MBUNGE wa jimbo la Vunjo, Dkt, Charles Kimei ametaka gharama za kuwaunganishia maji wananchi pamoja na bei za unit za maji zipitiwe upya ili kuwajengea hamasa wananchi wengi zaidi kutaka kujiunga na huduma zao.
Ameyasema hayo leo wakati alipotembelea mamlaka zinazohusika na uzalishaji na usambazaji maji safi na salama kwa wananchi pamoja na jumuiya za watumia maji Uchira na bodi ya maji ya Kirua-Kahe.
"Kwa sasa gharama za mwananchi kuunganishiwa maji ni kubwa sana kulinganisha na hali ya uchumi waliyo nayo na hi sio dhamira ya serikali ya awamu ya tano chini ya Rais aliyejipambanua pasipo shaka kuwa mtetezi wa wanyonge Mhe Dkt Magufuli"alisema Dkt Kimei
Alisema lengo ni kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma hii ya maji safi na salama umbali usiozidi mita 400 au karibu zaidi sasa kwa gharama hizo watashindwa na watakuwa mnamkwamisha Mhe Rais na kuwa naomba wakae na kupitia upya gharama hizo.
Kimei alisema kwa kuwa teknolojia imekua siku hizi mafundi wanatakiwa kuitumia iiki kupunguza baadhi ya gharama zisizo za lazima wakati wa uunganishaji maji ili kuwasaidia wananchi hao.
Vilevile alisema bei za unit za maji sio rafiki, pamoja na idadi ya walaji wa maji kuongezeka kila siku kwa kila mamlaka bado wamekuwa wakipandisha bei kwa zaidi ya asilimia mia moja.
" Nawaomba pia hili mlitazame kwani wananchi wetu uchumi wao bado sio mzuri tuwape bei ambazo ni nafuu naamini linawezekana." Alisema Dkt Kimei.
Aidha alitembelea uboreshaji wa miundombinu ya maji ambapo kwa jumuiya ya maji Uchira walimtembeza kwenye kisima walichochimba kwa mapato yao ya ndani na kuungwa mkono na serikali kupitia RUWASA kwa kupewa takribani milioni 100 ambacho kimefungwa pampu, umeme pamoja na kuwekewa umeme wa jua 'Solar panels' ili kuwahudumia wananchi maji safi na salama.
Katika hatua nyingine Dkt Kimei aliwapongeza Mwenyekiti wa bodi ya jumuiya ya watumia maji Uchira Lazaro Mfinanga na meneja wake Mhandisi Samwel Ignas kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kupeleka huduma kwa wananchi Kama inavyostahili
Akiwa Bodi ya Kirua-Kahe ambapo alipokelewa na meneja wa bodi hiyo, Mambea Mshana ambaye alimuelezea utendaji kazi wa bodi na changamoto zake ikiwemo baadhi ya wananchi kutotaka kufungiwa mita za maji ili walipie huduma hiyo pamoja na kumtembeza kujionea uboreshaji mkubwa uliofanyika kwenye chemchem ya maji Kisanja ikiwa ni utekelezaji wa maazimio ya kikao kazi alichokutana nao Januari mwaka huu.
Akiwa katika eneo hilo Dkt Kimei aliridhishwa na uboreshaji wa miundombinu ya maji unaofanyika ambapo aliahidi kuwa mhamasishaji na mtoaji wa elimu kwa wananchi kupitia majukwaa mbalimbali atakayokuwepo jimboni juu ya umuhimu wa kufungiwa mita za maji na kulipia maji ikiwemo ni uboreshaji wa miundombinu ya maji ambayo inatoa uhakika wa wao kuendelea kupata maji safi na salama.
Aidha alisema ataendelea kuishauri serikali kupitia wizara ya maji ione umuhimu wa kutoa ruzuku hata kwenye ununuzi wa mita za maji na kuvutia uwekezaji kwenye viwanda vya kutengeneza mita hizi hapa nchini ili kumpunguzia mzigo wa gharama mwananchi ambaye anatozwa takribani shilingi laki moja kwa ajili ya ununuzi wa mita za maji wakati wa zoezi la uunganishwaji maji.
Deodatus Macha na Edwin Mtey no wananchi wa eneo la Kahe ambapo walimshuru mbunge huyo kwa kuwatembelea ili kujua changamoto zao na kuwa uongozi ni pamoja na kuwajali wananchi wako na sio kutokomea Hadi kuonekana kipindi Cha uchaguzi.
Imeandikwa na Gift Mongi


0 Comments:
Post a Comment