BENKI ya CRDB imepata faida ya shilingi Bilioni 387 kabla ya kodi ukilinganisha na Shilingi Bilioni 236 waliyopata mwaka 2020.
Aidha faida hiyo imesababisha ongezeko la faida kwa hisa moja kuongezeka kufikia shilingi 36 kutoka shilingi 22 kwa hisa iliyotolewa mwaka uliopita ambapo ongezeko hilo ni sawa na asilimia 64.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela ameyasema hayo leo Mei 18, 2022 jijini Arusha wakati akizungumzia maandalizi ya mkutano mkuu wa 27 wanahisa utakaofanyika Mei 21, 2022 jijini hapa.
Amesema kuwa wamefanikiwa kupunguza mikopo chechefu kutoka asilimia 9 hadi 3 kwa mwaka 2019 hadi 2022.
"Nakupitia hilo tumefanikiwa kupunguza riba kwa kuangalia sekta muhimu inayoleta tija kubwa kwenye uchumi wa nchi ambayo ni kilimo,"amesema Mkurugenzi huyo.
Nseleka alisema lengo ni kugusa watu wengi walio kwenye sekta nzima ya kilimo ambapo wakulima wengi watafaidika na huduma wanazotoa wao kama benki ya CRDB.
Amesema mkutano huo pia utafanyika kidjitali “Hybrid Meeting” ili kutoa fursa kwa wanahisa wengi zaidi kushiriki kwani sio wote wanaweza kufika Arusha siku hiyo.
“Kwa kuzingatia uzoefu tulioupata kwa kufanya mkutano wa 26 ambao ulifanyika kwa mara ya kwanza kwa kwa njia zote mbili. Mwaka jana Wanahaisa walipitisha kuendelea kutumia njia zote mbili za kuendesha mkutano kwa mwaka huu 2022,” alisema Nsekela.
Amesema mtandaoni Wanahisa wataweza kujiunga kuanzia saa 2:00 asubuhi kupitia link https://escrowagm.com/crdb/login.aspx au kupitia SimBanking App, ambapo imewekwa sehemu ya ya kujisajili kushiriki Mkutano Mkuu.
“Tumeweka muongozo wa jinsi ya kushiriki mkutano mkuu kwa njia ya mtandao kupitia tovuti yetu ya www.crdbbank.co.tz, mitandao yetu ya kijamii, lakini pia maelekezo yametumwa kwa ujumbe mfupi kwa Wanahisa,” alisema Nsekela .
Amesema ajenda mbalimbali zitajadiliwa katika Mkutano Mkuu huo ikiwa ni pamoja na uchaguzi wa wajumbe wa bodi, kuteua wakaguzi wa hesabu, na kujadili na kupokea Taarifa ya Bodi ya Wakurugenzi, na Taarifa ya Hesabu zilizokaguliwa.
MWIGULU MGENI RASMI
Mkutano Mkuu wa 27 wa Wanahisa wa Benki ya CRDB utatanguliwa na semina maalum kwa wanahisa yake ili kukuza uelewa wa masuala mbalimbali ya fedha na uwekezaji katika masoko ya mitaji.
Semina hiyo itafanyika siku ya Ijumaa tarehe 21/05/2022 kuanzia saa 3 asubuhi katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC) ambapo Waziri wa Fedha na Mipango, Mwigulu Nchemba anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Kwenye semina hiyo mada mbalimbali zitawasilishwa na wataalamu wa masuala ya fedha, sheria na uwekezaji katika masoko ya mitaji.
kauli mbiu ya Mkutano wa mwaka huu ni “Thamani Endelevu”, ambapo Mkurugenzi wa Mawasiliano wa benki hiyo, Tully Mwambapa anasema inaelezea ni kwa namna ambavyo Benki yetu imekuwa ikiimarika katika utendaji, na hivyo kupelekea ukuaji.
“Kama ambavyo ameeleza Mkurugenzi Mtendaji mwaka huu Bodi imekuja na pendezeko la gawio la Shilingi 36 kwa hisa sawa na ongezeko la asilimia 64, hii ni kiashiria tosha kuwa kumekuwa na thamani endelevu katika uwekezaji wa Wanahisa wetu,” anasisitiza Mwambapa.


No comments:
Post a Comment