WANAHISA wa Benki ya CRDB wamepitisha kwa kauli moja mapendekezo ya Bodi ya Wakurugenzi kuhusu malipo ya gawio la Shilingi 36 kwa kila hisa ambayo yanaleta jumla ya thamani ya gawio la mwaka wa fedha 2021 kufikia Sh 94 bilioni.
Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa 27 wa Benki ya CRDB, Mwenyekiti wa Bodi ya Benki hiyo Dkt. Ally Laay alisema gawio lililoidhinishwa kwa kila hisa ni ongezeko la asilimia 64 ikilinganishwa na Shilingi 22 kwa kila hisa iliyotolewa mwaka jana.
Alisema kuwa hiyo inaashiria ukuaji wa mapato kwa kila hisa ambapo katika kipindi cha mwaka 2021 yalikuwa Shilingi 102.7.
Laay alisema kuwa a kuwa kampuni tanzu za Benki hiyo ziliendelea kuchangia vyema katika biashara ya kundi huku kampuni tanzu ya Burundi pekee ikichangia faida ya jumla ya Shilingi bilioni 12.8 huku kampuni tanzu ya bima ikichangia faida ya shilingi milioni 859 ambapo jumla ya mchango wa kampuni tanzu kwenye faida ya kundi ilikuwa asilimia tano.
"Nafurahi kuripoti kwenu kwamba tumepata maendeleo makubwa katika kupata leseni na vibali vinavyohitajika kutoka kwa mamlaka za nyumbani pamoja na DRC. Tunatarajia kuanza uendeshaji ndani ya nusu ya pili ya mwaka wa fedha wa 2022.,” alibainisha alipokuwa akiwasasisha wanahisa kuhusu upanuzi wa kimkakati wa Benki hadi DRC.
Akizungumzia utendaji wa mwaka uliopita, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema mapato ya uendeshaji ya Kampuni yaliongezeka kwa asilimia 14.3 sawa na Shilingi bilioni 924.0 kutoka Shilingi bilioni 808.7 mwaka 2020.
Alisema kuwa ukuaji huo ulitokana na ongezeko la asilimia 11.3 ya mapato ya jumla ya riba, yaliyotokana na ukuaji mzuri wa mikopo kwa wateja wadogo na wakati. Pamoja na ukuaji wa mikopo Benki hiyo lilifunga mwaka na uwiano wa mikopo chechefu wa wa asilimia 3.3 kulinganisha na kiwango cha udhibiti cha soko cha asilimia tano
Nsekela alisema Benki ya CRDB pia ilirekodi ukuaji mkubwa wa mizania wa mwaka hadi mwaka wa asilimia 23 kutoka Shilingi trilioni 7.2 mwaka 2020 hadi Shilingi trilioni 8.8. Ukuaji huo ulisababishwa na ukuaji wa asilimia 19.4 wa amana za wateja hadi Shilingi trilioni 6.5 kutoka Shilingi trilioni 5.4 zilizoripotiwa mwaka 2020, na ukuaji wa 20.6% wa fedha za wanahisa.
"Kutokana na mtazamo wetu makini katika mwaka huo, Benki yetu iliendelea kukamata masoko kwa bidhaa na huduma bunifu, hivyo kupelekea ukuaji endelevu katika mapato na faida yetu. Tuliendelea kufanyia kazi changamoto za wateja ili kuboresha utoaji wetu wa huduma na kuhakikisha tunawapa uzoefu uliobora zaidi pindi watumiapo huduma zetu,” aliongeza.
Akizungumzia kuhusu mipango ya mbeleni, Nsekela alisema kipaumbele cha Benki hiyo ni kuimarisha vichocheo vya ukuaji, na kujenga misingi imara ya uendelevu ambapo aliutangaza mwaka wa fedha wa 2022 kuwa mwaka wa mwisho wa mkakati wa muda wa kati wa Benki ya CRDB ambao ulikuwa na jukumu muhimu katika kuimarisha utendaji, na umeipa msingi mzuri benki hiyo kukabiliana na siku zijazo.
Akizungumzia malipo ya gawio hilo, aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu Mtendaji wa Benki hiyo na Mbunge wa Vunjo, Dkt. Charles Kimei, alieleza kufurahishwa kwake na kuendelea kuongezeka kwa gawio huku akibainisha kuwa ukuaji huo ni mkubwa kupata kutokea.
Dkt. Kimei alisema kuwa hisa za benki hiyo zimebakia kuwa chachu ya wawekezaji kwasababu benki hiyo haijawahi kushindwa kutoa gawio kwa Wanahisa wake.
Katika hatua nyingine, wanahisa waliidhinisha Ernst & Young kama Wakaguzi wa Nje wa Benki kwa mwaka wa fedha wa 2022, kuashiria imani yao katika sheria ya kiakili ya kampuni na kuendelea kwa Benki kuzingatia itifaki za utawala bora.

0 Comments:
Post a Comment