TAWIRI YABAINISHA MATUMIZI YA TEKNOLOJIA KATIKA TAFITI ZA WANYAMAPORI NCHINI

TAWIRI YABAINISHA MATUMIZI  YA TEKNOLOJIA  KATIKA  TAFITI  ZA WANYAMAPORI NCHINI





 


Ikiwa Kauli mbiu ya siku ya wanyamapori  duniani 3 Machi, 2024  ni "Unganisha Watu na Ulimwengu: Vumbua Matumizi  ya  teknolojia  Katika Uhifadhi  wa Wanyamapori " Taasisi  ya  Utafiti wa  Wanyamapori  Tanzania  (TAWIRI ) imebainisha matumizi ya  teknolojia yanavyorahisisha  tafiti  za wanyamapori  nchini. 



Akizungumza na Mwanahabari  wetu, Mkurugenzi Mkuu TAWIRI, Dkt. Eblate  Ernest  Mjingo  amesema teknolojia  mbalimbali  zimerahisisha  tafiti za  wanyamapori nchini kufanyika kwa wakati na kwa usahihi zaidi.


Dkt. Mjingo amebainisha miongoni mwa  teknolojia  zinazotumika katika tafiti za wanyamapori  ni pamoja na matumizi ya tekinolojia  ya akili mnemba (artificial intelligence)  kuchakata takwimu  na uchambuzi wa picha katika zoezi la kuidadi wanyama (sensa), teknolojia ya  mikanda ya visukuma mawimbi( GPS satellite Collar)  kufuatilia mienendo ya wanyamapori, matumizi ya ndege zisizo na Rubani rubani (Drone)kutatua changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu .



Pia, matumizi  ya helikopta/ndege kuwafuatilia wanyamapori kwa matibabu au kuwarejesha wanyama  maeneo ya hifadhi, kamera za kutega (camera  trap) kubaini  aina ya wanyamapori waliopo katika  maeneo mbalimbali na changamoto za uhifadhi na tekinolojia  ya vinasaba (DNA) kutambua afya ya uzazi wa wanyamapori kwenye mifumo ikolojia mbalimbali. 



Dkt. Mjingo amesema awali kabla ya matumizi ya teknolojia  kulikuwa na ugumu katika kufanya  tafiti za wanyamapori baadhi ya maeneo kwani iliwalazimu watafiti kutumia muda mrefu kufanya tafiti, kutumia gharama kubwa, usalama  mdogo .


 " kwa kutumia teknolojia  ya Akili mnemba (AI) kuchambua  picha na  kuchakata takwimu  imesaidia kutumia nusu ya siku zilizokuwa zimatumika awali sambamba na kupunguza gharama "  ameeleza Dkt. Mjingo


Vilevile  Dkt.Mjingo  amebainisha awali  ilikuwa vigumu kuwafuatlia tabia za wanyamapori kwani wanyamapori wakiona gari au watu mara nyingi hubadili tabia sambamba na ugumu kufuatilia wanyamapori  nyakati za usiku, msimu wa mvua na maeneo yasiyo  fikika ambapo kwa sasa teknolojia  ya kamera za kutega (camera  trap) inatumika nyakati za mchana na usiku. 


Aidha, Dkt.Mjingo ametoa wito kwa wadau   wa uhifadhi  na  utalii ndani  na  nje  ya  nchi  kushirikiana  na  TAWIRI kwa  kuzingatia tafiti za  wanyamapori  ni muhimu  katika  sekta ya uhifadhi  na  utalii  nchini ambapo  pia ametoa  wito kwa mamlaka  za uhifadhi  kutumia  ushauri  wa kisayansi unaotokana na  matokeo  ya tafiti  mbalimbali.

0 Comments:

Post a Comment