo yalitokea Mei 19,mwaka huu wakati wa mkutano Mkuu wa 23 wa wanahisa wa
benki hiyo uliofanyika jijini hapa wakati Dk Kimei akimalizia kutoa
taarifa yake ya utendaji wa benki kwa mwaka 2017 huku akiwaeleza kuwa
ataendelea kuwepo kwani anastaafu Mei, mwakani kisha wanahisa kuanza
kuijadili.
Dk Kimei alisema kuwa kuna wakurugenzi 13 wa benki hiyo ambao
amefanya nao kazi ka ukaribu kwa muda mrefu pamoja na wafanyakazi wa
benki hiyo ndiyo siri ya benki hiyo kufanya vizuri ambapo alionekana
sauti yake kuanza kubadilika kisha kufuta machozi.
Wakichangia
taarifa yake ya utendaji wanahisa hao walisema kuwa kutokana na kazi
nzuri aliyofanya mkurugenzi mtendaji huyo hakuna ulazima wa kumuondoa
kwa haraka hasa kipindi hiki ambapo kuna ushindani mkubwa wa mabenki
hapa nchini.
Wanahisa hao walisema kuwa Dk
Kimei aongezewe muda wa kufanya kazi ili aandae mtu sahihi wa kushika
nafasi hiyo kwa kile walichodai kuwa mkurugenzi mtendaji huyo ndiyo
nguzo ya benki hiyo.
"Kimei ndiyo nguzo kubwa
ya CRDB kama Rais (john Magufuli) amemsifu wakiwa kule Chato wakati
wakifungua tawi la CRDB na kuahidi kumpa kazi endapo tutamuacha. Kama
Mkuu nchi amemsifu nyie mnasemaje ondoka? Mtu akitaka kuvunja nyumba
anaondoa nguzo kubwa," alisema mwanahisa Olle Sirikwa.
Alionya
kuwa kuna vita kubwa ya mabenki hapa nchini kwa sasa hivyo akawata
wanahisa wawe makini kwa kile alichodai kuwa kuondoka kwa Dk Kimei
kunaweza kusababisha athari kubwa kwa benki.
Wanahisa
hao walienda mbali wakidai kuwa mkutano mkuu ndiyo wenye maamuzi ya
mwisho juu ya masuala yote yanayoihusu benki hiyo hivyo kama bodi ya
wakurugenzi haikubaliani na hoja hiyo na kuamua kujiuzulu wafanye hivyo
na mkutano mkuu utachagua wajumb wapya wa kuunda bodi hiyo.
"Tukae
chonjo akiondoka huyu mtu baada ya miaka miwili tunaweza kuona vumbi
sisi wanahisa tunasema 'Kimei shall remain until further notice'
wakurugenzi msikasirike kwa sababu mkikasirika hatutawachagua," alisema
mwanahisa Ole Sirikwa na kuongeza.
"Na kama
mkikataa jiuzuluni tutachagua wengine, mwacheni Kimei akae mpaka amalize
vizuri akabidhi na mtu wa kushika nafasi yake,".
Aidha
mwanahisa mwingine alidai kuwa Dk Kimei tu ndiye mwenye uwezo wa kwenda
ikulu kufuatilia mikopo iliyotolewa kwa udhamini wa Serikali ambayo ni
mikubwa na mpaka sasa haijarejeshwa.
Aidha
walidai kuwa endapo italazimu Dk Kimei kustaafu kama alivyokwisha
tangaza basi mrithi wake atoke hapahapa nchini badala ya kuleta watu nje
ya nchi ambao watalazimika kukaa na kuanza kujifunza utamaduni wetu.
"Lazima
mrithi apatikane ndani ya benki yetu, haiwezekani hawa vijana wetu
waliofundishwa kazi washindwe kuchukua nafasi hiyo lakini kwa sasa Dk
Kimei aongezewe miaka miwili au mitatu ili amalizie hiki kipindi kigumu
cha uchumi ndipo aondoke," alisisitiza mwanahisa mmoja ambaye jina lake
halikuweza kupatikana mara moja.
Akijibu hoja
hizo Dk Kimei alisema kuwa, "Mimi siliagi ukiona nimelia ujue nilikuwa
'too emotional' ukipata furaha sana unalia na ukipata uchungu sana
unalia, naomba suala hili ( la kustaafu) lisisumbue watu umefika umri
fulani unastaafu lakini naamini mambo yanasikilizwa,".
BODI YASHIKILIA MSIMAMO
Kwa
upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi a benki hiyo, Ally Laay
aliwaeleza wanahisa hao kuwa waliwachagua ili waendeshe benki hiyo kwa
mujibu wa sheria ambapo walikuwa wakimpa Dk Kimei mkataba wa miaka minne
ambapo miaka ya nyuma alitaka kustaafu akamuongezea miaka miwili.
"Desemba
28, mwaka jana Dk Kimei alitokea kwenye media na kutangaza anajiuzulu
mei 2019 na sisi bodi tulitoa tangaza desemba 29, 2017 tukatangaza
mchakati wa kumpata mkurugenzi mtendaji," alisema Mwenyekiti huyo wa
bodi.
Alisema kuwa walifuata taratibu zote
zinazotakiwa ikiwemo kutoa taarifa kwa soko la hisa Dar es Salaam na
tumeajiri wataalam wa kusimamia zoezi la kupata mridhi wa Dk Kimei.
Laay
alisema kuwa japo Dk Kimei atastaafu lakini wataendelea kumtumia kwa
namna ambayo wataona inafaa huku akiwahakikishia wajumbe wa hisa kuwa
wanaamini watala waliowaajiri watawezesha kupatikana mkurugenzi mwenye
sifa kama za Dk Kimei au kumzidi.
0 Comments:
Post a Comment