MIKOA ya Arusha, Temeke, Kinondoni, Tanga na Dodoma imekuwa ikiongoza kwa vitendo vya ukatili kwa kijinsia, watoto na walemavu kwa kipindi cha miaka mitano.
Aidha kwa jumla ya wanawake zaidi ya 30 wameuawa na wenza wao kutokana na ukatili wa majumbani na ukatili wa wenza kwa mwaka 2021.
Hayo yalisemwa leo May 9, 2022 Kaimu mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha sheria na haki za binadamu,(LHRC), Fulgence Massawe akiongea wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku tatu ya kuwajengea uwezo waendesha mashitaka kutoka mikoa ya Arusha, Mwanza na Kigoma.
Amesema kuwa ripoti hiyo imeelezea pia kuongezeka kwa ukatili wa kimwili, ndoa za utotoni pamoja na ukeketaji ambapo mikoa iliyoripotiwa kuongoza kwa ukatili wa watoto ni pamoja na Arusha, Tanga, Shinyanga, Mwanza na Ilala.
"Kumekuwa na changamoto mbalimbali katika utekelezaji na ulinzi wa watoto wanaokinzana na sheria, watoto wanaoingiliana na sheria pamoja na Watoto waathirika wa ukatili ambapo upatikanaji haki kwao umekuwa changamoto mara nyingi," alisema Massawe na kuongeza
...Kumekuwa pia na changamoto katika upatikanaji haki kwa wahanga wa vitendo vya Ukatili wanawake kwa wanaume,".
Kaimu Mkurugenzi huyo wa LHRC amesema kuwa waendesha mashtaka ni wadau muhimu sana katika upatikanaji haki wa wanawake, Watoto Pamoja na watu wenye ulemavu.
Amesema LHRC wakaona ni vema wanatakiwa wajengewe uwezo kutambua sheria, miongozo na mienendo ya ulinzi wa haki za Watoto, haki za wanawake, huduma na haki za watu wenye ulemavu ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Akifungua mafunzo hayo, Katibu Mmkuu Wizara ya Sheria na Katiba, Mary Makondo amesema wizara hiyo inajukumu kubwa la kusimamia mfumo mzima wa haki jinai nchini katika kufanya marekebisho ya sheria na sera zinazosimamia mfumo huo .
Amemtaka mwendesha mashtaka wa serikali kuzidisha kutoa fursa za kuwapatia mafunzo zaidi na wajibu , waendesha mashtaka nchini ili kuwajengea uwezo waweze kutenda majukumu yao kwa haki na weredi mkubwa.
"Tanatarajia mtajifunza zaidi namna ya kutatua changamito ya ucheleweshaji na uendeshaji wa mashauri ili kupunguza mrundikano wa mashauri mahakamani na msongamano wa mahabusu magerezani"amesema
Naye, Mkurugenzi wa mashitaka nchini, (DPP), Sylvester Mwakitalu aliwataka waendesha mashtaka kusimamia vema haki wakati wakiendesha mashauri ya kijinsia mahakamani na kuleta matokeo chanya na yenye tija .
Alisema tatizo la ukatili kwa mwanamke na watoto bado ni kubwa sana hapa nchini kuliko takwimu zinazotajwa kwa sababu mengi hayatolewi taarifa katika vituo vya polisi hivyo kwa waendesha mahistaka kunahitaji umahili na weredi mkubwa.
"Mimi nitafuatilia kwa waendesha mashtaka mmoja mmoja na nitafika kila mkoa na wilaya ili kuona waendesha mashtaka mnavyosimamia mashauri hayo ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto, "alisema DPP.
LHRC imeungana na Wizara ya katiba na Sheria kuwajengea uwezo waendesha mashtaka takribani 100 hapa nchini na lengo letu ikiwa kufikia takribani waendesha mashtaka wote Tanzania nzima.
Mafunzo haya yanalenga kuwajengea waendesha mashtaka uwezo kwenye masuala ya haki jinai kwa mtoto, huduma kwa watu wenye ulemavu, kanuni za mahakama za watoto wanaokinzana na sheria.
Pia watafundishwa juu ya wajibu wa waendesha mahakamani katika ulinzi wa wanawake , Watoto na watu wenye ulemavu, Jinsia na Ukatili wa Kijinsia, masuala ya ushahidi, ulinzi wa Watoto na wanawake .
Pia wahanga wa ukatili Mahakamani, masuala ya haki za Binadamu, jinsia na haki za wanawake pamoja na kujadili changamoto mbalimbali katika ulinzi na utekelezaji wa haki za wanawake, watoto pamoja na watu wenye ulemavu kulingana na majukumu yao.



No comments:
Post a Comment