WATETEZI WA HAKI ZA BINADAMU WAKEMEA YANAYOENDELEA ARUSHA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
Mkoa wa Arusha hususani Manispaa ya Jiji la Arusha ilijulikana kama “Geneva of Africa”. Hii ilitokana na ukweli kwamba ndani ya Manispaa ya Arusha watu mbali mbali wenyeji kwa wageni walikuwa na uhakika wa usalama wa maisha yao.
Hali hii imebadilika miaka ya karibuni na kuwa tofauti na ilivyokuwa ikijulikana kwa watu wengi ndani na nje ya nchi yetu ya Tanzania. Hali hii ya kulifanya jiji la Arusha kuendelea kupoteza hadhi yake ya kuwa “Geneva of Africa”, inatokana na wimbi la vikundi vya watu wanaosadikika kuwa vikundi vya kigaidi kuendelea kutishia amani na utulivu wa jiji hili la Arusha kwa urushaji wa mabomu ya mara kwa mara.
Siku chache zilizopita, tulishuhudia kupitia vyombo vya habari juu ya taarifa za shehe wa msikiti wa Suni kurushiwa bomu akila daku nyumbani kwake maeneo ya Majengo, mjini hapa. Wakati hilo halijatoka masikioni na akilini mwa wakazi wa Arusha na Tanzania kwa ujumla, usiku wa kuamkia leo (8/7/2014), tumesikia taarifa kupitia vyombo vya habari zilizotolewa na msemaji wa jeshi la Polisi nchini, akielezea kutupwa kwa bomu jingine na kuwajeruhi watanzania wanane wenye asili ya Kiasia pamoja na watoto wawili katika maeneo ya Gymkana karibu na Mahaka kuu ya Tanzania kanda ya Kaskazini, mkoa Arusha.
SLPC, tukiwa ni asasi ya kiraia inayotetea Haki za Binadamu tulizipokea taarifa za tukio hilo kwa masikitiko makubwa kwani kitendo hicho kinahatarisha Haki za Binadamu. Kutokana na hali hiyo, SLPC tunazitaka mamlaka husika za ulinzi kuhakikisha kuwa zinawasaka na kuwakamata wale wote waliohusika katika kitendo hicho na kuwafikisha katika vyombo vya sheria kama walivyofanya kwa wale waliohusika katika tukio jingine la bomu lililorusha katika baa ya Night Park miezi michache iliyopita mjini hapa. Endapo vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na raia, havitafanya jitihada za ziada kukomesha vikundi hivi vya ugaidi, ni dhahili kuwa  raia wasiokuwa na hatia wataendelea ama kupata ulemavu au kupoteza maisha yao na kukosa Haki ya Kuishi ambayo ni haki ya msingi ya Haki za Binadamu. SLPC, tunaamini kuwa vikundi vya ugaidi kama vile Alshababu, Bokoharamu na Al Qaida, vilianza kama vikundi vidogovidogo na leo ni makundi tishio katika nchi za Kenya, Nigeria na Iraq. Hivyo basi, SLPC tunaamini kuwa ikiwa kundi hili la watu ambao wanaendela kutumika katika vitendo hivi vya ugaidi hawatadhibitiwa na hatimaye kutokomezwa kabisa mapema, ni hakika kuwa wataleta madhara makubwa baadaye si kwa Jiji la Arusha tu bali kwa Tanzania nzima.
SLPC tunaamini kuwa vyombo vinavyosimamia ulinzi na usalama wa raia na mali zao,  vitahakikisha kuwa kundi hili la watu wachache wanaohatarisha usalama na Haki za Binadamu, litadhibitiwa mapema kabla halijaleta madhara makubwa.
SLPC tunahitimisha kwa kusema kuwa vyombo vya usalama na ulinzi, mwananchi mmoja mmoja, Asasi za kiraia na Taifa kwa ujumla tuungane kwa pamoja kuhakikisha kuwa tunawafichua wale wote wanaojihusisha kwa namna moja au nyingine katika vitendo hivi vya kigaidi. “Ni ukweli usiopingika kuwa bila usalama, hakuna Haki za Binadumu”. Aidha, SLPC, tunapenda kuwakumbusha wananchi wa Arusha na Tanzania kwa ujumla kuwa kulinda, kuhifadhi na kudumisha umoja wa taifa ni wajibu wa kila raia kama ilivyo katiba yetu ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, ibara ya 28(1).
Taarifa hii imetolewa na; MR. MASESA MASHAURI, Mwenyekiti -SLPC,
Simu Na. 0768 610580.

0 Comments:

Post a Comment