EXCLUSIVE: Upo hapa WARAKA wa NDESAMBURO kwa Raid JPM

NA DK. PHILEMON NDESAMBURO
Mh. Philemon Ndesamburo
"RAIS Dk. John Magufuli alishasema serikali yake ni ya kubana matumizi. Suala la kubana matumizi kwa serikali, taasisi, familia na mtu binafsi ni la kawaida sana lakini ni muhimu.


Kubana matumizi ni njia ya kuonesha nidhamu katika kutumia fedha za walipa kodi. Kwa misingi hii, kitu kikubwa kinachozingatiwa katika kubana matumizi ni nidhamu na uadilifu. Kubana matumizi kunaweza kutokana na sababu kadhaa;



Moja, ni ukosefu wa raslimali fedha. Serikali hulazimika kubana matumizi kama haina rasilimali fedha au zilizopo hazitoshi kulingana na mahitaji yaliyopo.


Pili,Serikali inaweza kubana matumizi kutokana na kuishiwa mapato huku matumizi yakiwa makubwa.
Nidhamu ya kubana matumizi inapaswa kuzingatiwa zaidi na serikali za nchi maskini. Lakini pia serikali zingine duniani hubana matumizi licha ya kuwa na mapato makubwa ya kujitosheleza.


Kutokana na utafiti wangu wa kutaka kujielimisha zaidi juu ya dhana ya kubana matumizi serikalini, nimegundua kuwa viongozi wengi duniani huwa wanatekeleza dhana ya kubana matumizi kwa kuondoa matumizi yasiyo ya lazima kwa serikali.



Matumizi yasiyo ya lazima kwa serikali ni pamoja na posho na matumizi ya anasa kwa viongozi.
Kwa hiyo, ili kubana matumizi, fedha zilizokuwa zitumike kwenye maeneo yasiyo ya lazima zinaelekezwa kwenye kuhudumia mahitaji ya wananchi.


Baada ya hapo, nikajaribu kuainisha maeneo ya kuyaangalia ili kujua serikali inabanaje matumizi. Eneo muhimu ambalo nina uhakika linaweza kusaidia kubana matumizi ni kupunguza ukubwa wa serikali na Bunge.



Nchi nyingi, hasa maskini ikiwemo Tanzania, ukubwa wa serikali na Bunge ni maeneo ambayo ni mzigo kwa walipa kodi kutokana na kuongeza matumizi ya serikali na hivyo kutafuta fedha nyingi.
Kwa Tanzania, ukubwa wa serikali unaotokana na mambo makuu mawili; moja ni ubovu wa Katiba tuliyonayo na pili ni tabia ya kugawana madaraka kwa kuangalia urafiki,undugu na uhusiano wa kivyama.
Viongozi wetu wamekuwa wakitumia ubovu wa Katiba kugawana vyeo. Kwa mfano,serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli inadaiwa kugawa vyeo vya uteuzi kwa watu wengi ambao ni wana CCM walioshindwa kwenye uchaguzi wa kura za maoni ndani ya chama hicho au kwenye uchaguzi mkuu wa 2015.



Kwa kweli, Rais Magufuli kama ilivyokuwa kwa mtangulizi wake, anaongoza serikali kubwa sana ambayo ikipunguzwa itasaidia kubana matumizi.
Idadi ya wabunge nayo ni kubwa sana. Hali hii, haiendani kabisa na kauli ya kubana matumizi. Serikali kubwa, matumizi nayo makubwa. Hakuna sababu kwa Tanzania nchi maskini kuwa na bunge kubwa karibu sawa na Uingereza nchi tajiri na yenye uchumi mkubwa.



Rais Magufuli ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa amefanya mabadiliko kwenye chama chake yaliyopunguza idadi ya wajumbe kwenye vikao vya Halmashauri kuu na mkutano mkuu. Hatua hii inapunguza mzigo wa gharama ya kufanya vikao.



Ninadhani, dhamira hii ihamishiwe kwenye serikali anayoiongoza ambayo ni kubwa sana.
Kwenye chama chake amefanya mabadiliko yaliyopunguza ukubwa wa Kamati Kuu kutoka wajumbe 34 hadi 24, hali inayofanya wanaoingia kwa kupigiwa kura kupungua hadi wanne kutoka 10.
Aidha, nafasi za ujumbe wa Halmashauri Kuu zimepungua kutoka 388 hadi 158, huku wengi wakiingia kwa nafasi zao na wajumbe kutoka wilayani wameondolewa.



Haya ndiyo yaliyoitwa mabadiliko ndani ya CCM yaliyopachikwa jina la mtu mmoja cheo kimoja.
Kupunguza ukubwa wa halmashauri kuu na kamati faida yake inaonekana kwenye kupungua gharama.
Haya ameyafanya kwenye ngazi ya chama. Naona ni vema Rais aangalie pia juu ya kupunguza ukubwa wa serikali na Bunge ili kuendana na dhana ya kubana matumizi.


 Namshauri afanye yafuatayo:
Mosi, Rais magufuli aangalie uwezekano wa kuondoa nafasi za wakuu wilaya na mikoa. Nafasi hizi za kuteuliwa zikiondolewa, hakuna athari zozote katika utekelezaji wa majukumu ya mkoa na wilaya.


Kwa mfano kwenye ngazi ya wilaya kuna watu watatu wa kuteuliwa; mkuu wa wilaya, mkurugenzi na katibu tawala wilaya utawala(DAF)
Kwenye ngazi ya mkoa kuna mkuu wa mkoa na Katibu Tawala Mkoa (RAS). Watu wote hao wanafanya kazi ambazo zinafanana kwa karibu.



Ninafikiri, ili kubana matumizi Magufuli afikirie kuondoa nafasi za wakuu wa wilaya na mikoa.Majukumu yao wanaweza kupewa makatibu tawala.



Pili, Rais Magufuli aangalie uwezekano wa kuondoa nafasi za unaibu waziri kwenye wizara. Kwa kuwa kila wizara ina kKatibu na watendaji wengine.Majukumu haya yanaweza kufanywa na Katibu na wasaidizi wengine kwenye wizara husika.


Mwisho namshauri Rais Magufuli arejee kwenye mapendekezo ya iliyokuwa Tume ya mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na jaji mstaafu Joseph Warioba.
Ni mapendekezo yanayozingatia kupunguza ukubwa wa serikali na Bunge. Kwa mfano mapendekezo ya Bunge la shirikisho kuwa na wabunge 75 yana mashiko katika kupunguza matumizi.



Akiyafanya haya ile kauli yake ya “ninabana matumizi” itakuwa na maana. Wahenga walisema matendo hukidhi haja maridhawa kuliko maneno.



Mwandishi wa makala ni Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Kilimanjaro, Mbunge mstaafu wa jimbo la moshi mjini"

0 Comments:

Post a Comment