Tuesday, March 29, 2022

KONGO YAINGIA RASMI EAC, MENGI YATARAJIWA

 


Mkutano wa 19 wa wakuu wa nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki unafanyika leo Machi 29, 2022 huku ajenda kuu ikiwa ni kuiidhinisha rasmi nchi ya Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo kuwa mwanachama mpya wa jumuiya hiyo kongwe barani Afrika.

Congo iliomba kujiunga na jumuiya hiyo tangu mwezi Februari mwaka 2021 na mamlaka husika zilikuwa bado zinapitia ombi hilo kwa kuzingatia mkataba wa kuanzishwa kuwa jumuiya ya Afrika Mashariki.

 

 Awali katika mkutano wa 18 wa wakuu wa nchi uliofanyika mwaka jana , katibu mkuu wa jumuiya ya Afrika Mashariki   Dr. Peter Mathuki alibainisha kuwa mwezi Machi mwaka huu hatua zote za Congo kujiunga na jumuiya hiyo, zitakuwa zimekamilika.

 

Kikao kilichotangulia cha  baraza la mawaziri wa jumuiya hiyo , kimependekeza kwamba  wakuu wa nchi katika mkutano wao wa leo, wazingatie ripoti ya timu ya uhakiki kuhusu maombi ya jamhuri ya kidemokrasi ya Congo ya  kujiunga na jumuiya hiyo.

 

Katibu mkuu wa umoja wa mataifa Antonio Guterres aliwahi kutoa wito kwa nchi duninai kuimarisha ushirikiano wa kimataifa wa kikanda na hata kiulimwengu, na hivyo jumuiya ya Afrika Mashariki inachukua wigo wa kupanua uanachama wake kutoka nchi sita hadi kufikia saba.

 

Pamoja na mambo mengine, mkataba wa kuanzishwa kwa Jumuiya  ya Afrika Mashariki unaeleza kuwa, nchi nyingine inaweza kujiunga na Jumuiya hiyo iwapo itaungwa mkono na nchi wanachama na iwapo nchi hiyo inayoomba itakuwa imetimiza masharti yafuatayo ya uongozi bora, Demokrasia, inaheshimu sheria, inasheshimu haki za binadamu, na kwamba iwe jirani na mojawapo ya nchi wanachama.   

Mpaka sasa jumuiya ya Afrika Mashariki inaundwa nan chi sita, ambazo ni Kenya, Tanzania, Burundi, Rwanda, Uganda na Sudan kusini iliyojiunga mwaka 2016. 

 

 Maamuzi hayo yanakuja kufuatia mapendekezo ya kikao cha baraza la mawaziri kilichoketi tarehe 25 Machi kwamba Congo imekidhi vigezo vya kujiunga na jumuiya hiyo kongwe barani Afrika.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

WAKUU wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, (EAC),  wameidhinisha kuingizwa kwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo katika umoja huo.

 

Wamefikia muafaka huo katika mkutano wao wa kilele uliofanyika leo Machi 29,2022  kwa njia ya mtandao ambapo baada ya Kongo kujiunga na jumuiya hiyo inakuwa na nchi saba.

 

"Waheshimiwa maraisi ninapenda kutumia fursa hii kuwashukuru sana kwa kunikaribisha katika mkutano huu maalumu ambapo kwa mara ya kwanza ninazungumza kwa niaba ya wananchi wa Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo kama mwanachama mpya wa jumuiya ya Afrika Mashariki,” amesema rais Tshisekedi.

 

Pamoja na mambo mengine Tshisekedi amesema anatarajia kwamba kuwa ndani ya jumuiya ya Afrika Mashariki kutaisaidia nchi yake kuwa na ulinzi na usalama hasa eneo la Mashariki mwa Congo ambalo linakumbwa na machafuko.

 

Wachambuzi wa masuala ya kimataifa wanadai kuwa Kongo imekuwa mwanachama rasmi wa EAC lakini hakuna mengi yanayoweza kubadilika mara moja.

 

Taifa la Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo lipo kusini mwa jangwa la Sahara lina watu wanaofikia milioni 90 na ni taifa la pili kwa ukubwa barani Afrika baada ya Algeria iliyoko kaskazini mwa Afrika.

 

Katika kikao cha leo,  wakuu wa nchi kwa pamoja wameikaribisha Congo na kuonesha matarajio ya kila upande kufaidika, Kama anavyoeleza Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan.

 

"Tanzania inasema karibu sana DRC. Ni matumaini yangu kwamba DRC inauharakisha mchakato wa kukamilisha makubaliano yaliyo katika mkataba wa kujiunga, ili kuwapa

wananchi wake fursa ya kufurahia matunda ya jumuiya. Maamuzi yenu ya kujiunga na jumuiya yatasaidia kupatikana na amani na ulinzi, umoja na mshikamano sio tu Congo bali kwa jumuiya nzima kwa ujumla.” Amesema Samia.

 

Kwa sasa Jumuiya ya Afrika Mashariki imepanuka kutoka umoja unaoundwa na nchi sita na kuwa saba hivyo unatarajiwa kuwa wigo mpana zaidi wa kibiashara kuanzia bahari ya hindi mpaka ya atlantiki.

 

Katibu Mkuu wa EAC, Peter Mathuki amesema amefurahi sana huku akitoa  wito wa  kuondolewa kwa vikwazo vyote vya kibiashara baina ya nchi wanachama.

 

"Sisi ni majirani na DRC, lakini hatufanyi biashara nayo sana kwa sababu tu hakuna mfumo. Bidhaa nyingi zinazokuja DRC zinatoka nje ya Afrika Mashariki kama vile Zambia na Asia," Mathiki amewaeleza waandishi wa habari mara baada ya kikao hicho cha wakuu wa nchi na kuongeza.

 

…Kwa hiyo, tunatazamia kuweka utaratibu ambao utahakikisha biashara kati yetu na DRC inaimarika." Amesema Mathuki

 

 

Wabunge wa Kongo bado wanapaswa kuidhinisha sheria na kanuni za EAC kabla ya kuanza kutumika.

 

Raia wa Kongo wanaotaka kutembelea nchi nyingine wanachama - Burundi, Kenya, Rwanda, Sudan Kusini, Tanzania na Uganda - bila visa wanaweza kuhitaji kusubiri kwa muda mrefu zaidi kwa sababu ushirikiano kamili katika EAC unaweza kuchukua miezi au hata mwaka.

 

Sudan Kusini ilichukua muda wa miezi minne kutoka kwa mkataba wa jumuiya mwezi Aprili 2016 hadi kuwa mwanachama kamili wa EAC mwezi Agosti mwaka huo.

 

 

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ilituma maombi ya uanachama mwaka wa 2019, ikitumai kuboresha uhusiano wa kibiashara na kisiasa na majirani zake wa Afrika Mashariki.

 

 

Kongo inapakana na wanachama wote wa EAC isipokuwa Kenya, na inatumai kuvutia wawekezaji zaidi kutoka kanda hiyo hivyo kujiunga na EAC  kunaipa nchi hiyo ufikiaji bora wa vifaa kama vile bandari za Bahari ya Hindi za Dar es Salaam na Mombasa.

 

 

 

Kinadharia, nchi za Afrika Mashariki zinaweza kupata ufikiaji wa Afrika Magharibi na Bahari ya Atlantiki kupitia DR Congo, lakini mitandao ya barabara na reli ya nchi hiyo itahitaji kuboreshwa kwa kiwango kikubwa kwanza.

 

 Njia pekee ya kuvuka nchi hii kubwa, ambayo ni theluthi mbili ya ukubwa wa Ulaya Magharibi, kwa sasa ni kwa ndege.

Upanuzi huu unaowezekana wa uhusiano wa kibiashara kutoka Bahari ya Hindi hadi Atlantiki utasaidia kupanua uwezo wa kiuchumi wa kanda wakati ambapo bara hili linafanya kazi ya kutekeleza Mkataba wa Biashara Huria wa Bara la Afrika (AfCFTA)

 

 

 

Kwa sasa Kiingereza na Kiswahili ndizo lugha rasmi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, ingawa kumekuwa na mazungumzo kuhusu kuanzisha Kifaransa, ambacho kinazungumzwa nchini Rwanda na Burundi.

 

Lugha rasmi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ni Kiswahili, Kifaransa, Kilingala, Kituba (Kikongo) na Tshiluba ambapo wataalamu wanasema asili ya lugha nyingi katika eneo hili inapaswa kuangaliwa kama fursa na sio kizuizi.

 

Kumekuwa na msukumo wa kukuza matumizi makubwa ya Kiswahili, hasa baada ya Umoja wa Afrika kukipitisha kama lugha rasmi ya kazi mwezi Februari 2022.

 

Hata hivyo, baadhi ya mikoa kama vile Magharibi mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na sehemu za mataifa mengine ya EAC haizungumzi kiswahili

 

 

No comments:

Post a Comment