Umoja wa Mataifa umesema unahitajia dola milioni 900 za Marekani kufikia mwishoni mwa mwaka huu kwa ajili ya kunusuru maisha ya raia milioni 6 wa Somalia wanaohitajia misaada ya dharura ya kibinadamu.
Akiongea katika ufunguzi wa Kongamano la Kimataifa kuhusu Somalia linalofanyika katika mji mkuu wa Uingereza, London hii leo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres amesema Wasomali milioni 6 wanahitajia misaada ya kibinadamu haraka iwezekanavyo, wakiwemo watoto wadogo zaidi ya laki 2 na 75 elfu, wanaosumbuliwa na utapiamlo na lishe duni.
Rais wa Somalia Mohammed Abdullahi Farmajo (Karikati) |
Taarifa ya Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa UNICEF iliyowasilishwa katika kongamano hilo ambalo mwenyeji wake ni Waziri Mkuu wa Uingereza, Theresa May imesema kuwa, raia milioni 2.9 wa Somalia wataendelea kuishi katika maeneo yanayokumbwa na ukame na baa la njaa hadi kufikia Juni mwaka huu, na hali hiyo inatazamiwa kuzidi kuwa mbaya iwapo hatua za dharura hazitachukuliwa.
Rais wa Somalia Mohamed Abdullahi Farmajo ameliambia kongamano hilo kuwa, atafanya juu chini kuona anatekeleza yale yote aliyoyaahidi katika kampeni za uchaguzi wa rais, hususan kupambana na maadui watatu wakuu wa taifa hilo ambao ni ugaidi, njaa na ufisadi.
0 Comments:
Post a Comment