tacri yapongezwa kwa jitihada za kuiwainua wakulima kiuchumi

MKUU wa Wilaya Moshi, Dkt. Ibrahimu Msengi ameipongeza Taasisi ya Utafiti wa Kahawa nchini, (TaCRI) kwa jitihada  zake inazofanya kwa kushirikiana na halmashauri za wilaya nchini  katika kufufua zao la kahawa kwa lengo la kuimarisha kipato cha wakulima wa zao hilo.

Aliyasema hayo wakati akizindua kampeni ya ugawaji miche ya kahawa katika kijiji cha Manushi Ndoo ikiwa ni mwendelezo wa zoezi la ugawaji micho linalofanywa kwa pamoja kati ya halashauri ya wilaya ya Moshi na TaCRI.



Dkt. Msengi  alisema kuwa jitihada hizo si za kupuuzwa bali zinapaswa kuigwa na halmashauri nyingine nchini kwani mbali na kuwanufaisha wakulima pia itakuza uchumi wa Taifa kwani mbali ya kuwaongezea kipato wakulima pia huliwezesha Taifa kupata fedha za kigeni baada ya kahawa hiyo kuuzwa kwenye soko la dunia.

Alisema kuwa pamoja na wakulima wengi wa
kahawa kukata tamaa kutokana na changamoto mbalimbali zinazolikabili zao hilo ikiwemo kushuka kwa bei,  TaCRI  bado imekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha wakulima wanandeleza kilimo hicho.

Mkuu huyo wa wilaya alisema kuwa  zao la kahawa bado lina thamani kubwa huku akibainisha kuwa kushuka kwa bei ni changamoto ambayo inaweza kutokea katika biashara yoyote hivyo wasikate tamaa.


Aliwataka wakulima hao kuendelea kulitunza na kulienzi zao hilo ili kuiwezesha kujirudia kwa historia ya miaka ya nyuma wakati zao hilo likijulikana kama mkombozi wa wakulima mkoani Kilimanjaro.


Hata hivyo Dkt. Msengi  aliwashauri halmashauri hiyo ya Moshi kuangalia uwezekano wa kuacha kutoa miche bure kwa wananchi badala yake iwahamasishe wananchi kuchangia fedha kidogo, hatua ambayo itawapa uchungu na kuwafanya waitunze.

“Tengenezeni utaratibu wa kuwafanya wananchi wanunue miche hii, msiwape bure ili waweze kuitunza vizuri na kufanikisha malengo ya
serikali ya kufufua zao la kahawa, kwani uzoefu umeonyesha kuwa vitu vya bure huwa havithaminiwi, hivyo kuwapa miche hii bure wanaweza
wakajisahau na wasiitunze”alisema Mkuu huyo wa Wilaya.


Kwa upande wake Mtafiti wa usambazaji teknolojia na mafunzo kutoka TaCRI, Jeremiah Magesa, alisema kuwa endapo halmashauri zote nchini
zitaiga mfano wa halmashauri ya wilaya ya Moshi, katika kipindi cha miaka mitano, nchi itakuwa na ongezeko kubwa la uzalishaji wa kahawa.

Hata hivyo alishauri halmashauri hiyo wakati wakiendelea kugawa miche wahakikishe wataalam wa kilimo wakiwemo maafisa ugani wawe wanatoa elimu kwa wakulima wa kahawa juu ya kilimo bora cha zao hilo jambo alilodai litawawezesha kulima kitaalamu na kuongeza thamani ya mazao yao.

Magesa aliwasisitiza wakulima wa kahawa nchini kutokatishwa tamaa na kushuka kwa bei ya kahawa kwenye soko la dunia kwani kahawa ni zao endelevu na kipindi hiki ni cha mpito kitapita, na kitaingia kingine ambacho bei itakuwa juu kama inavyotokea mara kwa mara hivyo akawataka waendelee kulima kahawa bora na kwa kuzingatia ushauri toka kwa wataalam wa zao hilo.

0 Comments:

Post a Comment