Wednesday, January 15, 2014

MAIGE ADAI WIZARA YA MALIASILI NI YA KUCHINJA MAWAZIRI

MBUNGE wa Msalala, Ezekiel Maige, (CCM)  amesema kuwa mifumo mibovu ya uendeshaji iliyopo Serikalini inasababisha baadhi ya wizara kukumbwa na misukosuko ambapo imefikia hatua  Wizara ya Maliasili na Utalii inafahamika kama ya  “kuchinja” mawaziri na  na ile ya Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI kuwa ya kutia Mawaziri “kashikashi”.

Aliyasema hayo jana jijini hapa mara baada ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa, (LAAC) kupokea taarifa ya halmashauri ya jiji la Arusha.

Maige ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii kabla ya kujiuzulu huku akilalamika kuonewa alisema kuwa mifumo iliyopo kwa sasa haiwawezeshi Mawaziri au Makatibu Wakuu kujua utendaji wa wafanyakazi walio chini yao ili kuwawezesha kuwapandisha vyeo kutokana na utendaji badala yake hufanya maamuzi kwa kuzingatia majungu wanayopelekewa.

Alisema kuwa ni vema suala la nidhamu ya wafanyakazi likazingatiwa katika jitihada za kukabiliana na tatizo la ubadhirifu wa fedha za umma ambapo alishauri ni vema ofisi ya mkuu wa mkoa ikatumika kama ngazi ya nidhamu kwa watendaji wa halmashauri zilizopo kwenye mkoa husika badala ya mamlaka hayo kuwa wizarani.

“Haiwezekani mtu akafuja fedha kwenye halmashauri halafu akatakiwa kubeba nyaraka zake akajieleze kwenye mamlaka yake ya nidhamu iliyopo Dodoma, ndiyo tunaona wanaenda kule badala ya kuwajibishwa wanatoa rushwa wanahamishiwa halmashauri nyingine” alisema Maige.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa TAMISEMI, Kasim Majaliwa aliwataka wakurugenzi wote nchini kuhakikisha wanawaelimisha watumishi wao waliokaribia kustaafu kuhakikisha wanarudisha fedha za mishahara zitakazowekwa kimakosa kwenye akaunti zao pindi wanapostaafu.

“Waelimisheni wastaafu wakiona wamestaafu lakini mshahara unaendelea kuingia kwenye akaunti zao ni vema wakazirudisha vinginevyo watakuja kukatwa fedha hizo kwenye malipo ya mafao yao ya mwisho” alisema naibu Waziri huyo.

Alipongeza uamuzi wa Halmashauri ya jiji la Arusha kwa mkakati waliyojiwekea wa kuhakikisha nyumba za udongo zinaondoka katikati ya jiji ambapo alishauri halmashauri nyingine kuiga mfano huo na kwenda mbali zaidi kwa kuangalia uwezekano wa kuwakopesha ili waweze kujenga nyumba bora za kuishi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Rajab Mbaruku alisema kuwa wajumbe wa kamati hiyo wamejikita katika kutafuta matatizo yaliyopo kwenye halmashauri hiyo ili waweze kuishauri serikali namna ya kuboresha na si kupiga kelele.

No comments:

Post a Comment