KESI ya wananchi wa watano wa Loliondo wanaopinga tangazo la Waziri wa Maliasili na Utalii lililotumika kuwaondoa kwenye maeneo yao imepangwa kuendelea Mei 4, 2023 baada ya upande wa jamhuri kuomba muda wa kuleta mapitio ya mwanasheria wa serikali kuhusu katazo hilo.
Shauri hilo la mapitio namba 21/2022 limekuja leo Machi 14,2023 mbele ya Jaji Mfawidhi, Joachim Tiganga wa mahakama Kuu Kanda ya Arusha kwa ajili ya kutajwa.
Wakili wa Serikali, Mkama Msalama akiwasilisha ombi hilo amesema kuwa muda huo utamwezesha kukaa na watu wa Wizara ya Maliasili na Utalii ili kulipitia kwa undani tangazo hilo huku akisisitiza kuwa watu hao watapatikana muda wiki hii.
Mahakama hiyo iliridhia ombi hilo na kuwapa muda wa siku saba (mpaka Machi 21) upande wa Jamhuri kuleta mahakamani hapo kiapo kinzani cha maombi hayo ambapo upande wa waleta maombi watatakiwa kuwasilisha majibu yao ndani ya siku saba (mpaka Machi 28,2023) endapo watahitaji kufanya hivyo .
Kwenye shauri hilo wananchi hao, Latang’amwaki Ndwati , Ndalamia Taiwap, Megwari Moko, Ezekile Sumare na Latajewo Sayari wanawakilishwa na mawakili, Joseph Shangay, Denis Moses na Hamis Mayombo huku wajibu maombi Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri wa Maliasili na Utalii wakiwakilishwa na wakili wa Serikali, Msalama.
Wananchi hao wa vijiji vilivyokuwa kwenye Tarafa ya Loliondo waliofungua shauri hilo wanadai kuwa waliathirika na mchakato wa eneo hilo la Kilometa za Mraba 1,500 kutangazwa na serikali kuwa pori tengefu la Pololeti.
Wananchi hao wanaiomba mahakama itoe zuio dhidi ya tangazo la serikali namba 421 la Juni 17, 2022 kwa kuwa ni batili kwa kile wanachodai kuwa halikufuata taratibu za kisheria hivyo si halali na halipaswi kutumika.
Katika ombi lao la pili wanaiomba mahakama itamke kwamba serikali, taasisi na watu wake wasiruhusiwe kuingia kwenye eneo hilo kuendesha operesheni zao mpaka mahakama hiyo itakapotoa uamuzi wa maombi yao.
.
0 Comments:
Post a Comment