Kesi ya Wajumbe wa CHADEMA Zanzibar Yakwama Kusikilizwa

 


Kesi ya madai iliyofunguliwa na baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Wadhamini wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutoka Zanzibar, ikipinga kile kinachodaiwa kuwa ni ubaguzi na kutengwa kwa upande wa visiwani katika shughuli za chama hicho, imeahirishwa na sasa imepangwa kusikilizwa Julai 10, 2025 katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam.

Kesi hiyo ilitarajiwa kuanza kusikilizwa leo mbele ya Jaji Hamidu Mwanga, lakini ilishindikana baada ya Mahakama kutoa taarifa kuwa Jaji huyo hayupo kwa sababu anasikiliza kesi nyingine katika Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara. Kutokana na hali hiyo, Msajili Aziza Mbage aliiahirisha kesi hiyo hadi tarehe mpya.

Wajumbe waliowasilisha kesi hiyo ni aliyewahi kuwa Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA Zanzibar, Said Issa Mohamed, Makamu Mwenyekiti Mstaafu wa chama hicho, Ahmed Rashid Khamis, na Maulida Anna Komu.

Wakiwa mbele ya Mahakama, walieleza kuwa CHADEMA imekuwa ikiiweka Zanzibar pembeni kwenye masuala ya kiutawala na usimamizi wa rasilimali za chama, hasa fedha.
"CHADEMA kimekuwa kikiiweka Zanzibar kama mkoa wa kawaida bila kuzingatia kuwa ni sehemu yenye mamlaka kamili ya kisiasa na kiutawala," alisema Said Issa Mohamed.

Mnamo Juni 10, 2025, Mahakama hiyo ilikubali ombi la zuio la muda lililowasilishwa na wajumbe hao, ikiizuia CHADEMA kufanya shughuli zozote za kichama hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.

Katika zuio hilo, Mahakama ilielekeza kuwa:
"Katibu Mkuu wa CHADEMA, mawakala na wafuasi wa chama hicho ambao wamepewa dhamana ya kuendesha shughuli za chama, wasijihusishe kwa namna yoyote na shughuli za kisiasa hadi kesi hiyo itakaposikilizwa," ilieleza taarifa ya Mahakama.

Pamoja na hilo, Mahakama imeagiza kuwa mali zote za chama hicho, zisitumike kwa kipindi chote cha zuio hilo, hadi pale uamuzi wa mwisho wa kesi hiyo utakapotolewa.

Kesi hiyo inazidi kufuatiliwa kwa karibu na wadau wa siasa nchini, hasa kutokana na madai ya kuwepo kwa mgawanyiko wa kiuendeshaji ndani ya chama hicho kikuu cha upinzani.

0 Comments:

Post a Comment