Katika kipindi hiki muhimu kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, viongozi wa dini nchini Tanzania wameungana kwa sauti moja wakisisitiza umuhimu wa haki, maridhiano na amani ya kweli. Wametumia madhabahu ya Pasaka kutoa kauli zenye uzito mkubwa kwa Serikali na vyombo vyake, wakitaka hatua za dhati zichukuliwe kuhakikisha siasa za nchi zinaendeshwa kwa misingi ya haki, uhuru na maridhiano.
TEC: Viongozi wa Kisiasa Waliokamatwa Waachiwe Bila Masharti
Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania (TEC), kupitia kwa Rais wake ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Katoliki Lindi, Mhashamu Wolfgang Pisa, limetoa wito kwa Serikali kuwaachilia mara moja na bila masharti viongozi wa kisiasa waliokamatwa kwa kudai haki.
“Amani ya kweli haiwezi kupatikana kwa kutumia nguvu bali kwa maridhiano na haki,” amesema Askofu Pisa, akiongeza kuwa ni wajibu wa kila Mtanzania kulinda amani kwa kuhakikisha mifumo ya uchaguzi inarekebishwa ili kutoa nafasi kwa upatikanaji wa viongozi wa haki na wa kweli.
DCT: Serikali na CHADEMA Wakutane Meza ya Mazungumzo
Askofu wa Kanisa la Anglikana, Dayosisi ya Central Tanganyika (DCT), Dkt. Dickson Chilongani naye amesisitiza kuwa suluhu ya kweli ya mvutano wa kisiasa ni mazungumzo ya pande husika.
“Tumesikia juzi pamoja na nchi yetu kuwa haina vita, lakini watu wake hawana furaha... Tungeomba viongozi wa pande zote mbili wakae pamoja wamalize tofauti zao kwa njia ya mazungumzo,” alisema Askofu Chilongani kwenye Ibada ya Pasaka katika Kanisa Kuu la Roho Mtakatifu, Dodoma.
Aliitaka Serikali kutatua kero kama rushwa, ubadhirifu na ukiritimba ambazo zinakwamisha ustawi wa taifa.
KKKT: Amani Isibebwe na Kauli Bali Matendo ya Haki
Askofu Shoo: Vyombo vya Dola Viheshimu Maamuzi ya Wananchi
Mkuu wa Dayosisi ya Kaskazini ya KKKT, Askofu Dkt. Fredrick Shoo, ametoa wito kwa vyombo vya dola, hasa Jeshi la Polisi, kuhakikisha havitumiki vibaya wakati wa uchaguzi.
“Ni wakati wa Tanzania kuandika historia mpya ya uchaguzi wa kidemokrasia unaozingatia amani, usawa na maridhiano ya kweli,” alisisitiza katika ibada ya Pasaka mjini Moshi.
Askofu Mwaikali: Tuombee Taifa, Tuchague Viongozi Wenye Hofu ya Mungu
Rais Samia: Pasaka Iwe Tafakari ya Upendo, Haki na Uadilifu
Kupitia salamu zake za Pasaka, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametoa wito wa kitaifa wa mshikamano na amani.
“Siku hii njema ikawe pia ya tafakari kwetu sote juu ya upendo wetu kwa Muumba wetu na wenzetu; juu ya kujitoa kwa bidii na weledi katika utekelezaji wa majukumu yetu... juu ya haki ambazo daima huambatana na wajibu,” ameandika Rais Samia.
Kauli hizi kutoka kwa viongozi wa dini zinaakisi uhitaji wa haraka wa maridhiano ya kitaifa, mazungumzo ya kisiasa, na utekelezaji wa haki katika mchakato mzima wa uchaguzi.
Kwa sauti moja, viongozi hawa wameweka mbele maslahi ya taifa, wakisisitiza kuwa amani ya kweli haiwezi kufanikishwa pasipo haki na usawa. Ni wakati wa kuisikiliza miito hii na kuchukua hatua stahiki kwa ajili ya mustakabali wa Tanzania.





0 Comments:
Post a Comment