AAIDRO KUWAINUA KIUCHUMI WANAWAKE ARUSHA DC

 


SHIRIKA lisilo la Kiserikali la Maendeleo na Msaada la kanisa Katoliki Jimbo Kuu Arusha, (AAIDRO), limeanza kutekeleza mradi wa zaidi ya shilingi milioni 230 kwa ajili  kusaidia kuwainua kiuchumi  wanawake, kuwapa elimu ya ujasiriamali na namna ya kukabiliana na ukatili wa kijinsia.

 


Mkurugezi Mtendaji wa AAIDRO, Padri, Faustine Mosha ameyasema hayo katikati ya mwezi huu wakati akimweleza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, Seleman Msumi juu ya utekelezaji wa mradi huo wa mwaka mmoja akiwa ameambatana na uongozi wa taasisi hiyo.

 

Amesema kuwa mradi huo wa majaribio umelenga kuwanufaisha wananchi 200 ambapo  Kanisa limeona ni vema kushirikiana na Serikali kuwahudumia wananchi katika sekta nyingine zaidi ya ile ya kiroho na kuongeza kuwa wanatarajia kupata ushirikiano mkubwa kutoka kwa watalamu wa halmashauri ili kutekeleza mradi huo ipasavyo.

 

Padri Mosha amesema kuwa idara ya maendeleo waliona ni vema wakapanua wigo kwa kuyaangalia makundi ya kijamii ya kimkakati  ikiwemo wanawake hasa kipindi hiki cha kuelekea jubilei ya miaka 60 tangu kuanzishwa kwa jimbo kuu la Arusha ambayo itaadhimishwa kuanzia mwakani mwezi machi.

 

“Tukampata huyo mhisani kutoka Ujerumani anayeitwa Misereor ambapo wamekubali kuwasaidia wanawake rasilimali fedha na ujuzi kidogo ili kuhakikisha idara hiyo ya kinamama inaweza kuwasaidia wanawake kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali yatakayowawezesha kujitambua katika suala zima la maendeleo ya jamii,” amesema Padri Mosha na kuongeza.

 

…Tukaona tulenge katika mkakati wa kuona wanawake wanatambua vizuri masuala ya haki zao, wanashirikishwa vizuti katika kutambua rasilimali walizonazo na namna ya kuzitumia na wao wenyewe kujitambua hivyo kuweze kuchochea maendeleo endelevu kwa mwanamke mmoja mmoja na jamii kwa ujumla,”.

 


Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, Msumi, amelishukuru Kanisa Katoliki na  AAIDRO kwa kuona umuhimu wa kuunga mkono juhudi za serikali za kuwajengea uwezo wananchi kujikwamua kiuchumi, kazi ambayo ingefanywa na serikali.

“Kama Hamashauri tuko tayari kushirikiana na kanisa kwa kuzingatia jukumu la serikali ni kuweka mazingira rafiki kwa mashirika yanayofanya kazi za kuhudumia jamii kulingana na mpango mkakati wa serikali, tunao watalamu wa kutosha katika idara zote, hivyo watashirikiana nanyi katika hatua zote za utekelezaji wa mradi huu,” amesema  Mkurugenzi huyo wa halmashauri ya Arusha.

 

Kwa upande wake mratibu wa mradi huo, Irene Mosha, Amesema mradi huo uko chini ya Idara na Mradi wa wanawake na Maendeleo,  (WIDGAD) ambapo utawawezesha wanawake kiuchumi katika masuala ya kilimo, kukuza biashara zao, usawa wa kijinsia, kupinga ukatili kwa wanawake ikiwemo ndoa za utotoni na mambo mengine yanayofanana na hayo.

 

Amesema kuwa mradi huo utawanufaisha wananchi wa kata za Nduruma na Bwawani kwenye vijiji vya Mzimuni, Kigongoni Themi ya Simba na Bwawani ambapo utatekelezwa kwenye awamu tatu na kwa sasa uko katika hatua za awali  ukitarajiwa kukamilika  ifikapo Juni 2023.

 

 “Kupitia mradi huu tunategemea kuwaiwezesha jamii kuwa na uwezo wa kujikomboa kifkra, uwezo wa kujitegemea kiuchumi katika kujipatia pato la familia, pamoja na kuwa na jamii huru isiyokuwa na ukatili wa aina yoyote katika masuala ya kijinsia,” amesema Moshi.

Mtaalam Mshauri wa AAIDRO, Rafael Kajuna amesema kuwa wamekuwa na miradi kadhaa ya kusaidia wananchi waliyowahi kuitekeleza kwenye maeneo ambayo waliridhishwa kwa namna wananchi walivyoipokea na kuiendeleza ndiyo sababu wakaona ni vema wakaelekeza miradi mingine kwenye maeneo hayo.

 

Mjumbe wa bodi ya AAIDRO, Isaya Doita amewasihi watendaji mradi huo na wale  halmashauri wafanye kazi iliyokusudiwa kwa uaminifu ili kuwezesha kufikiwa malengo yatakayosaidia kupatikana kwa mtafi mkubwa utakaowanufaisha wananchi wengi zaidi.

 

 

0 Comments:

Post a Comment