MALKIA WA UHOLANZI AKOSHWA NA BIMA PIMA KWA WAKULIMA




MALKIA Maxima wa Uholanzi ameelezea kuridhishwa na namna taasisi ya kutengeneza bima ya mazao na mifugo,(ACRE Afrika) nchini Tanzania ilivyowawezesha wakulima kupata fidia ya mazao kutokana na janga la ukame kupitia 'bima pima'.






Ameyasema hayo leo, Oktoba 18, 2022 wakati akijadiliana na  wakulima wa mahindi kwenye Chama Cha Msingi Cha Ushirika cha Uduru Makoa kilichopo Kata ya Machame Kaskazini, wilayani Hai, mkoani Kilimanjaro.

 


Malkia Maxima ambaye alionekana kuuliza maswali mengi wakulima hao ameelezea kufurahishwa na namna ambavyo wakulima hao wanaelezea kunufaika na bima hiyo huku akishauri mifumo hiyo ya bima iboreshwe zaidi ili iweze kuwafikia wakulima wengi zaidi.

 


Kwenye majadiliano hayo Mkulima mhamasishaji, Cleopa Mushi ambaye alishiriki kuhamasisha wakulima kununua vocha (bima) ili kukabiliana na majanga ya ukame na uhaba wa mvua amesema kuwa msimu ujao yeye na wakulima wenzake wamejipanga kununua vocha nyingi zaidi kwani wameona mafanio yake.

 

"Nimewahi kupata malipo ya bima ya shilingi 120,000, mimi nimeona faida ya huu mradi kwa sababu hizo fedha nilitumiwa kwenye simu yangu  wakati wa maandalizi ya msimu mwingine wa kilimo. Hivyo ikanisaidia kwa sababu msimu iliopita nilikuwa sijapata mavuno vizuri hivyo ingenilazimu kwenda kuuza vitu vingine ili niweze kuanza kuandaa shamba lakini malipo ya boma ya  ACRE Afrika yamenisaidia sana," amesema Mushi.

 

Mkulima mwingine Irene Ndenshao alisema kuwa yeye alinunua vocha moja ambayo inauzwa shilingi elfu moja kwa hofu kuwa huenda anaweza kutapeliwa hivyo baada ya msimu kuisha mavuno hayakuwa mazuri.

 

" Nilishangaa kuona natumiwa shilingi 12,000 kwenye simu yangu nikashangaa sana kwa sababu nilikuwa nimesahau kama nilikuwa nimekata bima ya mazao hivyo kwenye msimu huu nimepanga kununua vocha nyingi zaidi," alisema Ndenshao.

 


Akimkaribisha Malkia Maxima kuzungumza na wakulima hao, Mkurugenzi wa kampuni ya Acre Afrika, nchini Tanzania, Chrisopher Mazali alisema kuwa wanatekeleza mpango wa wa kutengeneza bima hapa nchini kuanzia mwaka 2015 ambapo wameanza na mikoa ya kilimanjaro na Arusha.

 

"Ujio wa Malkia Maxima hapa kwenye kata ya Uduru ulikuwa ni kuja kujifunza huduma ya bima ya mazao tunayotoa kwa wakulima wa  mahindi ambapo miradi kama hii tunaisimamia kwenye wilaya za Siha mkoani Kilimanjato  na Arumeru mkoani Arusha," alisema Mazali na kuongeza.

 

...Bima tunayotoa kwa wakulima wadogo inaitwa 'bima pima' ni bima tunayoitoa kwa mfumo wa vocha ambayo imelenga kuwatambulisha wakulima mfumo wa bima ambapo vocha moja inauzwa shilingi elfu moja.

 

Hii inalinda gharama za uwekezaji za mpaka shilingi 12,000 kwa kadi moja hivyo mkulima akipata hasara anaweza kulipwa fidia mpaka shilingi 12,000 ambapo mkulima anaweza kununua vocha zaidi ya moja kulingana na gharama anayotaka kuilinda kwenye kilimo chake,".

 

Mazali alisema kuwa wameanza kuendesha shughuli zao nchini kuanzia mwaka 2015 ambapo wamekuwa wakitumia wakulima wahamasishaji kuwaelimisha umuhimu wa bima hiyo inayolipa majanga ya ukame na mvua nyingi inayoharibu mazao.

 


"Tumejipanga kutoa bima kwa wakulima laki moja kwenye msimu ujao wa kilimo na tutafanya hivyo kwenye mikoa saba nchini. Mbali ya mahindi tutaangalia na mazao mengine kama alizeti, pamba, kahawa,tumbaku na mazao mengine yanayokabiliwa na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi," alisema Mzali.

   

 


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya mbegu ya SeedCo, kanda ya Afrika Mashariki, Clive Mugadza alisema kuwa wamejikita kuzalisha mbegu zinazohimili changamoto za tabianchi hivyo kuwawezesha wakulima kupata mavuno mengi na bora.

 


" Tunawashauri wakulima kujiunga na bima ya kilimo kwani inapotokea majanga  yanayoweza kuwasababisha wasipate mavuno ikiwemo  upungufu wa mvua basi waweze kupata fidia ikiwemo kupatiwa bure mfuko wa mbegu za mahidi kwa ajili ya msimu unaofuata," alisistiza Mugadza.

 


Naye Meneja Mkuu wa Bima, benki ya CRDB, Wilson Mzava alisema kuwa wanashirikiana na taasisi ya ACRE Afrika wameandaa mpango mzuri sana wa bima ya kilimo inayotoa fidia kwa wakulima pindi wanapokumbwa na majanga. 

 

"Bima ya mazao inayotolewa benki ya CRDB inaongeza uhakika wa chakula nchini pia inamuongezea mkulima uhakika wa kipato hivyo tunawashauri wakulima wengi kujiunga na bima hii,' alisema Mzava.

 


Naye Meneja wa CRDB kanda ya Kasikazini, Chiku Issa alisema kuwa kwa hapa nchini benki yao inaongoza kwa kutoa mikopo ya kilimo hapa nchini kwa kutoa asilimia 43 ya mikopo yote ya kilimo iliyotolewa hapa nchini.


Amesema kuwa hiyo inatokana na benki hiyo kuwajali wananchi kwani zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania ni wakulima hivyo ili benki inaunga mono juhudi za serikali katika kuwainua wananchi kiuchumi kupitia mikopo hiyo ya kilimo.

 


"Tunatoa mikopo kuanzia kwenye mbegu zinapoingia mashambani tumekuwa tunaungana na wadau ambao wanatoa pembejeo za kilimo tumekuwa tunatoa bima ya afya kwa wakulima, bima hii ni ile ya Taifa, (NHIF)



Tumekuwa tunamlipia mkulima bima awali bila yeye kutoa hata shilingi moja, akishavuna mazao yake fedha hiyo inalipwa kupitia AMCOS  yake ambapo bima hiyo huwanufaisha baba, mama na watoto wanne wa familia moja.



Mmoja wa wakulima alimweleza Malkia Maxima kuwa wameona mafanikio makubwa kupitia bima hiyo kwani imewawezesha kuhama kutoka kilimo cha mbegu za kienyeji ambacho kwenye ekari moja  walikuwa wanapata gunia nne za kilo 100 kila moja ambapo kwa sasa wananunua mbegu za kampuni ya  SeedCo zinazowawezesha kupata wastani wa magunia 25 mpaka 40 kwa ekari.

 

 

 

0 Comments:

Post a Comment